Thursday, December 31, 2015

TAHADHARI YA JESHI LA POLISI KUHUSU MKESHA WA MWAKA MPYA

Tunapoelekea kumaliza mwaka 2015 na kuukaribisha  mwaka mpya wa  2016, wananchi hutumia muda huo kwenda  katika nyumba za ibada ama kusherekea katika maeneo mbalimbali ya starehe, ambapo uzoefu unaonyesha kuwa baadhi ya watu hupenda kutumia fursa hiyo kufanya vitendo  vinavyohatarisha usalama wa raia mali zao.
Jeshi la Polisi nchini, limejipanga vizuri katika mikoa yote kwa kushirikiana na vyombo vingine vya ulinzi na usalama ili kuhakikisha kwamba vitendo vyovyote vya uhalifu vitakavyojitokeza  hususani katika kipindi hiki cha kuelekea mkesha wa mwaka mpya vinadhibitiwa. Ulinzi umeimarishwa kwenye maeneo yote ya kuabudia, fukwe za bahari, sehemu za starehe na maeneo mengine yote ambayo yatakuwa na mikusanyiko mikubwa ya watu.
Aidha,  Jeshi la Polisi linatoa tahadhari kwa wananchi wote kuwa makini na kuchukua hatua stahiki za haraka kwa kutoa taarifa pindi wanapoona viashiria vyovyote vya uhalifu katika maeneo yao ya makazi ama maeneo ya biashara. Simu za polisi endapo mwananchi atakuwa na taarifa ni 111 au 112.
 Pia,  Jeshi la Polisi linawatahadharisha wale wote ambao watakuwa wakitumia barabara kuwa makini na kuzingatia sheria za usalama barabar
ani na hasa kwa madereva wa magari na pikipiki, kuepuka kujaza watu kupita kiasi, kwenda mwendo kasi, kutumia vilevi pamoja na kupiga honi hovyo.
Vilevile, wananchi kuacha tabia ya kuchoma matairi barabani pamoja na kupiga mafataki. Aidha, yeyote atakayefanya vitendo hivyo hatua kali za kisheria zitachukuliwa dhidi yake.
Nawatakieni watanzania wote kheri ya mwaka mpya.
Imetolewa na:
Advera John Bulimba-SSP
Msemaji wa Jeshi la Polisi.
Makao Makuu ya Polisi.        

No comments: