Tuesday, October 20, 2015

DK. MAGUFULI AZURU MAKABURI YA BABU NA BIBI YAKE, KATOMA – GEITA VIJIJINI

Mgombea urais wa Jamhuri ya Muungano kwa Tiketi ya CCM, Dk. John Magufuli, akielekea katika makaburi ya makaburi ya babu na bibi yake mzaa wa baba, eneo la Katoma, wilayani Geita Vijijini huku akiwa ameambatana na ndugu zake ikiwemo baba zake wadogo na mama zake wadogo.
Mgombea urais wa Jamhuri ya Muungano kwa Tiketi ya CCM, Dk. John Magufuli, akiwa katika makaburi ya makaburi ya babu na bibi yake mzaa wa baba, eneo la Katoma, wilayani Geita Vijijini akiwatambulisha ndugu zake ikiwemo baba yake mdogo, Michael Magufuli.
Enao la Makaburi ya familia ambapo huwa wanazikwa na hapo ndipo kuna kaburi la babu na bibi yake ikiwemo ndugu zake wengine.
Dk. Magufuli akiongoza ibada ndogo ya kuwaombea dua.
Mgombea urais wa Jamhuri ya Muungano kwa Tiketi ya CCM, Dk. John Magufuli, akionyesha moja ya kaburi la ndugu zake.
Baada ya kumaliza dua… akielekea kuongea na wanakijiji wa eneo la Katoma.
Dk. John Magufuli akiwaomba kura wakazi wa Katoma, wilaya ya Geita Vijijini.,
Ujumbe wa wanaKatoma wakati wakimsikiliza Mgombea urais wa Jamhuri ya Muungano kwa Tiketi ya CCM, Dk. John Magufuli.
— 
Dk. Magufuli alifika nyumbani kwa babu yake saa 6.30 mchana na kupokewa na baba yake mdogo, Michael Magufuli, kabla ya kupelekwa kwenye makaburi hayo, ambako aliongoza ibada ndogo ya kuwaombea dua.

Akizungumza kwenye eneo hilo, Michael alisema makaburi hayo ni ya babu na bibi wa mgombea huyo pamoja na ndugu zake wengine, waliofariki dunia miaka mingi iliyopita.

Michael alisema asili ya ukoo wa Dk. Magufuli ni Katoma, ambako ndiko baba yake alikozaliwa kabla ya kuhamishia makazi yake Chato.

“Tumezoea kumuona ndugu yetu kwenye tv na kumsikiliza kwenye redio, leo tumefurahi kumuona yeye mwenyewe,”alisema na kuongeza kuwa wanamuombea dua kwa Mungu ili aweze kuchaguliwa kuwa rais wa awamu ya tano ya serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

Kwa upande wake, Dk. Magufuli alisema amefarijika kufika tena katika eneo hilo kwa sababu ndiko alikozaliwa na kukulia na pia ndiko ukoo wake ulikoanzia.

Dk. Magufuli alitumia fursa hiyo kuwatambulisha ndugu zake kwa wanahabari kabla ya kuingia kwenye nyumba ya familia, iliyoko umbali wa mita 30 kutoka barabara itokayo Kamanga kwenda Sengerema.

Mgombea huyo alisema jina la Pombe alipewa na bibi yake, aliyemtaja kwa jina la Anastazia, siku alipoivisha pombe yake.

Alisema babu yake, marehemu Michael, alifariki dunia akiwa na umri wa miaka 1.3 baada ya kumuuguza kwa muda mrefu akiwa Dar es Salaam na baadaye kumrejesha Katoma.

“Kwangu siku hii ni ya pekee. Nilipojua kwamba nitasafiri kwa kutumia njia hii, niliona ni lazima nipite hapa kwa sababu ndiko maisha yangu yalikoanzia,”alisema Dk. Magufuli na kusifu maendeleo yaliyopatikana katika kijiji hicho, ikiwemo nishati ya umeme.

Aliwaomba wakazi wa kijiji hicho wamuombee dua kwa Mungu ili aweze kushinda kiti cha urais, katika uchaguzi mkuu wa rais, wabunge na madiwani, unaotarajiwa kufanyika nchi nzima Jumapili.

Akihutubia mkutano uliofanyika kijiji cha Nkome, Jimbo la Geita Vijijini mkoani Geita, mgombea huyo alisema mikutano aliyoifanya katika mikoa yote nchini, imemuhakikishia kupata ushindi wa tsunami katika uchaguzi mkuu wa mwaka huu.

Alisema kote alikokwenda, wananchi wamemuhakikishia kumpigia kura kwa wingi kutokana na kuvutiwa na sera zake, hivyo kumuhakikishia ushindi wa kishindo, ambao  ameufananisha na tsumani.

Aidha, mgombea huyo alisema serikali yake itaboresha uvuvi wa samaki katika Ziwa Victoria kwa kuwakopesha wavuvi zana za kuvulia samaki.

Alisema lengo la serikali yake ni kuona wavuvi wanafanya biashara na kutajirika, tofauti na ilivyo sasa.

Aidha, alisiema serikali yake imepania kufufua viwanda vyote vilivyokufa ili kuongeza ajira kwa vijana na pia kuongeza bei ya zao la pamba ili wakulima waweze kunufaika na kilimo cha zao hilo.

Aliyataja malengo mengine ya serikali yake kuwa ni kuongeza thamani ya matunda yanayolimwa hapa nchini kwa kujenga viwanda vya juisi ili kuondokana na ununuzi wa juisi kutoka nje ya nchi.

“Haiwezekani tukaendelea kuagiza juisi kutoka nje. Ninaposema serikali yangu itakuwa ya viwanda, hiyo ndio dhamira yangu,”alisema.

No comments: