Thursday, August 20, 2015

NEC YAWAOMBA VIONGOZI WA DINI KUTOKUWA NA UPANDE WAKATI WA KUWAELIMISHA WANANCHI KUHUSU UCHAGUZI MKUU UJAO.

tu1
Mwenyekiti wa Tume ya Taifa ya Uchaguzi Jaji, Damian Lubuva akitoa mada jana jijini Dar es salaam kwa viongozi wa madhehebu mbalimbali waliohudhuria mkutanoni .
tu2
Baadhi ya viongozi wa dini waliohudhuria mkutano ulioandaliwa na NEC jana jijini Dar es salaam wakifuatilia mada iliyokuwa zikiendelea.
tu3
Wanasekretarieti ya maandalizi ya mkutano NEC na wadau mbalimbali  na baadhi ya waandishi wakifuatilia mjadala kuhusu wajibu wa viongozi wa dini kuelekea uchaguzi mkuu ujao.
tu4
Mwenyekiti wa Tume ya Taifa ya uchaguzi Jaji, Damian Lubuva akiteta jambo na mmoja  wa makamishna wa Tume hiyo Prof Amon Chaligha jana jijini Dar es salaam wakati wa mkutano wa NEC na wadau mbalimbali.
tu5
Mkurugenzi wa Tume ya Taifa ya Uchaguzi Bw. Kailima Ramadhani akitoa mada kuhusu mchakato mzima wa uchaguzi na hatua zilizofikiwa hadi sasa jana jijini Dar es salaam wakati wa mkutano wa viongozi wa madhehebu ya dini.
………………………………………………………………………..
Tume ya Taifa ya uchaguzi  NEC  imewaomba viongozi wa dini zote kutumia majukwaa yao kuwaelimisha wapiga kura bila kuonyesha hisia za kuegemea upande wowote wa mgombea  ili waweze kufanya maamuzi sahihi wakati wa uchaguzi Mkuuu ujao.
Kauli hiyo imetolewa na Mwenyekiti   wa NEC, Jaji Damian Lubuva kwenye Mkutano uliofanyika leo jijini Dar es Salaam uliowakutanisha wadau hao wa uchaguzi na kuwakumbusha wajibu wao katika jamii hususani katika kipindi hiki ambacho nchi inaelekea katika uchaguzi mkuu.
Alisema kuwa  taasisi za kidini zinaaswa kama walivyo wadau wengine katika kipindi hiki cha uchaguzi kuhubiri amani na kuendelea kutoa elimu kwa watanzania ili zoezi hili liishe kwa amani na kuwaacha watanzania wakiwa na umoja na mshikamano licha ya tofauti za kiimani zilizopo miongoni mwao.
“Tume inawataka, nyinyi  viongozi wa dini, mnapotoa mafundisho ya uchaguzi kwa waumini wenu kuhakikisha hamuonyeshi hisia za kuwa upande wa chama chochote cha kisiasa na zaidi kuepuka kushawishi waumini wenu kuegema chama au mgombea fulani” amesema Jaji Lubuva.
Mmoja wa washiriki wa mkutano huo , Askofu Philemon Phiri wa kanisa la EAGT-Mikocheni -A ameiasa Tume hiyo  kusimama katika haki, uhuru na kuhakikisha wanatangaza washindi bila kuonyesha upendeleo  ili kuivusha nchi ikiwa  salama.
Mshiriki mwingine kutoka Kanisa la Moravian Mchungaji Alamu Kajuna alisema kuwa amani ndiyo tunu kwa kila mwanadamu, hatutegemei vurugu wakati  huu wa uchaguzi maana amani inapotoweka wanaoumia ni wananchi wakiwamo waumini wao hivyo wao kama taasisi zinazoshirikiana na wananchi kwa karibu kuhakikisha wanatoa elimu kwa wananchi ili tupate viongozi kwa amani
Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC) imekutano na viongozi hao na wadau wengine ikiwa zimebaki siku mbili kuanza kwa kampeni hapo Jumamosi ijayo kwa ajili ya maandalizi ya uchaguzi mkuu ujao.

No comments: