Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa, Ban Ki Moon, akizungumza wakati wa Mkutano wa Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa kuhusu dhana ya wajibu wa kuwalinda raia, ambapo alisema licha ya kuasisiwa kwa dhana hiyo dunia bado imeendelea kushuhudia maisha ya watu wasiokuwa na hatia yakiendelea kupotea kwa sababu tu Jumuiya ya Kimataifa inashindwa kutumiza wajibu wake kwa wakati.
Balozi Tuvako Manongi akizungumza wakati wa Majadiliano ya Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa kuhusu dhana ya kuwalinda raia (R2P) majadiliano yaliyojielekeza katika kutathimini mafanikio na changamoto za utekelezi wa dhana hiyo ikiwa ni miaka kumi tangu kuasisiwa kwake.
Picha hii ya maktaba ni ya wakimbizi katika kambi moja nchini Tanzania, ambao jana jumanne akizungumza katika Mkutano wa Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa, Mwakilishi wa Kudumu wa Tanzania katika UN Balozi Tuvako Manongi amesema kutoka na wimbi kubwa linaloendelea la wakimbizi kukimbilia mataifa mengine kutafuta usalama wao. Jumuiya ya kimataifa haina budi kushirikiana na bila kubagua katika kuwalinda na utoaji wa huduma na misaada ya kibinadamu kwa wakimbizi.
Na Mwandishi Maalum, New York
Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, imetoa wito kwa Jumuiya ya Kimataifa wa kushirikiana katika wajibu wa kuwalinda na kuwapatia misaada ya kibinadamu, wakimbizi wanaokimbia machafuko, vita na migogoro katika nchi zao.
Wito huo umetolewa siku ya jumanne na Balozi Tuvako Manongi,Mwakilishi wa Kudumu wa Tanzania katika Umoja wa Mataifa, wakati Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa, lilipokutana kwa majadiliano ya siku moja kuhusu utekelezaji wa dhana juu ya wajibu wa kulinda raia (R2P) mafanikio na changamoto zake.
Dhana ya wajibu wa kuwalinda raia dhidi ya mauaji ya kimbari, uhalifu wa kivita, mauaji ya kikabila na uhalifu dhidi ya binadamu ilianzishwa mwaka 2005 wakati wa mkutano wa Kimataifa uliofanyika mwaka huu, ambapo viongozi wakuu wa nchi na serikali walikubaliana kwamba wajibu wa kwanza wa kuwalinda raia dhidi ya udhalimu wa aina yoyote ile ni wa serikali yenyewe husika.
No comments:
Post a Comment