Friday, September 25, 2015

MGOMBEA UBUNGE JIMBO LA KIBAHA KULIVALIA NJUGA SUALA LA CHANGAMOTO YA WAKINAMAMA WAJAWAZITO

 Mgombea wa jimbo la kibaha mjini kupitia chama cha mapinduzi (CCM) Sylivesta Koka akisalimiana na wananchi wa kata ya msangani kabla ya kuanza kwa mkutano wa hadhara wa kampeni za uchaguzi.
 Wananchi wakiwa wanashangilia jambo katika mkutano huo wa hadhara.(Picha zote na Victor Masangu)
 Mwenyekiti wa CCM Wilaya ya Kibaha Maulid Bundala akiwaonyesha wananchi waliohudhulia katika mkutano huo moja ya  kadi ya chadema iliyorudishwa na mwanachama wa chadema, kulia kwake ni mgombea ubunge jimbo la Kibaha mjini Silvestry Koka.

NA VICTOR MASANGU, KIBAHA
MGOMBEA ubunge wa jimbo la Kibaha mjini Silvestery Koka amesema kwamba endapo akichaguliwa na wananchi  atahakikisha analivalia njuga suala la changamoto inayowakabili wakinamama  wajawato kwa kujenga wodi za kujifunguliwa pamoja na kuongeza vifaa tiba sambamba na kupatiwa matibabu bure  ili kupunguza ongezeko la vifo.
 
 
Akizungumza katika mkutano wa hadhara wa kampeni kwa wananachi wa kata ya Msangani mgombea huyo amesema kwamba wakinamama wajawazito wamekuwa wakipata usumbufu mkubwa wakati wa kujifungua na wakati mwingine wanapoteza maisha  hivyo ataweka mikakati madhubuti ya kuboresha huduma ya afya lengo ikiwa ni kuokoa maisha yao.
 
Koka amebainisha kwamba mpango huo upo katika ilani ya chama cha mapinduzi na utekelezaji wake tayari umeshaanza kufanyika sambamba na kuongeza kasi ya ujenzi wa zahanati ili kuweza kuwasogezea huduma kwa urahisi wananchi wasipate shida ya kupatiwa matibabu.
 
Aidha alisema kwamba katika kuboresha sekta ya afya ataweka utaratibu mzuri wa kuhakikisha wazee wote wanapatiwa matibabu bure bila ya kupaata usumbufu wowote na kuwa atakuwa anafanya ziara za mara kwa mara kutembelea zahanati vituo vya afya pamoja na hospititali ili kuweza kubaini changamoto.
 
Akizungumzia kuhusiana na changamoto ya  maji katika kata ya Msangani mgombea pamoja na mikakati yake aliyojiwekea kuondokana na kero hiyo mgombea huyo alisema kwa sasa kuna miradi ya maji ipatayo  14   ambayo  imeshatekelezwa kwa kipindi cha miaka mitano iliyopita na lengo la kuweza kutatua changamoto ya maji.
 
 Kwa upande wao wananchi wa kata hiyo ya Msangani akiwemo Said Mohamed na  Rashid Abed  awakusita kuzungumzia  changamoto zinazowakabili hususan suala la maji ambalo kwa upande wao limekuwa ni kero kubwa kutokana na kutembea umbali wa kilometa nane kwa ajili ya kwenda kufuata  maji.
 
Walisema kwamba kwa sasa wana imani endapo mradi huo wa maji ukikamilika utaweza kuwanufaisha kwa kisi kikubwa na kutatua kero ya maji ambayo imekuwa ni kilio cha siku nyingi kwa wakazi wa kata ya msangani.
 
“Kwa upande wetu kwa sasa tunaona juhudi ambazo zinafanywa na mbunge ambaye alimaliza muda wake tumeshuhudia baadhi ya maeneo wameshaaza kupata maji safi na salma hivyo kitu kikubwa kwa mgombea ambaye tutamchagua alitilie mkazo suala la maji ili tusiweze kusumbuka kutembea umbali mrefu,”alisema wananchi hao.
 
Wananchi wa kata ya Msangani kwa sasa bado  wanakabiliwa na  changamoto mbali mbali katika sekta ya afya hususan wakinamama wajawazito pamoja na huduma ya maji hivyo kunahitajika kufanyike  juhudi za makusudi kwa viongozi watakaochaguliwa kuhakikisha    wanatafuta njia mbadala kuzitatua kero hizo.

No comments: