Monday, March 28, 2016

RAIS MAGUFULI AMWAPISHA RC SONGWE, APOKEA TAARIFA YA CAG YA 2014/15


Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe Magufuli amemwapisha Mkuu wa mkoa mpya wa Songwe Luteni Mstaafu Chiku Gallawa, ambaye hakuapishwa pamoja na wakuu wa mikoa wenzake Machi 15, 2016.

Uapisho huo umefanyika leo tarehe 28 Machi, 2016 Ikulu Jijini Dar es salaam, na kuhudhuriwa na Makamu wa Rais Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan na Waziri Mkuu Mheshimiwa Kassim Majaliwa.

Luteni Mstaafu Chiku Gallawa anakuwa Mkuu wa Mkoa wa kwanza kwa Mkoa mpya wa Songwe, ulioanzishwa kwa kuugawa mkoa wa Mbeya, Kusini mwa Tanzania.

Wakati huo huo, Rais Dkt. John Pombe Magufuli amepokea taarifa ya ukaguzi wa hesabu za serikali ya mwaka 2014/2015 kutoka kwa Mkaguzi na Mdhibiti Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG) Prof. Mussa Assad, Ikulu Jijini Dar es salaam.

Rais Magufuli amepokea taarifa hiyo yenye ripoti tano, ikiwa ni utaratibu wa kikatiba unaomtaka Mkaguzi na Mdhibiti Mkuu wa Hesabu za Serikali, kukabidhi kwa Rais taarifa ya ukaguzi kabla ya mwisho wa mwezi Machi.

Baada ya kupokea taarifa hiyo, Rais Magufuli ataikabidhi mbele ya bunge katika siku saba za mwanzo za kikao kijacho cha Bunge kitakachofanyika Mjini Dodoma.Rais Magufuli amempongeza Mkaguzi na Mdhibiti Mkuu wa Hesabu za serikali na timu yake kwa kuandaa taarifa hiyo, na ametoa wito kwa chombo hicho kuendelea kufanya kazi kwa uhuru na ufanisi, huku akiahidi kuwa serikali itatoa ushirikiano wa kutosha kufanikisha kazi zake.

Gerson Msigwa
Kaimu Mkurugenzi wa Mawasiliano, IKULU
Dar es salaam

28 Machi, 2016

No comments: