Monday, December 21, 2015

TSHABALALA AKABIDHIWA TUNZO YA MCHEZAJI BORA WA MWEZI SIMBA SPORT CLUB

Katika kuongeza morali na kuwazawadia wachezaji wanaofanya vizuri, Klabu ya Simba ilianzisha Tunzo ya Mchezaji Bora wa Mwezi kuanzia mwezi wa Septemba 2015.
Mshindi wa mwezi wa Oktoba, 2015 ni Mohamed Hussein Tshabalala ambapo amepata kura nyingi zaidi zilizopigwa na mashabiki na wapenzi wa Simba na soka wa Tanzania kwa ujumla kupitia simu za mkononi ambao pia wamejiunga na huduma ya Simba News.
Akikabidhiwa tunzo pamoja na pesa taslim Tsh 500,000/= na Mwanachama na Shabiki wa Simba Mbunge wa Busega Simiyu Mh. Raphael Chegeni, beki wa kushoto Mohamed Tshabalala alisema “tangu nilipotata taarifa za kushinda tunzo ya mchezaji bora kwa mwezi wa 10 nilifurahi sana na leo furaha yangu inazidi zaidi, kwanza napenda kumshukuru Mungu kwa kuniwezesha kuwa mchezaji na kuweza kushinda tunzo hii, pili kuushukuru Uongozi na wapenzi wa Simba walioona mchango wangu kwenye kikosi cha Simba na kunipigia kura kwa wingi na mwisho napenda kushukuru familia yangu pamoja na watu wangu wote wa karibu ambao wamekuwa mchango mkubwa kwenye mafanikio yangu ya soka”. Ninachoweza kuwaahidi ni kuwa kamwe sitowaangusha kwani tunzo hii itakuwa chahu katika mafanikio yangu aliongeza Tshabalala.
Mwanachama na Shabiki wa Simba Mh. Chegeni alisema “kwanza kabisa nashukuru kwa Simba kunipa heshima ya kuweza kuwa mgeni rasmi katika kutoa tunzo hii kwa Tshabalala, napenda kumshauri Tshabalala na wachezaji wetu wengine kuendelea kujituma kwa bidii kwa ukiweka nidhamu, kujituma na kufanya kazi kwa bidii ni lazima mafanikio utayapata”.
Akizungumza leo jijini Dar es salaam Rais wa Simba Evans Aveva alisema “Uongozi, wanachama na wapenzi wa Simba wanathamini mno mchango wa wachezaji katika kuifanya timu yetu ifanye vizuri, hivyo tumeona ni jambo la busara kuwa klabu ya kwanza Nchini Tanzania kuwa na tunzo za mchezaji wake bora. Tunaamini kuwa Tunzo ya Mchezaji bora wa mwezi wa Simba itaongeza ari na kujituma kwa wachezaji wetu. Sisi tukiwa kama viongozi ni kazi yetu ya msingi kuhakikisha kuwa wachezaji wetu hasa wale wanaojituma zaidi wanatambuliwa na kuenziwa’’.
Akizungumza jinsi tunzo ya mchezaji bora itakavyoendeshwa, Mkurugenzi Mkuu wa EAG Group ambao ni washauri na watekelezaji wa Masoko na Biashara wa Simba, Imani Kajula alisema “Wanachama na wapenzi wa Simba na wapenda michezo ndio watakao kuwa wanachagua mchezaji bora wa mwezi kwa kutuma jina la mchezaji wanayempendekeza kwenda kwenye namba 15460, Ni wale tu ambao wamejiunga na Simba News kupitia mtandao wa Voda na Tigo wataweza kupiga kura kuchagua mchezaji bora wa mwezi wa Simba’’
Tukumbuke kuwa unaweza kumchagua mchezaji bora wa mwezi ukiwa umejiunganisha na huduma ya Simba News kwa kutuma jina la mchezaji kwenda namba 15460. Zoezi la kumchagua mchezaji bora wa mwezi wa October, 2015 linaanza tarehe October 10, 2015. Piga kura mara nyingi zaidi kuweza kumpata mchezaji wako bora wa Mwezi October, 2015.
Simba News ni huduma iliyoanzishwa na Simba ili kuwapa wapenzi wa Simba habari mbalimbali za Simba popote pale walipo ikiwemo matokeo, majina ya wachezaji wanaocheza mechi, usajili na habari nyingine za klabu ya Simba. Kujiunga na Simba News tuma neno Simba kwenda namba 15460 ni maalum kwa Tigo na Vodacom.

No comments: