Bendera ya Palestine itapepea nje ya Makao Makuu ya Umoja wa Mataifa, hii inafuatia Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa kupitisha azimio ambalo linatoa fursa kwa nchi ambazo si mwanachama kamili wa Umoja huo kupeperusha bendera yake Makao Makuu ya Umoja wa Mataifa.
Ubao wa Matangazo ndani ya Ukumbi Mkuu wa Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa, ukionyesha matokeo ya kura katika tukio la kihistoria kufanyika ambapo Baraza hilo limepitisha azimio linalotoa fursa kwa Palestina kupeperusha bendera yake. Nchi wanachama walipiga makofi kushangilia kupitishwa kwa azimio hilo, ambalo Israel imesema Palestina inatafuta umaarufu kwa njia za mkato badala ya kurejea kwenye meza ya mazugumzo.
Na Mwandishi Maalum New York
Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa, jana Alhamis, limepitisha Azimio ambalo kwa mara ya kwanza tangu kuanzishwa kwa Umoja huo, litaruhusu nchi ambazo siyo mwanachama kamili kupeperusha bendera yake katika Makao Makuu ya Umoja wa Mataifa.
Kupitishwa kwa azimio hilo ambalo limepigiwa kura za ndiyo 119 za hapana nane na zisizofungamana na upande wowote 45 kunaipa fursa Palestina kupeperusha bendera yake nje ya Makao Makuu ya Umoja wa Mataifa.
Mara baada ya matokeo ya kura kutangazwa rasmi, Wajumbe wa Mkutano wa Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa walipiga makofi kama ishara ya kufurahia kupitishwa kura nyingi azimio hilo.
Palestina kama ilivyo kwa Vatican inahadhi ya Nchi Mwangalizi isiyo Mwanachama wa Umoja wa Mataifa (Non -Member Observer States)
Kwa mujibu wa Azimio hilo nambaA/69/L.87 linaloelezwa kuwa ni la kihistoria, linamtaka Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa kuhakikisha kwamba Bendera ya Palestina inapeperushwa ndani ya siku 20 ( septemba 30)wakati wa Mkutano wa Baraza Kuu la 70 la Umoja wa Mataifa.
Akiwasilisha azimio hilo mbele ya wajumbe, Mwakilishi wa Kudumu wa Iraq na ambaye ni mwenyekiti wa kundi la nchi za kiarabu alisema kupeperushwa kwa bendera ya Palestina ni kielelezo cha utekelezaji wa matakwa yaliyomo ndani ya Katiba ya Umoja wa Mataifa ya kwamba, nchi zote na watu wake wako sawa na wana haki sawa.
No comments:
Post a Comment