Wednesday, July 20, 2016

MAKAMU WA RAIS AZINDUA RIPOTI YA LISHE YA DUNIA LEO JIJINI DAR ES SALAAM


Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Samia Suluhu Hassan akihutubia wakati wa Uzinduzi wa Ripoti ya Lishe ya Dunia kwenye mkutano uliofanyika jijini Dar es Salaam.
Waziri wa Afya,Maendeleo ya Jamii,Jinsia,Wazee na Watoto Mhe.Ummy Mwalimu akizungumza kwenye mkutano wa kuzindua ripoti ya lishe ya Dunia ambao mgeni rasmi alikuwa Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano Mhe. Samia Suluhu Hassan.
Baadhi ya Wadau wakifuatilia kwa makini mkutano huo wa uzinduzi ya ripoti ya Lishe ya Dunia.
Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Samia Suluhu Hassan (kulia) akikata utepe kuashiria kuzindua ripoti ya Lishe ya Dunia, katkati ni Waziri wa Afya,Maendeleo ya Jamii,Jinsia,Wazee na Watoto Mhe.Ummy Mwalimu na Mkurugenzi Mtendaji wa PANITA ,Dkt. Tumaini Mikindo

Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Samia Suluhu Hassan amesema serikali ya awamu ya TANO itatoa msukumo mkubwa katika kukabiliana na tatizo la utapiamlo nchini kwa kuweka mipango na mikakati imara ikiwemo kuongeza bajeti ya lishe, kuongeza virutubisho kwenye vyakula na kutumia vyema wataalamu wa lishe katika kupambana na tatizo hilo hapa nchini.

Makamu wa Rais Samia Suluhu Hassan ametoa kauli hiyo jijini Dar es Salaam Trh 20-Jul-16 katika hotuba yake ya uzinduzi wa Ripoti ya Dunia ya Utapiamlo ambayo imetilia mkazo masuala ya lishe kama msingi wa Maendeleo hapa nchini na Duniani kwa ujumla.

Makamu wa Rais amesema viongozi wa serikali katika ngazi zote za wilaya na mikoa wanatakiwa kuunga mkono jitihada za kuondoa utapimlo nchini kwa kuweka msukuko wa kipekee katika ngazi zote za maamuzi.Ameeleza kuwa jitihada zinazofanywa na serikali kwa ushirikiano na wadau wa Maendeleo wa Ndani na Nje ya Nchi zimesaidia kwa kiasi kikubwa kushusha kiwango cha udumavu nchini kutoka asilimia 42 mwaka 2010 hadi kufikia asilimia 34 mwaka 2015.

Amefafanua kuwa kutokana na mafanikio hayo, serikali imetoa mwongozo wa bajeti ya mwaka 2016/17 kwa kutenga kiasi cha shilingi milioni 500 kwa ajili ya masuala ya lishe kwa kila mtoto wa umri chini ya miaka MITANO hapa nchini

Makamu wa Rais Samia Suluhu Hassan amesema pamoja na fedha hiyo kuwa kidogo lakini serikali itaendelea kuongeza kiasi cha fedha kwenye bajeti zijazo hadi kufikia kiasi cha dola 8.5 sawa na shilingi elfu 18000 kwa kila mtoto hapa nchini kama ilivyoshauriwa na jopo la wataalamu wa Benki ya Dunia na wa masuala ya afya na uchumi duniani.

Makamu wa Rais pia ameziagiza Halmashauri zote Nchini kupitia TAMISEMI zihakikishe zinatumia fedha hizo vizuri na kwa malengo yaliyokusudiwa na sio vinginevyo.

No comments: