Thursday, August 31, 2017

NIMR YAFANYA UTAFITI WA VIFO VINAVYOTOKEA KATIKA HOSPITALI ZA TANZANIA

Mkuu wa Mkoa wa Morogoro Dkt Kebwe Stephen akimsikiliza Mwanasayansi Susan Rumisha aliyekuwa akitoa maelezo mbalimbali kuhusu juu ya umuhimu wa utafiti wa vifo vinavyotokea katika Hospitali za Tanzania,uliofanyika hivi karibuni uliofanywa na Taasisi ya Taifa ya Utafiti wa Magonjwa ya Binadamu (NIMR) na mrejesho unaoendelea. Dkt Kebwe aliwatembelea na kuzungumza nao washiriki wa Warsha hiyo iliyofunguliwa jana mkoani Morogoro.
 Mwanasayansi Peter Emanuel akitoa maelezo mbele ya Mkuu wa Mkoa wa Morogoro Dkt Kebwe Stephen wakiwemo na washiriki wengine wa Warsha hiyo.
Mkuu wa Mkoa wa Morogo Dkt Kebwe Stephen (pili kulia) akiwa katika picha ya pamoja na washiriki mbalimbali wa Warsha hiyo inayoendelea mkoani humo.


=====   ===== ====== ======

MUKHTASARI WA TAARIFA YA UTAFITI WA VIFO VINAVYOTOKEA KATIKA HOSPITALI YA TANZANIA 

Utangulizi 

Taarifa za vifo ni moja ya vyanzo muhimu vya takwimu katika kupanga mipango na kuandaa sera ya afya. Kuainisha vyanzo vya vifo katika hospitali zetu ni muhimu ili kufuatilia ongezeko la matukio ya vifo na kuweka vipaumbele katika kuboresha huduma za afya. Hata hivyo, kumekuwa na uhaba mkubwa wa takwimu za vifo vinavyotokea katika hospitali zetu zilizoainishwa kama inavyostahili. 

Utafiti huu ulifanywa kuainisha matokeo ya vifo katika hospitali 39 za Tanzania ili kubaini maradhi yanayoathiri jamii yetu. Utafiti huu pia ulichunguza uwepo, upatikanaji na ubora wa takwimu za vifo hospitalini. 

Mbinu za utafiti: Utafiti huu ulifanyika kati ya Julai na Desemba 2016 na ulihusisha jumla ya hospital 39. Hospitali hizo ni pamoja na hospitali ya Taifa Muhimbili, Hospitali za Rufaa za Kanda na Mikoa, Hospital Maalum na hospitali za Wilaya. Takwimu hizi zilipatikana kutoka kwenye rejesta za hospitali na za Wakala wa Vizazi na Vifo katika ofisi za Mikoa na Wilaya. Taarifa zilizokusanywa zilihusu wasifu wa jinsia ya mgonjwa na chanzo cha kifo.

Vyanzo vya vifo viliwekwa katika makundi 45 kulingana na utaratibu wa makundi ya magonjwa uliowekwa na Shirika la Afya Duniani. 

Matokeo: Kwa ujumla kulikuwa na ugumu katika upatikanaji wa takwimu. Utunzaji wa takwimu katika hospitali nyingi ulikuwa na mapungufu makubwa, na baadhi ya takwimu hazikupatikana katika baadhi ya hospitali au baadhi ya miaka iliyokusudiwa. Utunzaji wa takwimu ulikuwa mzuri kiasi katika hospitali za kanda kuliko za mikoa na wilaya. Matumizi ya majina ya magonjwa kwa kufuata mwongozo wa kimataifa yalikuwa hafifu. 

Jumla ya vifo 247,976 vilitolewa taarifa katika kipindi cha miaka 10 (2006-2015). Kulikuwa na tofauti kubwa katika idadi ya vifo kati ya jinsia ya kiume na ya kike. Vifo vingi viliathiri zaidi wanaume kuliko wanawake. Vifo vingi vilitokea katika hospitali za Mikoa ya Dar es Salaam, Morogoro na Mwanza. 

Vifo katika kundi la watoto chini ya miaka 5 vilichangia 20% ya vifo vyote. Vifo vingi viliathiri kundi la watu wenye umri wa miaka 30-45. Kwa wastani, watu wengi hufa wakiwa na umri wa miaka 31 (wanaume miaka 33 na wanawake miaka 29). 

Magonjwa yaliyoongoza kusababisha vifo ni malaria (12.8%), magonjwa ya mfumo wa hewa (10.1%), UKIMWI (8.0%), upungufu wa damu (7.8%) na magonjwa ya moyo na mfumo wa damu (6.3%). 

Vifo kwa baadhi ya magonjwa vilipungua katika kipindi cha miaka 10 iliyopita. Kati ya mwaka 2006 na 2015; vifo kutokana na malaria vilipungua kwa 47%, UKIMWI kwa 28% na Kifua Kikuu kwa 26%. Hata hivyo, kumekuwa na ongezeko kubwa la vifo vilivyosababishwa na magonjwa yanayoathiri kundi la watoto wachanga (chini mwezi mmoja) kwa 128%. 

Hospitali za mkoa wa Dar es Salaam zilikuwa na wagonjwa wengi waliokufa kutokana na malaria, UKIMWI, ajali, maambukizi ya bakteria kwenye damu, upungufu wa damu, saratani na kifua kikuu. Mkoa huu ulifuatiwa kwa karibu na Morogoro ambao ulikuwa na vifo vingi vilivyotokana na malaria na kifua kikuu. Malaria na upungufu wa damu ulichangia vifo vingi kwenye kundi la watoto chini ya miaka mitano. Vifo vingi kutokana na UKIMWI na Kifua Kikuu viliathiri watu wazima. Ajali ziliathiri kundi kubwa la vijana; wakati saratani ziliathiri makundi ya umri wote. 

Uchanganuzi wa maradhi katika makundi ya magonjwa ya kuambukiza, magonjwa yasiyoambukiza na kundi la ajali na majeraha ulionesha tofati kubwa kati ya mikoa na mikoa. Mikoa ya Pwani, Geita na Katavi iliathirika zaidi na magonjwa ya kuambukiza na utapia mlo. Vifo kutokana na ajali na majeraha viliathiri zaidi mikoa Rukwa, Tabora, Singida na Kigoma. Kundi la magonjwa yasiyoambukiza limeathiri zaidi mikoa ya Ruvuma, Manyara, Dar es Salaam na Mwanza. 

Hitimisho: Utafifi umeianisha changamoto katika ukusanyaji, uchanganuzi na matumizi ya takwimu katika hospitali zetu. Kumekuwa na matumizi hafifu ya majina ya magonjwa kwa kutumia mwongozo wa kimataifa. Vyanzo vikuu vya vifo nchini Tanzania ni malaria, maradhi yanayoathiri mfumo wa kupumua, UKIMWI, upungufu wa damu na magonjwa ya moyo na mfumo wa damu. Kumekuwa na ongezeko kubwa la vifo vya watoto wachanga, na ongezeko la vifo kutokana na magonjwa ya mfumo wa kupumua katika kipindi cha miaka 10 iliyopita. 

Mapendekezo: (i) Serikali iandae mwongozo wa ukusanyaji, matumizi, utunzaji na uhifadhi bora wa takwimu za afya; (ii) Kujenga uwezo wa watumishi wa afya katika uchanganuzi ili kuboresha matumizi ya takwimu; (iii) Kuimarisha mfumo wa takwimu wa kielektroniki; (iv) Kuimarisha mafunzo ya madaktari katika utumiaji wa mwongozo wa kimataifa wa kuanisha magonjwa na vyanzo vya vifo.

WATAALAMU WAAINISHA UMUHIMU WA KUIPITIA UPYA SERA YA MAENDELEO YA VIWANDA ENDELEVU (SIDP 1996-2020)


JA3A9647
Mkuu wa Idara ya Utafiti na Machapisho wa Taasisi ya Tafiti za Kiuchumi na Kijamii (ESRF), Profesa Fortunata Makene akitoa neno la ukaribisho kwa niaba ya Mkurugenzi Mtendaji wa ESRF, Dk. Tausi Kida wakati wa mkutano wa awamu ya pili ya kuangalia Tabia nchi, Uboreshaji kilimo, na mahusiano yake na biashara kwa jumuiya ya Afrika Mashariki (PACT EAC2), uliofanyika mwishoni mwa wiki katika ukumbi wa mikutano wa ESRF jijini Dar es Salaam.

Katika mkutano huo ilikubalika haja ya kuwa na mikakati ya utetezi kwa kuangalia tafiti zitakazofanywa juu ya kinachojiri katika maendeleo kwa kuzingatia mabadiliko ya tabia nchi, usalama wa chakula na biashara. Zaidi ya yote, pia wadau waliona kuna haja kubwa ya kuwa na tafiti itayoweza kuonesha ni kwa kiasi gani sera ya SIDP (1996-2020) imeweza kuchangia katika ukuaji wa viwanda Tanzania, na changamato zipi imekumbana nazo ambazo zinapaswa kutatuliwa na kuanishwa wakati wa mapitio ya sera hii.
Akiwasilisha hoja yake ndugu Solomon Baregu, Mtafiti wa ESRF na Meneja wa Mradi wa PACT EAC 2, amesema kwa kuangalia hali halisi ya sasa ipo haja kwa wataalamu kutambua changamoto zinazojitokeza katika maendeleo endelevu ya viwanda na kukiangalia kilimo kama msingi wa uimarishaji wa viwanda.
Aidha alisema kwamba kwa kuangalia hali ya sasa ipo haja kubwa ya kubadili kilimo cha Tanzania ili kuboresha maisha ya wananchi na kuimarisha viwanda kwa kuvipatia mali ghafi ya kutosha na yenye ubora.
Alisema ni vyema kuelewa uhusiano uliopo katika sera za maendeleo ya viwanda na kilimo ili kuwa na mpango mahsusi wa utetezi kwa lengo la kuimarisha viwanda.
Katika mkutano huo washiriki pia walipitia mambo mbalimbali na hatua zinazochukuliwa kupitia sera ya mpango wa maendeleo wa viwanda unaomalizika 2020.
JA3A9658
Mkurugenzi Msaidizi wa idara ya Ushirikishaji Kikanda kutioka Wizara ya Viwanda, Biashara na Uwekezaji, Bi. Sekela Mwaisela akisoma hotuba ya ufunguzi kwa niaba ya Katibu Mkuu wa wizara hiyo wakati wa mkutano wa awamu ya pili ya kuangalia Tabia nchi, Uboreshaji kilimo, na mahusiano yake na biashara kwa jumuiya ya Afrika Mashariki (PACT EAC2), uliofanyika mwishoni mwa wiki katika ukumbi wa mikutano ESRF jijini Dar es Salaam.
Miongoni mwa mambo yaliyojitokeza kwenye mazungumzo ya tafiti  ni umuhimu wa kuoanisha sera mbalimbali katika kilimo na viwanda kuzihuisha na kuzipa mwelekeo wenye maana kama chachu katika kuimarisha uchumi wa viwanda.
Walisema ipo haja ya kuangalia sera hizo ili ziwe msaada katika kuimarisha kilimo na kutoa ushindani kwa viwanda vinavyotegemea bidhaa za kilimo ili kujiimarisha.
Aidha katika mazungumzo kwenye mkutano huo imeelezwa kuwa ingawa serikali kupitia wizara zake mbalimbali na Ofisi ya Makamu wa Rais wamechukua hatua kadhaa kuwa na matokeo bora katika utetezi wa bidhaa za viwanda zinazotokana na kilimo, kukosekana kwa uangalizi na utekelezaji wa pamoja kumeleta shida kwa wananchi.
Sera ya sasa ya maendeleo endelevu ya viwanda (SIDP) imetengenezwa mwaka 1996 na itaisha 2020 lakini bado ipo haja ya kuweka mahusiano katika utekelezaji wa mpango huo wa maendeleo, kwani kwa mazingira ya sasa hakuna mahusiano na kuna vikumbo katika sera mbalimbali.
Wamesema kwamba sera hiyo haitoi mwanya wala mahusiano kati ya viwanda vya kuchakata mazao ya kilimo, mabadiliko ya tabia nchi, biashara na usalama wa chakula.
JA3A9677
Mtafiti wa ESRF na Meneja wa Mradi wa PACT EAC 2, Solomon Baregu akiwasilisha namna bora ya kufanya utafiti wenye lengo la kuoanisha mpango wa maendeleo endelevu ya viwanda na mabadiliko ya tabia nchi na kilimo wakati wa mkutano huo wa kuzungumzia mradi wa PACT-EAC2 uliofanyika mwishoni mwa wiki katika ukumbi wa mikutano wa ESRF jijini Dar es Salaam.
Aidha walisema kwamba mpango wa pili wa maendeleo (2016/17-2020/21) unaonesha haja ya kuweka Tanzania katika njia ya viwanda kwa kuijengea nchi uwezo wa kuzalisha katika kilimo na pia katika ufugaji.
Haja ya kubadilisha Kilimo inatokana na  ukweli kuwa ni moja ya sekta zinazoingiza kipato cha kigeni kwani inachangia asilimia 29.1 ya pato la taifa, huku ikichangia asilimia 30 ya fedha za kigeni.
Aidha ndio chanzo pekee cha uhakika cha biashara ikitoa asilimia 65 ya mahitaji ya viwanda (ghafi) na asilimia 90 ya chakula cha taifa huku ikiajiri asilimia 66.9 ya nguvu kazi ya Taifa.
Ndugu Peter Lanya, aliekua Makamu Mwenyekiti wa TCCIA, akitoa ufafanuzi zaidi alisema kwamba kunatakiwa mabadiliko katika sera hiyo ili kuupa usasa kwa kuwekeza kwenye mahusiano ya kilimo, mali ghafi kama taifa likitaka kuendelea kuelekea uchumi wa viwanda.
Naye ndugu, Joseph Kihaule, Afisa Mkuu wa Mazingira kutoka Ofisi ya Makamu wa Raisi, alisema kwamba kuna haja ya kubadilika katika kilimo ili kuweza kufanya vyema huku akisema mazungumzo ya kimataifa ya kupata muafaka, hususani yahusuyo mabadiliko ya tabia nchi, ni muhimu yakaunganishwa na sera mbalimbali ili kuimarisha kilimo na upatikanaji wa chakula.
JA3A9779
Aliyekuwa Makamu Mwenyekiti wa TCCIA, Peter Lanya akizungumzia SIDP 1996-2020 wakati wa mkutano wa awamu ya pili ya kuangalia Tabia nchi, Uboreshaji kilimo, na mahusiano yake na biashara kwa jumuiya ya Afrika Mashariki (PACT EAC2), uliofanyika mwishoni mwa wiki katika ukumbi wa mikutano wa ESRF jijini Dar es Salaam. Kulia ni Mkurugenzi Msaidizi wa idara ya Ushirikishaji Kikanda kutoka Wizara ya Viwanda, Biashara na Uwekezaji, Bi. Sekela Mwaisela.
Awali akifungua semina hiyo Katibu Mkuu  Wizara ya Viwanda, Biashara na uwekezaji (viwanda) Adelhelm Meru  alishukuru  taasisi za ERSF na CUTS International kwa kuona umuhimu wa kuwa na mkutano huo wanne wa kitaifa kuzungumzia mradi wa PACT-EAC.
Katika hotuba yake iliyosomwa na Mkurugenzi msaidizi Wizara ya Viwanda Ushirikishaji Kikanda, Bi. Sekela Mwaisela alisema kwamba wizara inatambua haja ya kuweka pamoja viwanda na uchakataji wa mazao ya kilimo kwa kuwa inasaidia kuweka sawa maendeleo ya viwanda.
Alisema kwamba kazi iliyofanywa na ESRF inaiweka wizara hiyo katika nafasi bora zaidi ya kufanya mabadiliko ya muhimu kufikia mwaka 2020.
Alisema sera hiyo iliyoanza 1996-2020 imepita katika maeneo matatu ambayo yalilenga kuimarisha  uwezo wa viwanda (1996-2000), matumizi ya teknolojia (2000-2010) na uimarishaji wa viwanda 2010-2020.
Alisema SIDP imesaidia kuimarisha viwanda na sasa lazima kuwepo na uangalizi ili kuwepo na mahusiano mazuri kati ya sera zote zinazotegemewa kuwezesha maendeleo endelevu ya viwanda.
JA3A9745
Afisa Mkuu wa Mazingira kutoka Ofisi ya Makamu wa Rais-Mazingira, Joseph Kihaule akichangia maoni katika mkutano huo uliofanyika mwishoni mwa wiki katika ukumbi wa mikutano wa ESRF jijini Dar es Salaam.
Naye Mkurugenzi Mtendaji wa ESRF, Dk. Tausi Kida katika hotuba yake iliyosomwa na Prof. Fortunata Makene amesema ipo haja kubwa ya kuwepo kwa mabadiliko katika SIDP kutokana na mahusiano yake na sekta nyingine hasa yenye uhusiano na kilimo.
Katika mkutano huo wa awamu ya pili ya kuangalia Tabia nchi, Uboreshaji kilimo, na mahusiano yake na biashara kwa jumuiya ya Afrika Mashariki (PACT EAC2), Dk Kida alisema kwamba taasisi yake imefurahi kutoa mchango kwa ajili ya kusaidia kuimarisha viwanda nchini.
Alisema mkutano huo unaoangalia namna ya kuboresha sera ya viwanda, SIDP (1996-2020), kabla ya utafiti utakaoanza baadae ni muhimu katika kuona kwamba kilimo kinaboreshwa sanjari na SIDP kwa kuweka mahusiano ambayo awali yalikosekana katika sera ya SIDP.
JA3A9740
Pichani juu na chini sehemu ya washiriki wakichangia maoni wakati wa mkutano huo uliofanyika mwishoni mwa wiki katika ukumbi wa mikutano ESRF jijini Dar es Salaam.
Alisema kwa taifa la Tanzania ili lisonge mbele ni vyema masuala muhimu katika SIDP yakaangaliwa ili kutekeleza mipango ya maendeleo ya viwanda kwa kuhusisha na uchakataji wa mazao ya kilimo.
Aidha alisema katika utafiti utakaosaidia kuboresha SIDP majukumu ya biashara ya kimataifa katika maendeleo ya viwanda na tabia nchi haviwezi kudharaulika.
Alisema utafiti utakaofanywa utasaidia kuongeza ‘nyama’ zaidi katika mikakati ya maendeleo kwa kufanya utetezi kwenye mabadiliko ya tabia nchi, biashara na usalama wa chakula kwa kufanya mabadiliko makubwa katika  uchakataji bidhaa za kilimo kwa kutambua pia makubaliano ya kimataifa ambayo Tanzania ni mshiriki, hususani UNFCCC na WTO.
JA3A9736
JA3A9704
Picha juu na chini washiriki kutoka taasisi mbalimbali za serikali na sekta binafsi walioshiriki kwenye mkutano huo.
JA3A9749
JA3A9695
Picha ya pamoja ya washiriki.

WATAALAMU na wanazuoni wamekubaliana haja ya kupitia mpango wa maendeleo endelevu wa viwanda, SIDP (1996-2020), ili kwenda na wakati kwa kubadili kilimo na kuiweka nchi katika njia bora ya kufikia uchumi wa viwanda.
Kauli hiyo imetamkwa kwa namna tofauti na wataalamu hao ambao wamekutana jijini hapa kuangalia uhusiano uliopo kati ya viwanda, mabadiliko ya tabia nchi na kilimo; na ni namna gani sera ya viwanda inaweza kupitiwa upya kuakisi mahusiano haya.
Warsha hiyo iliyoandaliwa na ESRF na CUTS International imelenga katika kuelezea umuhimu wa kuangalia  mahusiano ya sera ya maendeleo ya viwanda na mabadiliko ya tabia nchi, usalama wa chakula na biashara.
Wakijadili mada mbalimbali zilizowasilishwa katika semina hiyo iliyofanyika ESRF, wataalam hao walitambua umuhimu  wa pekee wa kupitia upya sera hiyo ili iweze kuonesha muunganiko fasaha uliopo kati ya viwanda, kilimo na biashara; na hatua/mikakati ipi iwepo kukinga adhma hii ya viwanda dhidi ya athari za mabadiliko ya tabia nchi.
Wamesema kwamba kwa kuunganisha sera ya maendeleo endelevu ya viwanda na uchakataji wa bidhaa za kilimo na kilimo chenyewe kunaleta mwanya wa kuweka msingi imara katika mchakato wa maendeleo na hasa viwanda. Pia, kwa kuwa na sera madhubuti, nchi itaweza kuvutia wawekezaji wa ndani na nje ya nchi kuwekeza katika sekta ya Viwanda, hususani viwanda vinavyotegemea maligafi za sekta ya kilimo.

Kamati za kudumu za bunge za Pac na Laac zaendelea na vikao vyake leo Mjini Dodoma

1
 Mjumbe wa kamati ya kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali (PAC) Mhe. Mussa Mbaruku akizungumza jambo pale kamati hiyo ilipokutana na viongozi kutoka Ofisi ya Mkaguzi na Mdhibiti Mkuu wa Hesabu za Serikali, kwa lengo la kuwapitisha Wajumbe wa kamati kuhusu hesabu za fedha za Taasisi husika, katika kikao kilichofanyika jana Mjini Dodoma. kulia ni Mjumbe wa kamati hiyo Mhe. Juma Aweso
2
 Mjumbe wa kamati ya kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali (PAC) Mhe. Japhet Hasunga akiongoza kikao cha kamati hiyo pale  ilipokutana na viongozi kutoka Ofisi ya Mkaguzi na Mdhibiti Mkuu wa Hesabu za Serikali, kwa lengo la kuwapitisha Wajumbe wa kamati kuhusu hesabu za fedha za Taasisi husika, katika kikao kilichofanyika leo Mjini Dodoma.
3
 Wajumbe wa kamati ya kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali (PAC) wakifuatilia mazungumzo baina yao na Viongozi kutoka Wizara ya Mifugo na Uvuvi lengo likiwa ni kupitia Mahesabu na Maagizo ya kamati hiyo, katika kikao kilichofanyika jana Mjini Dodoma kikiongozwa na Mwenyekiti wa kamati hiyo Mhe. Naghenjwa kaboyoka(katikati).
4
Mwenyekiti wa Kamati ya kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali za Mitaa (LAAC) Mhe. Vedasto Ngombale (katikati) akiongoza kikao cha kamati hiyo dhidi ya viongozi kutoka Ofisi ya Mkaguzi na Mdhibiti Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG), Hazina na Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI) katika kikao kilichofanyika jana Mjini Dodoma.kushoto ni Makamu Mwenyekiti wa kamati hiyo, Mhe. Abdallah Chikota na kulia ni katibu kamati wa Bunge, Ndg. Dismiss Muyanja


(PICHA NA OFISI YA BUNGE)

Serikali ya Marekani yarejea upya ahadi yake ya kufanya kazi na jeshi la wananchi wa Tanzania katika mapambano dhidi VVU/Ukimwi

1
2
3MR
Dar es Salaam, TANZANIA.  Serikali ya Marekani kupitia Taasisi ya kijeshi ya Walter Reed (WRAIR) imesaini upya makubaliano ya ushirikiano na Jeshi la Wananchi wa Tanzania (JWTZ) siku ya Jumanne, Agosti 29, 2017 katika sherehe ya kusaini tamko la pamoja la ushirikiano katika jitihada za kupambana na VVU/UKIMWI. WRAIR ni kitengo cha kikosi cha jeshi la Marekani kinachojihusisha na tafiti za kitabibu na kimefanya kazi moja kwa moja na JWTZ tangu mwaka 2004 kutekeleza programu za VVU/UKIMWI Tanzania.

Utiaji saini huo uliofanywa na Kaimu Balozi wa Marekani nchini Tanzania Dr. Inmi Patterson na Mkuu wa Huduma za Kitabibu wa JWTZ, Meja  Generali (Dk.) Denis Raphael Janga, unawakilisha dhamira ya pamoja katika upatikanaji endelevu wa huduma za afya na mpango mkakati wa kukabiliana na tishio la VVU/UKIMWI.

Makubalino ya awali, yaliyosainiwa mwaka Aprili 2011 yanabainisha ushirikiano wa pande hizo mbili katika kupunguza maambukizi mapya na kuboresha matibabu na huduma za kuzuia maambukizi.

Kupitia ushirikiano huu endelevu wa pande hizi mbili Mfuko wa Dharura wa Rais wa Marekani wa Kupambana na UKIMWI (PEPFAR) unatoa nafasi kwa majeshi ikiwemo JWTZ kuelewa vizuri tishio la afya, tabia na mazingira hatarishi yanayohusiana na kuenea kwa maambukizi ya VVU.

“Mafanikio ya ushirikiano wa WRAIR/JWTZ hayapingiki na faida zake ziko wazi.”alisema Kaimu Balozi Patterson. “Kwa pamoja tumehakikisha upatikanaji endelevu wa huduma za tiba kupitia ujenzi wa vituo vipya, ukarabati wa vituo vya zamani, vya matunzo na tiba na kutoa vifaa vya maabara.”

Ushirikiano huu wa pande mbili kati ya WRAIR na JWTZ umeundwa kuimarisha na kusaidia utafiti na utekelezaji wa jitihada za matunzo na matibabu ya VVU nchini Tanzania.

RAIS DKT MAGUFULI ASITISHA UBOMOAJI WA NYUMBA 300 TUANGOMA JIJINI DAR

Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Paul Makonda akizungumza na wananchi wa Tuangoma wilaya ya Temeke jijini Dar es Salaam  na kusitisha bomoa bomoa iliyokuwa ikiendelea katika eneo hilo. Pia  amewaomba kujiepusha na kujenga nyumba za kuishi katika maeneo hatarishi.



Baadhi ya wananchi wa Tuangoma Wilayani Temeke wakimsikiliza Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam leo (hayupo pichani),Mhe. Paul Makonda  mara baada ya kutembelea eneo lao na kuzungumza nao.
Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Paul Makonda akiwa amezungukwa na wananchi mbalimbali wa eneo la Tuangoma,akitembelea maeneo ambayo nyumba zake zilikuwa zikitarajiwa kukumbwa na zoezi  la bomoa bomoa.
Baadhi ya Nyumba ambazo zilitakiwa kubomolewa,ambapo kwa sasa hazitabolewa kufuatia agizo la Rais Dkt John Pombe Magufuli kusitisha zoezi hilo na kuwataka wahusika wafuate taratibu na sheria za Ardhi .


Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe, Dkt. John Pombe Magufuli pamoja na Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam Mhe Paul Makonda Wamesitisha zoezi la BOMOA BOMOA kwa Nyumba zaidi ya elfu kumi na saba (17, 000) zilizotangazwa KUBOMOLEWA na Baraza la Hifadhi ya Mazingira NEMC.

Hatua ya kusitisha zoezi hilo, Imekuja kufuatia Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam Mhe Paul Makonda kuzungumza na Mhe Rais, Dkt. John Pombe Magufuli kuhusiana na Sintofahamu ya bomoa bomoa hiyo ambayo amemueleza Mhe Rais Magufuli kuwa Taarifa za BOMOA BOMOA ya Nyumba elfu kumi na saba iliyotolewa HAIKUFIKA ofisini Kwake, Jambo ambalo ni tofauti na Taratibu za Utendaji kazi wa Serikali.
Mhe Makonda amesema, hata kama TAMKO hilo limetolewa na watumishi wa Mkoa mfano Wakurugenzi wa Manisapaa au Wakuu wa Wilaya walioko Chini ya Mamlaka ya Mkuu wa Mkoa LAZIMA Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam ipate taarifa na iridhie bomoa bomoa hiyo, na pia hata kama Taarifa zimetoka Wizarani inapaswa taratibu za kimaandishi zifuatwe kwa kujulisha Ofisi ya Mkoa.
"Haiwezekani mtu kutoa TAMKO la kuvunja Nyumba elfu kumi na saba bila Mkoa kujua, hilo HALIWEZEKANI," amesema Mhe Makonda.
Mhe Makonda amefafanua kuwa AMEONGEA na Mhe Rais Magufuli na Kumuuliza kama ana taarifa za zoezi la Ubomoaji wa Nyumba elfu kumi na saba ambapo Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam Mhe Paul Makonda ALIMUELEZA Mhe Rais Magufuli kuwa HANA taarifa hizo za UBOMOAJI, zaidi Ubomoaji wa Nyumba zilizo kwenye Hifadhi ya Barabara ya kuanzia Ubungo kwenda KIMARA na MBEZI Ubomoaji unaofanywa kwa ajili ya upanuzi wa Barabara ya Morogoro, Ubomoaji wa Nyumba zilizo Jirani na Reli hususani ni zile zinazohusiana na Ujenzi wa Reli Mpya na ya Kisasa.
Kutokana na Sababu hizo, Mhe Makonda amesema Mhe Rais amesikitishwa na TAMKO hilo la kutaka KUBOMOLEWA kwa Nyumba zaidi ya elfu kumi na saba na ametoa pole kwa Wananchi waliokumbwa na TAHARUKI ya TAMKO hilo la Ubomoaji, na kusisitiza kuwa Mhe Rais, Dkt. John Pombe Magufuli HAKUCHAGULIWA kwa ajili ya KUBOMOA Nyumba za watu na kusisitiza kuwa anataka wananchi WANAOISHI katika maeneo HALALI kuachwa mana AMEPATA taarifa kuwa huenda ZOEZI hilo lingekwenda mbali zaidi mpaka kwa Wananchi WASIOHUSIKA.
Katika HATUA nyingine, Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam Mhe Paul Makonda AMEPIGA MARUFUKU zoezi lolote UBOMOAJI wa Nyumba pasipo Ofisi yake kupewa TAARIFA na kisha KURIDHIA Ubomoaji huo.
Mwisho, Mhe Paul Makonda AMEWATAKA wananchi na wakazi wote wa Mkoa wa Dar es Salaam kuzingatia SHERIA na wasivamie maeneo au kuuziwa VIWANJA na Matapeli na pia AMEWATAKA wananchi kuchukua TAHADHARI hususani ni katika maeneo yote HATARISHI ambayo sio SALAMA kwa MAKAZI na kuwataka kila Mwananchi Mwenye Familia KUTAFUTA Salama kwa Maisha yake na ya Familia yake.
Mhe Makonda Pia ametoa OMBI Maalumu Kwa Waziri Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi Mhe William Lukuvi la KUBORESHA mfumo wa Ardhi katika Mkoa wa Dar es Salaam kwa kuanzisha mpango wa kuweka MAAFISA ARDHI katika KATA zote za Mkoa wa Dar es Salaam ambao watakuwa na JUKUMU la KUSIMAMIA, KURATIBU masuala yote ya Ardhi ngazi ya KATA hatua ambayo itasaidia kuondoa Migogoro na UTAPELI kwa Wananchi kuuziwa au kununua Ardhi katika maeneo ambayo HAYARUHUSIWI, ambapo amesema amepata wazo hilo kutokana na uzoefu aliopata akiwa Rais wa umoja wa Vyuo vikuu -TAHILISO ambapo alishirikiana na Bodi ya Mikopo kuanzisha mfumo wa kuwa na MAAFISAMikopo katika vyuo hatua iliyosababisha kuondoa kero ya wanafunzi kufuatilia Mikopo katika Ofisi za bodi ya Mikopo hatua ambayo imekuwa mwarobaini wa tatizo la kufuatilia Mikopo kwa wanafunzi, Mhe Makonda amesema atamwandikia OMBI hilo na kulifikisha Rasmi kwa Mhe Lukuvi ili amsaidie kulifikisha kwa Mhe Rais, Dkt. John Pombe Magufuli kwa ajili utekekezaji.
Imetolewa na Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam.
30/08/2017 

WAKUFUNZI WA WADADISI WA UTAFITI WA KILIMO NA MIFUGO WAPIGWA MSASA

 Mkurugenzi wa Shughuli za Kitakwimu wa Ofisi ya Taifa ya Takwimu Irenius Ruyobya akizungumza leo na Wakufunzi wa Wadadisi wa Utafiti wa Kilimo na Mifugo wa mwaka 2017 wakati wa mafunzo ya wakufunzi hao yanayoendelea kufanyika mkoani Morogoro. Utafiti wa Kilimo na Mifugo wa mwaka 2017 unatarajia kufanyika nchi nzima kuanzia mwezi Oktoba, 2017.

 Mtalaamu wa Kilimo na Mifugo kutoka Wizara ya Kilimo, Maliasili, Mifugo na Uvuvi, Zanzibar Mzee M. Mzee akiwafundisha Wakufunzi wa Wadadisi wa Utafiti wa Kilimo na Mifugo wa mwaka 2017. Mafunzo ya wakufunzi hao yanafanyika mkoani Morogoro ambapo utafiti huo unatarajia kufanyika nchi nzima kuanzia mwezi Oktoba, 2017.

 Mmoja wa Wakufunzi akiuliza swali wakati wa mafunzo ya Wakufunzi wa Wadadisi wa Utafiti wa Kilimo na Mifugo wa mwaka 2017 yanayofanyika mkoani Morogoro.  Utafiti huo wa Kilimo na Mifugo wa mwaka 2017 unatarajia kufanyika nchi nzima kuanzia mwezi Oktoba, 2017.

 Baadhi ya Wakufunzi wakijifunza mbinu mbalimbali zitazotumika kuwafundishia Wadadisi wa Utafiti wa Kilimo na Mifugo wa mwaka 2017. Mafunzo ya wakufunzi hao yanafanyika mkoani Morogoro ambapo utafiti huo unatarajia kufanyika nchi nzima kuanzia mwezi Oktoba, 2017.
Mkurugenzi wa Shughuli za Kitakwimu wa Ofisi ya Taifa ya Takwimu (NBS) Irenius Ruyobya akitoa maelekezo kwa waratibu wa mafunzo ya Wakufunzi wa Wadadisi wa Utafiti wa Kilimo na Mifugo wa mwaka 2017. Mafunzo ya Wakufunzi hao yanafanyika mkoani Morogoro na utafiti huo unatarajia kufanyika nchi nzima kuanzia mwezi Oktoba, 2017. (PICHA ZOTE NA VERONICA KAZIMOTO).

Na: Veronica Kazimoto-Mororgoro.

Jumla ya wakufunzi 52 wakiwemo Mameneja Takwimu wa mikoa yote nchini wamepewa mafunzo juu ya mbinu mbalimbali zinazotumika kufundishia wadadisi kwa ajili ya kupata takwimu bora za kilimo na mifugo.

Mafunzo hayo ya wiki moja yanayoendelea kufanyika mkoani morogoro, yanalenga kuwajengea uwezo wakufunzi hao ili waweze kuwafundisha wadadisi wa Utafiti wa Kilimo na Mifugo wa Mwaka 2017 kwa ajili ya kupata takwimu rasmi zitakazotumika katika kupanga mipango ya maendeleo.

Akizungumza wakati wa mafunzo hayo, Mkurugenzi wa Shughuli za Kitakwimu wa Ofisi ya Taifa ya Takwimu (NBS) Irenius Ruyobya amewataka wakufunzi wao kuzingatia kwa makini mafunzo hayo ili waweze kuwafundisha kwa ufanisi wadadisi wakaokusanya taarifa za utafiti huo wa kilimo na mifugo.

"Ili kuiwezesha nchi yetu kupata takwimu bora za kilimo na mifugo inatakiwa ninyi wakufunzi kuzingatia kwa makini mafunzo haya ili muweze kuwafundisha kwa ufanisi mkubwa wadadisi ambao watazunguka nchi nzima kukusanya takwimu za kilimo na mifugo", amesema Ruyobya.

Utafiti wa Kilimo na Mifugo hufanyika kila mwaka ambapo utafiti wa mwaka huu utafanyika kuanzia mwezi Oktoba, 2017 chini ya Ofisi ya Taifa ya Takwimu kwa kushirikiana na Wizara ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi na Wizara ya Viwanda na Biashara.