Tuesday, October 08, 2013

Ikulu yaanza mawasiliano na viongozi wa vyama vya siasa nchini vyenye hoja kuhusu Muswada wa Sheria ya Marekebisho ya Sheria ya Mabadiliko ya Katiba

                          THE UNITED REPUBLIC OF TANZANIA

                                                  DIRECTORATE OF PRESIDENTIAL COMMUNICATIONS

Ofisi ya Rais, Ikulu, imeanza mawasiliano na viongozi wa vyama vya siasa nchini vyenye hoja kuhusu Muswada wa Sheria ya Marekebisho ya Sheria ya Mabadiliko ya Katiba uliopitishwa karibuni na Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa nia ya kuandaa mkutano kati ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Jakaya Mrisho Kikwete  na viongozi wa vyama hivyo.

Mawasiliano hayo yameanza Jana, Jumatatu, Oktoba 7, 2013, kufuatia maelekezo ya Rais Kikwete kwa Ofisi ya Katibu wa Rais.

Kufuatia matukio yaliyotokea Bungeni wakati wa kujadiliwa na kupitishwa kwa Muswada huo mwezi uliopita, na maneno na kauli mbali mbali ambazo zimetolewa na wabunge wa vyama vya upinzani na wadau wengine kufuatia kupitishwa kwa Muswada huo na Bunge, Rais Kikwete katika hotuba yake kwa wananchi Ijumaa iliyopita, Oktoba 4, 2013, alisema kuwa hoja na kauli za wanaopinga Muswada huo zinazungumzika kwa nia njema ya kutafuta mwafaka katika mchakato wa kutafuta Katiba Mpya.

Kwa mujibu wa maandalizi hayo, Ofisi ya Rais, Ikulu inaangalia uwezekano wa kuitisha mkutano huo Jumapili ya Oktoba 13 ama Jumanne ya Oktoba 15, mwaka huu.


Imetolewa na:
Kurugenzi ya Mawasiliano ya Rais,
Ikulu.
Dar es Salaam.
 7 Oktoba, 2013

No comments: