Friday, October 09, 2015

DENMARK IMEAHIDI KUENDELEA KUIUNGA MKONO ZANZIBAR KATIKA HARAKATI ZAKE ZA KIUCHUMI

 Balozi Mpya wa Denmark Nchini Tanzania Einar Hebogard Jensen akisalimiana na Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Ali Iddi Ofisini kwa Balozi Seif Vuga Mjini Zanzibar alipofika kujitambulisha rasmi.
 Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Ali Iddi Ofisini kwa Balozi Seif akibadilishana mawazo na Balozi Mpya wa Denmark Nchini Tanzania Bwana Einar Hebogard Jensen.

Picha na –OMPR – ZNZ.                 
DENMARK imeahidi kuendelea kuiunga Mkono  Zanzibar katika harakati zake za Kiuchumi na Maendeleo kwa lengo la kudumisha uhusiano wa kihistoria wa muda mrefu uliopo kati ya pande hizo mbili.

Kauli hiyo imetolewa na Balozi Mpya wa Denmark  Nchini Tanzania Bwana Einar Hebogard Jensen wakati  akizungumza na Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Ali Iddi Ofisi kwake Vuga Mjini Zanzibar  akijitambulisha rasmi baada ya kuanza kazi yake ya Kidiplomasia kwa takriban miezi sita sasa.

Balozi Hebogard alisema  Denmark na Zanzibar pamoja na Tanzania kwa ujumla zimekuwa na uhusiano wa muda mrefu mara baada ya Uhuru wa Tanganyika na Mapinduzi ya Zanzibar ya Mwaka 1964 jambo ambalo Nchi hiyo imemua kuendelea  kusaidia Nyanja za Kiuchumi na Kijamii.

Alisema Denmark kupitia shirika lake la misaada ya Maendeleo la { DANIDA } pamoja na miradi tofauti inayosimamia  limekuwa likijikita zaidi katika kusaidia Sekta ya Elimu Nchini.

Balozi Mpya huyo wa Denmark Nchini Tanzania  ameelezea kuridhika kwake na mazingirabora pamoja na rasilmali nyingi zilizopo Tanzania na Zanzibar kwa ujumla.
Mapema Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Ali Iddi aliipongeza Denmark  kwa jitihada zake za kusaidia sekta ya Elimu katika kuimarisha majengo ya skuli mbali mbali Unguja na Pemba.

Balozi Seif alisema katika kuendeleza uhusiano wa pande hizo mbili alimuomba Balozi Einar Hebogard  Jensen kutumia nafasi yake katika kuwashawishi wawekezaji wan chi kutumia fursa ya uwekezaji hapa Zanzibar.

Alisema Zanzibar katika azma yake ya kuimarisha uchumi tayari imeshaimarisha miundombinu mbali mbali ikiwemo ile ya Sekta ya Utalii inayoonekana kukua na kusaidia pato la Taifa.

Othman Khamis Ame
Ofisi ya Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar
9/10/2015.


No comments: