Wednesday, December 30, 2015

BARAZA LA TAIFA LA UJENZI LAPOKEA MIGOGORO 41 NA KUFANIKIWA KUITAFUTIA UFUMBUZI KATIKA KIPINDI CHA MWAKA 2015

Mtendaji Mkuu wa Baraza la Taifa la Ujenzi Mhandisi Dkt. Leonard Chamuriho akizungumza na waandishi wa habari leo Jijini Dar es salaam kuhusu Baraza hilo lilivyofanikiwa kutatua migogoro kwa kushirikiana na wadau wa sekta ya Ujenzi nchini.
Baadhi ya waandishi wa habari wakimsikiliza Mtendaji Mkuu wa Baraza la Taifa la Ujenzi Mhandisi Dkt. Leonard Chamuriho leo Jijini Dar es salaam kuhusu Baraza hilo lilivyofanikiwa kutatua migogoro kwa kushirikiana na wadau wa sekta ya Ujenzi nchini.


Frank Mvungi- Maelezo

Baraza la Taifa la Ujenzi limepokea migogoro 41 na kufanikiwa kuitafutia ufumbuzi katika kipindi cha mwaka 2015 kwa kushirikiana na wadau wa sekta ya Ujenzi nchini.

Hayo yamesemwa na Mtendaji Mkuu wa Baraza la Taifa la Ujenzi Mhandisi Dkt. Leonard Chamuriho wakati wa mkutano na waandishi wa habari leo Jijini Dar es salaam.

Akizungumzia majukumu ya Baraza hilo katika kutatua Migogoro inayojitokeza katika Sekta hiyo, Mhandisi Chamuriho amebainisha kuwa migogogoro iliyojitokeza imekuwa ikitegemea Ukubwa wa mradi, Hali ya eneo la mradi, Ubora wa kazi, uelewa wa vipengele mbalimbali vya mkataba katika mradi husika na moja ya pande zinazohusika kukatisha mkataba.

Kakika kukabiliana na migogoro hiyo, Baraza hilo limekuwa likitumia njia mbalimbali ikiwemo kutoa ushauri wa kitaalamu kwa pande zinazohusika katika mradi, kuwakutanisha wadau chini ya Baraza, kuweka wahusika chini ya aliyetatua mgogoro husika.

Akifafanua, Mhandisi Dkt. Chamuriho amebainisha kuwa Baraza hilo limekuwa likitumia njia hizo kutatua Migogoro katika sekta hiyo pale inaposhindikana wahusika wanaweza kwenda mahakamani kama hatua ya mwisho katika kutatua mgogoro husika.

Pia alitoa wito kwa watanzania wote hasa wadau wa Sekta ya Ujenzi kuwa na uelewa mzuri wa jinsi ya kutekeleza miradi ya ujenzi kwa kuzingatia Sheria na kanuni ili kuepuka Migogoro.

Baraza la Taifa la Ujenzi ni Taasisi ya Serikali iliyoanzishwa kwa mujibu wa sheria ya Bunge namba 20 ya mwaka 1987 iliyofanyiwa marekebisho mwaka 2008.(National Construction Council Act, CAP 162,R.E.2008) ambapo Baraza lilianza kufanya kazi tarehe 17 August 1981.

No comments: