Wednesday, September 30, 2015

MAENDELEO ENDELEVU 17 YA DUNIA YAZINDULIWA TANZANIA

IMG_3349Mratibu wa Mashirika ya Umoja wa Mataifa na Mwakilishi Mkazi wa UNDP Bw. Alvaro Rodriguez (kulia) na Mwakilishi Mkazi wa Shirika la Umoja wa Mataifa la UN Women nchini Tanzania, Anna Collins-Falk (katikati) wakipata picha ya kumbukumbu sambamba na mmoja wa wadau wa maendeleo.

(Picha na Zainul Mzige wa Modewjiblog).
………………………………
Na Mwandishi wetu
UMOJA wa Mataifa kwa kushirikiana na Serikali ya Tanzania wamezindua rasmi malengo ya Maendeleo Endelevu 17 ( SDGs).
Malengo hayo ambayo pia yanajulikana kama malengo ya dunia yamezinduliwa jana Septemba 29 katika hoteli ya Serena jijini Dar es salaam.
Uzinduzi huo ulifanywa na Mratibu wa Mashirika ya Umoja wa Mataifa na Mwakilishi Mkazi wa UNDP Bw. Alvaro Rodriguez, Kamishina wa mipango (POPC) Bw. Paul Kessy, na Kamishina wa Mipango wa Zanzibar, Bw. Ahmed Makame kwa niaba ya serikali, Bi. Fionnuala Gilsenan, Balozi wa Ireland na Bi. Liz Lloyd, Ofisa Mtendaji Mkuu wa Benki ya Standard Chartered Tanzania kwa niaba ya wadau wa mradi wa Project Everyone Partners.
SDGs ni wito wa dunia wa kuchukuliwa kwa hatua za kuufuta umaskini, kuihami dunia dhidi ya uharibifu wa mazingira na kuhakikisha kwamba kila mwanadamu anaishi maisha stahiki katika amani na ustawi.
Katika malengo hayo 17 yapo makusudio 169 yanayotoa ramani ya utengenezaji wa sera za maendeleo na namna ya kutekeleza kwa miaka 15 ijayo.
Malengo hayo yakijengwa juu ya mafanikio ya malengo ya milenia (MDGs), yameingiza vitu vipya kama mapambano dhidi ya tofauti za kiuchumi, ubunifu, mabadiliko ya tabia nchi, lishe, amani na haki. SDGs ni mpango wa dunia unaojikita kwa ustawi wa wanancni na dunia.
IMG_3303Mkurugenzi Mkazi wa Shirika la Maendeleo (UNDP), Awa Dabo (kushoto) na Kiongozi wa mabalozi wa nchi za nje hapa nchini Mheshimiwa Juma Mpango, ambaye ni balozi wa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (DRC) wakiwa wameshikilia lengo namba 16 na 17 kati ya malengo 17 ya Maendeleo Endelevu ya Dunia ambayo yamezinduliwa rasmi nchini Tanzania jana 29, Septemba 2015.
Akizungumza umuhimu wa malengo hayo, Mratibu wa Mashirika ya Umoja wa Mataifa nchini na Mwakilishi wa UNDP Bw. Alvaro Rodriguez amesema: “Kwa mara ya kwanza katika historia ya dunia , serikali zimekutana na kukubaliana kupeana malengo kwa ajili ya kila mtu. Malengo haya yatasaidia mataifa yote kushirikiana katika kuwezesha ustawi, kupunguza matumizi na kuilinda dunia dhidi ya mabadiliko ya tabia nchi.Katika hilo watashughulikia elementi zinazohusu maendeleo endelevu: ukuaji wa uchumi, ustawi wa jamii na kulinda mazingira.”
Akizungumzia malengo hayo Bw. Paul Kessy amesema kwamba serikali ya Tanzania ipo tayari kwa malengo hayo.
Alisema kwamba Rais Jakaya Kikwete alikuwa New York, Marekani kwa ajili ya kutia saini malengo hayo na hilo linaonesha ni kiasi gani serikali ya Tanzania iko tayari kushirikiana na wadau wengine kuufuta umaskini.
Pia alisema:“Wakati huu, masuala ya uimarishaji wa muundo wa utekelezaji na kuamsha upya ushirikiano wa kidunia katika maendeleo ni msingi mzuri”
Naye Kamishina wa mipango wa Zanzibar, Bw Ahmed Makame : “Nikiangalia malengo haya 17 ya SDGs, ninafuraha kuona kwamba Zanzibar imekuwa sehemu ya mchakato huu…”.

No comments: