Friday, December 25, 2015

RAIS MAGUFULI AUNGANA NA WAKRISTO KUADHIMISHA SIKUKUU YA KRISMASI

JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA
KURUGENZI YA MAWASILIANO YA RAIS IKULU
Simu: 255-22-2114512, 2116898
E-mail: press@ikulu.go.tz
Tovuti : www.ikulu.go.tz               

Faksi: 255-22-2113425



OFISI YA RAIS,
      IKULU,
 1 BARABARA YA BARACK OBAMA,  
11400 DAR ES SALAAM.
Tanzania.
 

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe Magufuli ameungana na watanzania wote kuadhimisha Sikukuu ya Krismasi ambayo wakristo wote duniani huadhimisha siku ya kuzaliwa Yesu Kristo, zaidi ya miaka 2000 iliyopita.

Rais Magufuli na Mkewe Mama Janeth Magufuli wamesali ibada ya Krismasi katika misa takatifu iliyofanyika katika Kanisa la Mtakatifu Petro lililopo Oysterbay Jijini Dar es salaam.

Akitoa salamu za Krismasi baada ya kukaribishwa na Askofu Mkuu wa Jimbo Kuu Katoliki la Dar es salaam Mhadhama Kadinali Polycarp Pengo, Rais Magufuli amewatakia heri watanzania wote katika sikukuu hii ya Krismasi na kuwataka waishi kama ambayo Yesu Kristo aliishi, na kwa kutekeleza yote ambayo aliyafundisha.

Ametoa wito kwa watanzania kuishi kwa amani, upendo na Mshikamano huku wakizingatia kufanya kazi, hasa wakati huu ambapo yeye mwenyewe anahamasisha uchapa kazi kupitia kauli mbiu ya "Hapa Kazi Tu"

Rais Magufuli pia amewataka wakristo wote kuungana kuliombea taifa, kuwaombea viongozi na kuwaombea watanzania wote ili waweze kutimiza majukumu yanayowakabili.

"Ndugu waumini wenzangu, mimi ni yuleyule, nipo vilevile na nimekuja hapa kama Mkristo wa kawaida, muendelee kuliombea taifa hili na mtuombee pia sisi viongozi wake" Amesisitiza Rais Magufuli

Gerson Msigwa
Kaimu Mkurugenzi wa Mawasiliano, IKULU
25 Desemba, 2015

No comments: