Tuesday, August 25, 2015

NYUMBU KUENDELEA KUWAWEZESHA WANANCHI KUJIINUA KIUCHUMI

1
Mkurugenzi Mkuu wa Shirika la NYUMBU (Tanzania Automative Technology Centre) Brigedia Jenerali Anselim akiongea na waandishi wa Habari (hawapo pichani) kuhusu miradi mbalimbali iliyotekelezwa na shirika hilo inayodhamiria kuwawezesha wananchi kiuchumi ikiwemo utengenezaji wa matrekta madogo( power Tiller) ambayo yanalenga kumkomboa mkulima hapa nchini kwa kuondokana na matumizi ya jembe la makono.
2
Baadhi ya waandishi wa habari wakimsikiliza Mkurugenzi Mkuu wa Shirika la NYUMBU (Tanzania Automative Technology Centre) Brigedia Jenerali Anselim.
3
Mkuu wa Kitengo cha Mawasiliano Serikalini wa Wizara ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa Luteni Kanali Juma Nkangaa Sipe akiongea na Waandishi wa Habari (hawapo pichani) umuhimu wa kutoa habari za kuelimisha kwa jamii hasa zitakazowawezesha kuwajengea uwezo wa kimaarifa na kuwainua kichumi kupitia elimu hiyo.
4
Mhandisi Mkuu Msanifu Albert Wikedzi akiwaonesha waandishi wa Habari (Hawapo pichani) aina mbalimbali za sanifu zinazofanyika katika shirika hilo, wakati wa ziara ya waandishi wa habari katika kiwanda hicho Mjini kibaha.
5
Mhandisi Mkuu wa Karakana kutoka Shirika la NYUMBU (Tanzania Automative Technology Centre) Ayoub Mnzava akiwaonesha waandishi wa habari trekta ndogo (Power Tiller) iliyotengenezwa kwa lengo la kuongeza uwezo wa wazalishaji wa mazao ya kilimo kote nchini.
6
Mkuu wa Kitengo cha Usubiaji Mhandisi Anderson Ole Zakaria akiwaeleza waandishi wa habari namna kitengo hicho kinavyofanya kazi ili kukidhi mahitaji ya kiwanda ambapo alisema kitengo hicho kinayeyusha hadi tani 2.5 za chuma zinazotumika kutengeneza bidhaa mbalimbali zinazotoka katika shirika hilo.
7
Mkurugenzi Mkuu wa Shirika la NYUMBU (Tanzania Automative Technology Centre) Brigedia Jenerali Anselim akiwaonesha waandishi wa habari moja aina ya gari la kivita lililotengezezwa na shirika hilo.
8
Mkurugenzi Mkuu wa Shirika la NYUMBU (Tanzania Automative Technology Centre) Brigedia Jenerali Anselim (katikati) akiwa katika picha ya pamoja na waandishi wa habari waliokuwa katika ziara hiyo,kulia ni Mkuu wa Kitengo cha Mawasiliano Serikalini wa Wizara ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa Luteni Kanali Juma Nkangaa Sipe na kushoto ni mwandishi mwandamizi wa Channel Ten.
PICHA NA HASSAN SILAYO-MAELEZO
…………………………………………………………………………………
Na Frank mvungi-MAELEZO
Serikali kupitia shirika la Nyumbu imebuni na kuunda trekta ndogo (Power Tiller) kwa lengo la kuongeza uwezo wa wazalishaji wa mazao ya kilimo kote nchini.
Hayo yamesemwa na Mkurugenzi Mkuu wa Shirika la NYUMBU (Tanzania Automative Technology Centre) Brigedia Jenerali Anselim Bahati wakati wa ziara ya waandishi wa habari iliyolenga kuona jinsi shirika hilo linavyochangia katika kukuza uchumi wa Taifa tangu kuanzishwa kwake.
Akifafanunua kuhusu mafanikio ya shirika hilo Brigedia Jenerali Bahati amesema limekuwa likitekeleza miradi mbalimbali kama vile utengenezaji wa matrekta madogo( power Tiller) ambayo yanalenga kumkomboa mkulima hapa nchini kwa kuondokana na matumizi ya jembe la makono.
Akizungumzia moja ya sifa za matrekta hayo amesema kuwa yana uwezo wa kulima hekta nne kwa siku na yameundwa kwa kuzingatia mahitaji ya wananchi na dhamira ya Serikali yakumkomboa mkulima ili aweze kuchangia kikamilifu katika kukuza uchumi.
Miradi mingine ni mradi wa gari la zimamoto (RIV) ambapo ubunifu na uzalishaji wa magari ya zimamoto ambayo baadhi yanatumika hapa nchini kutoa huduma ya kudhibiti majanga ya moto ambapo kupia mafanikio ya mradi huo unaendelezwa ili kuzalisha magari yatakayotumiwa kwenye halmashauri za Wilaya na Miji kote nchini ambapo mradi huo unategemea ufadhili wa Serikali.
Lengo la mradi huo ni kubuni na kuzalisha magari ya zimamoto ya gharama nafuu ili kuongeza uwezo wa halmashauri zote nchini katika kukabiliana na majanga ya moto.
Shirika hilo pia limeendelea na kazi ya utafiti na ubunifu wa magari ya aina mbalimbali kama vile yakubeba mizigo,kusomba maji,kubeba mchanga na vifaa vya aina hiyo lengo likiwa ni kujenga misingi ya kuwaletea wananchi maendeleo endelevu katika nyanya mbalimbali.
Katika utunzaji wa mazingira shirika hilo limefanikiwa kubuni matela maalum yanayoweza kuvutwa na gari au trekta katika uondoshaji taka kwenye halmshauri za miji na yanaweza kubeba taka tani tano kwa mara moja hivyo kusaidia katika utunzaji wa mazingira.
Akizungumzia malengo ya shirika hilo Brigedia jenerali Bahati amesema ni kuwa kituo cha teknolojia endelevu,chenye utawala na uongozi bora,kuwa kituo kinachotegemewa katika utafiti na uvumbuzi wa kihandisi nchini,kusambaza teknolojia mbalimbali nchini kwa kuzalisha kwa wingi na kutoa huduma za uhakiki ubora kwa uhakika zaidi.
Naye Msemaji wa Wizara ya Ulinzi na Jeshi la kujenga Taifa Luteni Kanali Juma Nkangaa Sipe alitoa wito kwa watanzania kutumia zana zinazozalishwa na shirika hilo zikiwemo mashine za kuzalisha matofali,pampu za kusukuma maji kwa ajili ya kilimo cha umwagiliaji,mashine za kuchakata mazao kama korosho ili kuongeza thamani ,mashine za kuzalisha matofali na vipuri vya aina mbalimbali vinavyozalishwa kulingana na mahitaji ya mteja.
Shirika la nyumbu (Tanzania automotive Technology Centre) lilianzishwa Desemba 1985 lengo kuu likiwa kuwa kituo maalum cha kufanyia utafiti na kuendeleza uvumbuzi na ubunifu wa teknolojia mbalimbali ili kuongeza uwezo wa taifa kujiletea maendeleo endelevu katika nyanja zote kwa kuinua uchumi wa wananchi na Taifa kwa ujumla.

No comments: