Thursday, March 10, 2016

WAZIRI MKUU AWAHAKIKISHIA FURSA ZA UWEKEZAJI WA VIETNAM

Na Anitha Jonas – MAELEZO
Dar es Salaam.
Waziri Mkuu wa Serikali ya Jamhuri ya Muungano Tanzania Mheshimiwa Kassim Majaliwa amewahakikishia wawekezaji kutoka Vietnam kuwepo kwa fursa za uwekezaji nchini.
Majaliwa ameyasema hayo jana katika kongamano la ujumbe wa Rais wa Vietnam Mheshimiwa Troung Tan Sang pamoja na wadau wa uwekezaji kutoka nchini humo ambapo wanatarajia kufanya ziara ya siku nne nchini wakitazamia fursa za uwekezaji nchini.
“Nchi yetu inamazingira mazuri ya uwekezaji, usalama wakutosha na pia kuna uhahika wa soko kwani ipo mikataba ya kikanda ya kukuza masoko katika nchi wanachama kama EAC na SADC kwani katika nchi hizo kuna watu zaidi ya milioni 300”, alisema Majaliwa.
Akiendelea kuzungumza na wawekezaji hao Waziri Mkuu alisema serikali ya Tanzania imekuwa ikiboresha Mazingira ya uwekezaji nchini na hiyo imechangia ongezeko la wawekezaji.
Mbali na hayo Majaliwa alisema serikali imekuwa ikiboresha sheria na kuimarisha ushirikishwaji wa wadau wa sekta binafsi lengo likiwa ni kuchochea mazingiraya uwekezaji ikiwa ni kuimarisha uchumi wa taifa pamoja na kukuza kipato cha kila mtanzania.
Hata hivyo Waziri Mkuu aliipongeza Kampuni ya VIETTEL Tanzania Ltd kutoka Vietnam ambayo imewekeza katika Sekta ya Mawasiliano kwani imewasaidia watanzania wengi wa vijijini kupata mawasiliano.

No comments: