Tuesday, September 22, 2015

CCM NDIO CHAMA KINACHOPENDWA ZAIDI NA WANANCHI

TAKWIMU zinaonyesha kwamba wananchi hawaelewi nafasi rasmi ya Ukawa
22 Septemba, Dar es Salaam: Asilimia 62 ya wananchi wanasema kwamba wanajisikia wapo karibu zaidi na chama cha CCM kuliko vyama vingine. 
 
Aidha, walipoulizwa watawachagua wagombea wa chama gani – bila kutajiwa majina ya wagombea – wananchi 6 kati ya 10 walisema kwamba watawachagua wagombea wa CCM kwa Urais (66%), Ubunge (60%) na Udiwani (60%). Takwimu hizi zinatoa picha kwamba CCM inaungwa mkono, kama ilivyokuwa mwaka 2012.

Chadema ni chama cha pili kinachopendwa kushinda vyama vingine vya upinzani. Lakini wananchi wanaosema kwamba watawachagua wagombea wa Chadema kwa Urais, Ubunge na Udiwani wamepungua kidogo. Ikumbukwe kuwa, inawezekana wananchi wanaopenda zaidi mseto wa Ukawa waliunga mkono vyama vya CUF, NCCR-Mageuzi au NLD.

Mbali ya CCM na vyama vinavyounda Ukawa, chama cha ACT-Wazalendo kilitajwa na zaidi ya asilimia moja ya wananchi.

Walipoombwa kutaja moja kwa moja jina la mgombea Urais ambaye wangemchagua, asilimia 65 ya wananchi walimtaja mgombea wa CCM, John Magufuli. Asilimia 25 walimtaja mgombea wa Chadema (na Ukawa), Edward Lowassa. Asilimia 10 iliyosalia iligawanyika kati ya wale waliomtaja mmoja miongoni mwa wagombea urais wengine, waliokataa kujibu na waliokuwa bado hawana mgombea waliyempendelea. Hata hivyo, takwimu zilikusanywa kabla vyama vingine, kikiwemo ACT-Wazalendo, kuteua wagombea wao wa Urais. Takwimu hizi (zilizokusanywa kati ya Agosti na Septemba) sio utabiri wa matokeo ya uchaguzi. Zinaonyesha tu kwamba mwanzoni mwa kipindi cha kampeni, mgombea Urais wa CCM, John Magufuli, alikuwa anaongoza katika kura za maoni.

Aidha, vigezo muhimu vinavyohusu makundi mbalimbali ya watu (demografia) vilitumika kuchambua ni nani au makundi gani yanayowaunga mkono John Magufuli na Edward Lowassa. Wahojiwa ambao walikuwa vijana zaidi, wasomi zaidi, wanaume na wakazi wa mijini, walimuunga mkono Edward Lowassa. Makundi ya wahojiwa wazee zaidi, waliokuwa na elimu ya msingi tu, wanawake na wakazi wa vijijini walielekea kumuunga mkono zaidi John Magufuli kuliko vijana zaidi, wasomi zaidi, wanaume au wanaoishi mijini.

No comments: