Monday, November 16, 2015

KAMATI KUU YATEUA WATATU USPIKA

Katibu wa NEC Itikadi na Uenezi Nape Nnauye akizungumza na waandishi wa habari nje ya ukumbi wa NEC ,CCM Makao Makuu Dodoma akiwa ameshikilia kitabu cha Kanuni za Kamati ya Wabunge Wote wa Chama Cha Mapinduzi.
Kamati Kuu ya
Halmashauri Kuu ya Taifa ya CCM katika kikao chake cha siku moja kilichofanyika
jana Novemba 15, 2015 mjini Dodoma imewateua wana-CCM watatu watakaopigiwa kura
na wabunge wote wa CCM ili kumpata mgombea wa CCM katika nafasi ya Spika wa
Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.
Walioteuliwa
kugombea nafasi hiyo na Kamati Kuu iliyofanyika chini ya Mwenyekiti wa CCM,
Rais Mstaafu Dkt. Jakaya Mrisho Kikwete ni pamoja na Naibu Spika aliyemaliza
muda wake Ndugu JOB NDUGAI, Dkt. TULIA ACKSON na Ndugu ABDULAH MWINYI.
Kwa upande wa Naibu
Spika wa Bunge, mchakato wa kuchukua fomu kwa wabunge wa CCM wanaoomba ridhaa
kugombea nafasi hiyo utaanza leo Novemba 16, 2015 na kukamilika Novemba 17,
2015 saa kumi kamili jioni.
Wana-CCM hao watatu watapigiwa kura na Kikao cha Kamati ya Wabunge wote wa CCM kitakachofanyika
kesho Novemba 16, 2015 saa nne asubuhi katika ofisi za Makao Makuu ya CCM
Dodoma ilikuchagua jina moja kugombea nafasi hiyo katika Bunge la Jamhuri ya
Muungano.
Kuhusu nafasi ya Naibu Spika, alisema kulikuwa na kasoro za
kutofuata kanuni za chama ambapo hadi jana ni mwanachama mmoja tu ndiye
aliyekuwa amechukua fomu ya kugombea ambaye ni Mbunge wa Ilala, Mussa Azzan ‘Zungu,’
lakini atatakiwa kuchukua fomu upya.
“Ibara ya 57, Kanuni za kamati ya wabunge wote wa CCM toleo
la 2010 toleo la nne 2011, mbunge yeyote anayetaka kugombea nafasi ya Naibu
Spika atatakiwa kuchukua fomu kupitia kamati hiyo na atairudisha kisha kamati
itakaa kupata jina moja,” alisema Nape.
Kwa mujibu wa maelezo hayo mbunge wa chama hicho anayetaka
kugombea Unaibu Spika, atatakiwa kuchukua fomu leo Novemba 16, kwa ada ya Sh
100,000 kisha atairudisha kesho Novemba 17, ndipo kamati itakaa kuchambua na kupitisha
jina moja.
 Waandishi wa habari wakimsikiliza Katibu wa NEC Itikadi na Uenezi Nape Nnauye nje ya ukumbi wa NEC mjini Dodoma ambapo majina matatu yalipitishwa.

No comments: