Wednesday, December 16, 2015

UNCDF YATOA BILIONI 2.4/- KUSAIDIA MIRADI 6 YA MIUNDOMBINU

 
Mkurugenzi wa Mfuko wa Mtaji wa Maendeleo wa Umoja wa Mataifa, (UNCDF) nchini Tanzania, Peter Malika akizungumza na wageni waalikwa wakati wa makabidhiano ya misaada kwa miradi ya maendeleo iliyodhaminiwa na UNCDF Tanzania.
 
Naibu Katibu Mkuu Tamisemi, Kagyabukama E.Kiliba akisoma hotuba yake wakati wa kukabidhi hundi kwa mashirika binafsi na ya umma kwa ajili ya kuendeleza miradi ya maendeleo.
Naibu Katibu Mkuu Tamisemi, Kagyabukama E.Kiliba (katikati) akimkabidhi hundi bilioni moja na milioni sabini (1,070,000,000) Mkurugenzi wa Mji wa Kibaha, Bi. Jennifa C. Omolo (kulia) na kushoto ni Mkurugenzi wa Mfuko wa Mtaji wa Maendeleo wa Umoja wa Mataifa, (UNCDF) nchini Tanzania, Peter Malika.DSC_0211
Mkurugenzi wa Manispaa ya Moshi, Bw. Jeshi Godfrey Lupembe (kushoto) akikabidhiwa hundi ya shilingi milioni mia tano na tisa (509,000,000/=) na Naibu Katibu Mkuu Tamisemi, Kagyabukama E.Kiliba (kulia) pamoja na Mkurugenzi wa Mfuko wa Mtaji wa Maendeleo wa Umoja wa Mataifa, (UNCDF) nchini Tanzania, Peter Malika.
Naibu Katibu Mkuu Tamisemi, Kagyabukama E.Kiliba pamoja na Mkurugenzi wa Mfuko wa Mtaji wa Maendeleo wa Umoja wa Mataifa, (UNCDF) nchini Tanzania, Peter Malika wakiwakabidhi masisita hundi ya milioni miamoja na saba (107,000,000/=) wa kwanza kulia ni Msimamizi wa Mradi wa Umeme wa Lupali, Sister Imakulata Mlowe na Sister Helga Silinu ambaye ni fundi umeme katika mradi wa Lupali.
Mkuu wa wilaya ya Ileje , Mh. Rosemary Senyamule (kulia) akipokea hundi ya milioni mia mbili na milioni ishirini na sita (226,000,000/=) kutoka kwa UNCDF iliyotolewa na mgeni rasmi Naibu Katibu Mkuu Tamisemi, Kagyabukama E.Kiliba pamoja na Mkurugenzi wa Mfuko wa Mtaji wa Maendeleo wa Umoja wa Mataifa, (UNCDF) nchini Tanzania, Peter Malika.
Baadhi ya wageni waalikwa wakiendelea kufuatilia kwa makini kinachozungumzwa na baadhi ya viongozi.
Mkurugenzi wa Mji wa Kibaha, Bi. Jenifa C. Omolo akitoa neno la shukrani kwa niaba ya sekta za umma na sekta binafsi zilizopata msaada huo ili kuendeleza miradi ya maendeleo hapa nchini.
Picha ya pamoja.
…………………………………………………………………………………………
Na Mwandishi wetu 
  MFUKO wa Maendeleo ya Mtaji wa Umoja wa Mataifa (UNCDF) umetoa msaada wa shilingi bilioni 2.4 kama kianzio cha mtaji kwa waandaaji wa miradi kutoka sekta binafsi na umma. Katika hafla iliyofanyika leo na kufunguliwa na Naibu Katibu Mkuu TAMISEMI, Kagyabukama Kiliba hawala sita zilikabidhiwa wawakilishi wa waendeshaji katika miradi iliyotawanyika sehemu mbalimbali nchini. 
  Pamoja na hawala hizo za bilioni 2.4 imo pia shilingi bilioni 1.6 kwa ajili ya miradi yenye mwelekeo wa kibiashara inayoandaliwa na mamlaka za serikali za mitaa nchini Tanzania. Miradi iliyopewa kianzio cha mtaji ni pamoja na halmashauri ya mji wa Kibaha kwa ajili ya ujenzi wa kituo cha basi na soko la kisasa, halmashauri ya manispaa ya Moshi kwa ajili ya kituo cha kisasa cha mabasi cha biashara na manispaa ya Ileje kwa ajili ya ujenzi wa mnara wa redio kwa kushirikiana na sekta binafsi. 
  Mradi mwingine ni wa uzalishaji wa umemejua (mtandao wa vijijini) unaotekelezwa wilaya ya Korogwe na kampuni binafsi ya Ensol, mradi binafsi wa uzalishaji umeme kwa maji unaoendeshwa na wanawake wa wilaya ya njombe vijijini na mradi mdogo binafsi wa uzalishaji umeme wa Maguta uliopo wilayani Kilolo. Akizungumza kumkaribisha mgeni rasmi kutoa hundi hizo, Mkuu wa UNCDF nchini Tanzania Peter Malika alisema msaada uliotolewa umelenga kuonesha mafanikio ya program ya mradi wa fedha za nahalia (LFI) wa UNCDF katika kusaidia waandaaji wanaojishughulisha na miradi inayotoa mchango katika maendeleo ya uchumi ya maeneo husika. 
  “Licha ya kuongezeka kwa upatikanaji wa mtaji wa uwekezaji kutoka vyanzo vya umma na binafsi kwa ajili ya miundombinu, ni kiasi kidogo sana kinachofikia miundombinu ambayo inaunda uti wa mgongo wa michakato ya uchumi. LFI ilibuniwa ili kushughulikia changamoto hizi na uliundwa ili kuonyesha kwamba miradi ya miundombinu ambayo inapewa kipaumbele na serikali za mitaa na jamii inaweza kuvutia fedha endapo matatizo ya soko la mtaji yaliyopo yatashughulikiwa” alisema Malika. 
  Aidha Malika alisema katika mwaka huu timu ya LFI ilitoa msaada wa kiufundi wa kulenga na kianzio cha mtaji kwa zaidi ya miradi 30,tisa kati ya hiyo ikiwa katika hatua za juu na kwa hiyo kuwa tayari kupokea uwekezaji ikiwemo miradi tisa iliyotunukiwa msaada jana. Tangu kuanzishwa kwake mwaka 2012 LFI-T imesaidia zaidi ya miradi ya maendeleo ya mahalia 30 nchini Tanzania katika hatua mbalimbali tangu uwekaji mipango hadi kuwa tayari kupokea uwekezaji kwa kufanyakazi kwa karibu na Tamisemi na taasisi za fedha. 
  Aidha LFI-T inasaidia miradi katika mikoa 18 iliyo katika sekta mbalimbali ikiwamo ya usindikaji mazao ya kilimo, tabia nchi, nishati salama na uzalishaji wa bidhaa za viwandani. Naye Naibu Katibu Mkuu Kiliba akizungumza na hadhara kabla ya kutunuku hawala hizo sita alisifu kazi ya ubunifu iliyofanywa na UNCDF katika utoaji fedha kwa maendeleo ya jamii na kusema hiyo ndiyo njia sahihi ya kusababisha maendeleo. Pia aliwapongeza waanzishaji wa miradi walipookea kianzia cha mtaji wa uwekezaji kutoka UNCDF na kuwatakia mafanikio mema huku akisema kwamba serikali ya Tanzania inakaribisha uendelezwaji wa program ya LFI-Tanzania. 
  Kiliba alisema kwamba wizara yake imeanzisha kitengo maalumu cha kuhakikisha kwamba miradi ya ushirikiano wa sekta ya umma na binafsi katika halmashauri inafanikiwa.Mmoja wa wakurugenzi wa halmashauri waliopewa mtaji huo wa kianzio, Jenifa Omolo kutoka halmashauri ya mjui wa Kibaha alishukuru UNCDF kwa kufanikisha halmashauri ya Kibaha kuwa na soko la kisasa na kituo cha basi cha kisasa. 
  AlisemaUNCDF na Tamisemi wamekuwa mstari wa mbele katika kuwezesha kutekelezwa kwa wazo hilo kuanzia mwanzo hadi sasa wanapopata mtaji huo. Alihimiza halmashauri nyingine nchini kupata msaada wa kiufundi kwa mawazo yao kutoka UNCDF ili kuwa na uwezo wa kusimamia maendeleo ya umma na jamii. “Hatuna soko katika mji wetu, kuna magenge tu na tuna kituo kidogo tu cha mabasi ambacho hakikidhi mahitaji- hizi zimekuwa changamoto kubwa kwetu kwa zaidi ya miaka kumi. Mji wetu unakua na sasa tunahitaji kuwa na miundombinu ya kisasa” alisema Omolo na kuongeza kuwa mji wa Kibaha una wajibu wa kutoa huduma bora na kwamba miundombinu mipya na ya kisasa itasaidia kuongeza mapato kwa mji huo.

No comments: