Monday, November 16, 2015

HUDUMA ZA MRI NA CT-SCAN ZASITISHWA KWA MUDA MUHIMBILI

Huduma za uchunguzi kupitia mashine ya MRI (Magnetic Resonance Imaging) katika
Hospitali ya Taifa Muhimbili (MNH) zimesimamishwa kwa muda kuanzia leo Novemba 16 kwa
ajili ya matengenezo zaidi.
Taarifa imetolewa LEO kwa vyombo vya habari na Mkuu wa Kitengo cha Mawasiliano ya
Umma na Huduma kwa Wateja wa MNH, Aminiel Aligaeha imesema matengenezo
hayo yataenda sambamba na matengenezo ya CT-Scan na kwamba tayari uongozi wa hospitali hiyo umewasiliana na Kampuni ya Philips ambayo ina mkataba wa kufanya matengenezo ya mashine  hizo.
“Mtakumbuka kwamba wiki iliyopita tuliwatangazia wananchi kuwa huduma za MRI
zimeanza kutolewa baada ya mashine hiyo kutengenezwa na kuanza kufanya kazi, hata hivyo
mashine ya MRI baada ya kufanya kazi Novemba 11 na tarehe 12 ilionekana kwamba ina hitilafu ya kiufundi ambayo inahitaji matengenezo zaidi, hivyo  iliyotulazimu kuisimamisha kufanya kazi  kuanzia Novemba 13 majira ya mchana.
Alisema baada ya uchunguzi wa kina mafundi wamegundua hitilafu kwenye mashine ya MRI
ambapo kifaa kimoja kinachoitwa RF Amplifier kimeharibika na inabidi kiwekwe kingine, kifaa
hicho kazi yake ni kuipatia mashine hiyo mawimbi ya sauti (radio frequency ) ambazo
zinahitajika katika sehemu nyingine za mashine ili kuiwezesha kufanya kazi yake vizuri,” amesema Aligaesha.
Akifafanua Aligaesha amesema kwa upande wa CT-Scan , uchunguzi wa mafundi
umeonyesha kuwa ina hitilafu kwenye vifaa viwili ambapo kifaa kinachoitwa Image re-const
Ructor( Server) kinachohusika kutengeneza picha kimeharibika na kifaa kingine kiitwacho
Inverter Power Supply kinachohusika kupeleka umeme wenye kiwango kinachohitajika kwenye
mashine kimeharibika.
Vifaa hivyo havipatikani nchini, hivyo vimeagizwa kwa hati ya dharura nchini Uholanzi
kwa mtengenezaji wa mashine hizo ambaye ni Philips na vinatarajiwa kuwasili nchini ndani ya
wiki hii.
“Tunawaomba wateja wetu wawe watulivu wakati huu ambapo suala hili tunalishughulikia” amesema  Aligaesha

No comments: