Wednesday, September 30, 2015

TASOI YAZINDUA KAMPENI YA SARATANI KWA KUTUMIA TEKNOLOJIA YA MAWASILIANO BILA MALIPO YOYOTE


Katibu Mkuu wa TASOI, Belinda Mlingo akizungumza na waandishi wa habari(hawapo pichani) wakati wa uzinduzi wa mpango mkakati endelevu wa kuendesha kampeni ya Mshikamano dhidi ya Saratani kwa kutumia technolojia ya mawasiliano bila malipo yoyote katika ukumbi wa Taasisi ya Saratani Ocean Road leo jijini Dar.
Mshauri kutoka Taasisi ya Saratani Ocean Road, Dk. Dominista Kombe ambaye akitoa takwimu ya wagonjwa wanaofika kutibiwa katika hospitali hiyo.
Mkurugenzi wa Idara ya Kinga Taasisi ya Saratani Ocean Road, Dk. Julius Mwaiselage  akizungumza jambo mbele ya waandishi wa habari(hawapo pichani) wakati wa uzinduzi huo uliofanyika katika ukumbi wa Taasisi ya Saratani Ocean Road leo.
 Waandishi wa habari wakiendelea kuchuka habari.
 Mkutano ukiendelea

Na Michael Maurus, Dar es Salaam
ASASI isiyo ya kiserikali ya Tanzania Social Outreach Initiative (TASOI), imezindua kampeni rasmi mpango mkakati endelevu wa kuendesha kampeni ya Mshikamano dhidi ya Saratani kwa kutumia teknolojia ya mawasiliano bila malipo yoyote.

Akizungumza leo jijini Dar es Salaam, Katibu Mkuu wa TASOI, Belinda Mlingo, alisema kuwa kampeni hiyo itatoa elimu, uhamasishaji na kutoa ushauri nasaha kwa wananchi kwa kupitia ujumbe mfupi wa simu (SMS).

Amesema kuwa katika kampeni hiyo, TASOI inashirikiana na wadau mbalimbali katika masuala ya afya, teknolojia na uhamasishaji wa jamii ili kutoa huduma hii muhimu bila malipo au gharama yoyote kwa watumiaji wa simu za mikononi.

“Kwa kumnukuu Mkurugenzi Mkuu wa Kitengo cha Magonjwa ya Yasiyoambukiza Wizara ya Afya, Profesa Ayoub Mgimba, ‘Hali halisi inadhihirisha kwamba magonjwa yasiyoambukiza kama saratani hivi sasa yamekuwa ni tatizo kubwa hasa katika nchi kama yetu ambapo ufahamu na mwamko ni mdogo sana juu mazingira hatarishi, viashiria, matibabu na matunzo ya wahanga wa magonjwa haya. Saratani inasababisha madhara makubwa ambayo yanaelekea kuwa majanga kwa jamii na kiuchumi kwa Taifa.”


Akielezea jinsi kampeni hiyo itakavyoendeshwa, Hellen alisema kuwa kwa muda wa miezi sita, watumiaji wa simu za mkononi za mitandao yote nchini, wataweza kupata taarifa za saratani kwa kupitia namba 15774 kwa kutuma neno CANCER au SARATANI kwenda namba hiyo na kuchagua lugha anayotaka kupokea taarifa hiyo, iwe ni Kiswahili au Kiingeza.

“Hapo utapokea ujumbe wenye elimu juu ya saratani, kati ya za viungo vya uzazi, yaani tezi dume, saratani ya matiti na shinga ya kizazi. Huduma hii itapatikana kupitia mitandao yote ya simu nchini, Vodacom, Airtel, Tigo, Zantel na TTCL,” alisema.

Ameongeza, “Tungependa pia kuwashirikisha wananchi wote kuchangia kwa hiyari ili tutimize malengo haya kwa pamoja. Na hii unaweza kuchangia Sh 1200 kwa mwezi au Sh 300 kwa wiki.

“Hili utaweza kulifanya kwa kukubali kupokea ujumbe mfupi kutoka kwetu ambao utakuwa na gharama ndogo ya Sh 150 tu. 

Pia unaweza kuchangia kupitia ezypesa, m-pesa, tigopesa, airtel money. Uchangiaji huu ni wa hiyari na hauzuii kupata huduma ya elimu ya saratani.”

Kwa upande wake, Daktari bingwa wa kwanza wa saratani mwanamke Tanzania, Dominista Kombe wa Ocean Road Cancer Istitute, amesema kuwa ni kweli saratani ni janga la jamii, hali halisi hapa Tanzania, saratani ni tatizo kubwa na linaongezeka kwa kasi, ni jumla ya ugonjwa wa HIV na ugonjwa wa TB, tatizo la saratani lilitakiwa kupewa kipaumbele zaidi.

“Tatizo jamii huwa haipo tayari kuweka wazi juu ya uginjwa huu kwa kuogopa aibu ya kutengwa, haya yote yakitokana na uhafamu mdogo juu ya ugonjwa huu,” amesema.

Amesema kuwa serikali imekuwa ikijitahidi kupambana na ugonjwa huu kwa kutoa huduma bure, lakini hata hivyo imejikuta ikishindwa katika kukabiliana nalo kwani tatizo ni kubwa mno, akiitaka jamii kusaidia katika vita hiyo kama walivyoamua kufanya TASOI waliokuja na mpango wao wa kampeni kupitia simu kuiwezesha jamii kujua juu ya viashiria vya janga hilo.

Amesema kuwa tatizo la saratani ni la dunia nzima, hivyo kuna ulazima wa jamii kujenga utaratibu wa kupima afya mara kwa mara kama ilivyo kwa nchi za Ulaya ambako imesaidia kupunguza ukubwa wa janga hilo kupitia chanjo.

Amesema kuwa Ocean Road hupokea wagongwa wapya 5000 kwa mwaka, kati yao asilimia 80, wanafika wakiwa katika hali mbaya kiasi kwamba hupewa tiba ya kuwaongezea siku tu, huku asilimia ndogo sana, huwahi na kupewa tiba inayowawezesha kuishi.

No comments: