Tuesday, June 02, 2026

RAIS SAMIA AANZA ZIARA YA KIHISTORIA URUSI, KUITANGAZA TANZANIA YA DIRA YA MAENDELEO 2050


Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akiagana na viongozi mbalimbali kwenye Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere (JNIA) Jijini Dar es Salaam kabla ya kuondoka nchini, kuelekea Shirikisho la Urusi kwa ziara ya Kitaifa itakayoanza tarehe 3 hadi 5 Juni, 2026 kwa mualiko wa Rais wa Shirikisho la Urusi, Mheshimiwa Vladimir Putin



Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, leo Juni 2, 2026 ameondoka nchini kuelekea Shirikisho la Urusi kwa ziara ya kitaifa ya kihistoria inayofanyika kufuatia mwaliko rasmi wa Rais wa Shirikisho la Urusi, Mhe. Vladimir Putin.

Mhe. Dkt. Samia aliondoka katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere (JNIA), Dar es Salaam, ambako alisindikizwa na viongozi mbalimbali wa Serikali kabla ya kuanza safari hiyo inayotarajiwa kufungua ukurasa mpya wa ushirikiano kati ya Tanzania na Urusi katika sekta za uchumi, biashara, uwekezaji, elimu, teknolojia, nishati na maendeleo ya miundombinu.

Ziara hiyo inakuja katika kipindi ambacho Tanzania inaendelea kutekeleza kwa kasi ajenda yake ya mageuzi ya kiuchumi na maendeleo jumuishi chini ya uongozi wa Rais Samia, huku nchi ikijipanga kufikia malengo ya Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050.

Katika ziara hiyo, Tanzania itapata fursa ya kuwasilisha mafanikio makubwa yaliyopatikana katika miaka ya hivi karibuni pamoja na mwelekeo wa maendeleo ya baadaye, hususan katika utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050 inayolenga kuifanya Tanzania kuwa nchi yenye uchumi imara, shindani na unaotoa fursa kwa wananchi wote.

Aidha, mazungumzo kati ya viongozi wa Tanzania na Urusi yanatarajiwa kuimarisha zaidi uhusiano wa kidiplomasia uliodumu kwa miongo kadhaa na kufungua milango mipya ya uwekezaji, biashara na ushirikiano wa kimkakati unaolenga kukuza ustawi wa wananchi wa mataifa hayo mawili.

Ziara ya Rais Samia nchini Urusi pia inaonesha kuendelea kuimarika kwa nafasi ya Tanzania katika diplomasia ya kimataifa, ambapo taifa linaendelea kujenga mahusiano yenye manufaa ya pamoja na mataifa mbalimbali duniani sambamba na kutangaza fursa zake za kiuchumi na maendeleo.

Kupitia ziara hiyo, Tanzania inatarajia kuendelea kujifunza uzoefu wa kimataifa, kuvutia mitaji na teknolojia mpya, pamoja na kuimarisha ushirikiano utakaochangia utekelezaji wa vipaumbele vya maendeleo ya taifa kwa manufaa ya vizazi vya sasa na vijavyo.

RAIS SAMIA AANZA ZIARA YA KIHISTORIA URUSI, KUITANGAZA TANZANIA YA DIRA YA MAENDELEO 2050

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akiagana na viongozi mbalimbali kwenye Uwanja wa Ndege wa Kimataifa w...