Wednesday, October 07, 2015

RAIS KIKWETE AWEKA JIWE LA MSINGI MRADI WA JENGO LA MAKAZI NA BIASHARA NHC MOROCCO SQUARE

Rais Jakaya Mrisho Kikwete akiwaeka jiwe la msingi la mradi mkubwa wa jengo la makazi na biashara la Morocco Square ambao ni mkubwa kwa eneo hili la Afrika Mashariki ambao umejengwa katika msingi mmoja. Wanaoshuhudia nia Mkurugenzi Mkuu wa Shirika la Nyumba la Taifa, Nehemia Kyando Mchechu, Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, William Vangimembe Lukuvi na Mkurugenzi Mkuu wa Benki ya CRDB PLC LTD, Dk Charles Kimei. 

Mradi huu una  uwezo wa kubeba watu 6000 na kutoa ajira ya zipatazo 24,750.  Mradi huu una majengo manne tofauti, ikiwemo ya ghorofa 22 kwa ajili ya nyumba 100 za makazi za vyumba vitatu na vinne, ghorofa 20 na 17 kwa ajili ya Ofisi na maduka makubwa  na  ghorofa 13 kwa ajili ya Hoteli  yenye vyumba vya kulala 81. Mradi huu una eneo maalum la kutua helkopta na eneo kubwa kwa ajili ya maegesho ya magari.

Jengo la NHC Morocco Square litakavyokuwa mara baada ya kukamilika.
Rais Jakaya Mrisho Kikwete akipata maelezo ya mradi wa Morocco Square kutoka kwa Mkurugenzi wa Ubunifu wa NHC, Issack Peter 
Rais Jakaya Mrisho Kikwete akipata maelezo ya mradi wa Morocco Square kutoka kwa Mkurugenzi wa Ubunifu wa NHC, Issack Peter 
 Baadhi ya wafanyakazi wa NHC na wageni waalikwa waliokuwapo katika shughuli hiyo.
  Baadhi ya wafanyakazi wa NHC na wageni waalikwa waliokuwapo katika shughuli hiyo.
  Baadhi ya wafanyakazi wa NHC na wageni waalikwa waliokuwapo katika shughuli hiyo.
 Mkuu wa Kitengo cha Mawasiliano kwa Umma na Huduma kwa Jamii Susan Omari akisalimiana na Mwenyekiti wa Bodi ya NHC, Zakhia Meghji wakati akiingia katika eneo la tukio.

  Rais Kikwete akiwasili katika eneo lililowekwa jiwe la msingi la Morocco Square.
 Rais Kikwete akisalimiana na wafanyakazi wa NHC wakati akiwasili eneo la tukio.
  Rais Kikwete akisalimiana na wafanyakazi wa NHC wakati akiwasili eneo la tukio.
  Rais Kikwete akifuatiliahotuba ya Mkurugenzi Mkuu wa NHC hayupo pichani wakati akiwasili eneo la tukio.

 Mkurugenzi Mkuu wa Shirika la Nyumba la Taifa, Nehemia Kyando Mchechu akisoma hotuba yake kwa Rais Kikwete.
  Mkurugenzi Mkuu wa Shirika la Nyumba la Taifa, Nehemia Kyando Mchechu akisoma hotuba yake kwa Rais Kikwete.
 Msondo Ngoma Music Band walikuwapo eneo la tukio wakitoa burudani
 Rais Kikwete akihotubia kabla ya kuweka jiwe la msingi la mradi wa NHC Morocco Square.

Wakuu wa Taasisi mbalimbali ambao walialikwa katika shughuli hiyo ya uwekaji wa jiwe la msingi

 Rais Kikwete na Baadhi ya Watendaji wakuu wa Menejimenti ya NHC.
 akiondoka eneo la Mradi
 Baadhi ya wafanyakazi wa NHC na wageni waalikwa waliokuwapo katika shughuli hiyo.

HOTUBA YA MKURUGENZI MKUU WA NHC, BW. NEHEMIA KYANDO MCHECHU, KUMKARIBISHA RAIS WA JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA, MHE. DK JAKAYA MRISHO KIKWETE, KUWEKA JIWE LA MSINGI KWENYE JENGO LA BIASHARA NA MAKAZI LA NHC MOROCCO SQUARE, DAR ES SALAAM, TAREHE 7 OKTOBA 2015
Mheshimiwa Jakaya Mrisho Kikwete, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania;
Mheshimiwa William Vangimembe Lukuvi, (Mb.), Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi;
Mheshimiwa Angela Kairuki; (Mb.), Naibu Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi;
Mheshimiwa, Said Meck Sadick, Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam ;
Mheshimiwa Paul Makonda, Mkuu wa Wilaya ya Kinondoni;
Ndugu Viongozi wa Serikali mlioko hapa,
Menejimenti na viongozi wa NHC mliopo hapa,
Wanahabari,
Ndugu Wageni Waalikwa,
Mabibi na Mabwana.
Awali ya yote,  Mheshimiwa Rais, napenda kutoa  shukrani  zangu za dhati kwako kwa kuweza kutenga muda wako na hasa katika kipindi hiki ambapo una majukumu mazito ya kitaifa na kuja kujumuika nasi hapa hii leo, Tumehemewa sana!.
Aidha, nichukue fursa hii kuwashukuru wote waliojumuika nawe hapa kwani sherehe ni watu na watu ni hawa wote waliofika hapa. Napenda kuwakaribisha watu wote katika siku ya leo ambayo ni muhimu sana kwetu hasa tunapoendeleza safari yetu ya ujenzi wa nyumba kwa ajili ya Watanzania hapa Morocco. Kwa niaba ya Menejimenti na Wafanyakazi wote wa Shirika nawashukuru sana kwa kushirikiana nasi katika uwekaji wa jiwe la msingi.
Mheshimiwa Rais, kwa mara nyingine, kwa niaba ya Menejimenti na Wafanyakazi wote wa Shirika, naomba nikushukuru sana kwa kukubali tena kuliweka Shirika letu kwenye ratiba yako na kuja kutuwekea jiwe la msingi katika mradi wetu wa nyumba za Biashara na Makazi za Morocco Square. Sote tunaelewa kuwa hivi karibuni uliweza kutufungulia jengo la biashara na Ofisi pale Lumumba Kigoma  na nyumba za gharama nafuu pale Mlole Kigoma. Ninafahamu kuwa unafanya hivyo kwa dhamira yako ya dhati ya kusukuma mbele ajenda ya kuwapatia wananchi nyumba bora. Msukumo wako katika sekta ya nyumba  tangu uchaguliwe kuwa Rais na sasa unakaribia kustaafu umetutia moyo sana na tumefarijika kuwa na Rais wa aina yako mwenye mtazamo chanya wa kukuza sekta ya nyumba.
Mheshimiwa Rais, ujenzi wa nyumba hizi umewapatia wananchi makazi bora, kupendezesha mandhari za miji yetu, kuongeza wigo wa kodi ya majengo na kodi ya ardhi, kuondoa makazi hafifu katika maeneo husika na kutoa ajira za moja kwa moja kwa wananchi.
Mheshimiwa Rais, mradi huu unaouwekea jiwe la msingi leo, ulianza Juni 2014 na unatarajiwa kukamilika mwanzoni mwa mwaka 2017. Mkandarasi  anayetekeleza ujenzi wa mradi huu mkubwa na wa aina yake ni Kampuni ya Kitanzania ya Estim Construction Ltd ya Dar es Salaam ambayo ni Mkandarasi Daraja la Kwanza aliyepatikana kwa kushindanishwa kimataifa. Hadi kukamilika ujenzi wa majengo yote manne ya mradi huu utagharimu kiasi cha shilingi billion 150 ambazo ni mkopo kutoka benki ya CRDB PLC. Mradi huu ambao ni mkubwa kuliko yote Afrika Mashariki una mita za mraba 110,000 zilizo katika msingi mmoja.  Kati ya mita hizo, 47,793 ni kwa ajili ya Ofisi, 24,924 ni kwa ajili ya makazi na mita za mraba 28, 827 ni kwa ajili ya biashara wakati kumbi za mikutano, maduka makubwa, sehemu za kuchezea watoto na maduka ya vyakula na hoteli ikiwa na ukubwa wa mita za mraba 8,456. Mradi huu una  uwezo wa kubeba watu 6000 na kutoa ajira ya zipatazo 24,750.  Mradi huu una majengo manne tofauti, ikiwemo ya ghorofa 22 kwa ajili ya nyumba 100 za makazi za vyumba vitatu na vinne, ghorofa 20 na 17 kwa ajili ya Ofisi na maduka makubwa  na  ghorofa 13 kwa ajili ya Hoteli  yenye vyumba vya kulala 81. Mradi huu una eneo maalum la kutua helkopta na eneo kubwa kwa ajili ya maegesho ya magari. Kwa ujumla mradi huu ukikamilika utaifanya nchi yetu kuwa na majengo yanayofanana na miji mingine mashuhuri duniani kama Dubai na Manhattan na kuwa kivutio kikubwa kwa  wageni mbalimbali kutoka nje ya nchi.  Hivyo ni jambo la faraja na la kujivunia kwa wewe Mheshimiwa Rais kuja kuweka jiwe la msingi ili kuacha alama muhimu ya ushiriki wako katika sekta ya nyumba nchini.
Mheshimiwa Rais, kutokana na eneo hili kuwa na ardhi yenye thamani kubwa, tayari wameshajitokeza wanunuzi wa baadhi ya Ofisi. Soko la Hisa la Dar es Salaam wameshanunua mita za mraba 900 za sehemu ya ofisi katika jengo hilo ili kupanua huduma zake. Kutokana na umuhimu wa Soko la Hisa katika ukuaji wa uchumi wa Taifa, jengo lenye Ofisi walizonunua litaitwa Exchange Tower na hivyo kuipa heshima nchi yetu. Mashirika mengine makubwa ya kitaifa na kimataifa yameshawasilisha maombi ya kununua ofisi katika mradi huu ikiwemo Kampuni ya Delloitte.
Mheshimiwa Rais, bei za uuzaji wa eneo la makazi zitakuwa Dolla za Kimarekani 1450 kwa mita ya mraba kwa wateja wa mwanzo na Dolla za Kimarekani 1600 kwa mita ya mraba kwa wateja watakaokuja baada ya muda wa punguzo kuisha. Eneo la Ofisi katika mradi huu litauzwa kwa kwa wastani wa dola za kimarekani 2,300 kwa mita moja ya mraba. Aidha, eneo la hoteli litauzwa au kupangishwa kwa kampuni au mtu yeyote mwenye uwezo wa kuendesha hoteli kwa viwango vya kimataifa. Ni vizuri nikaweka wazi Mheshimiwa Rais kuwa mradi huu umelenga watu wa kipato cha kati na juu tu kama ilivyo miradi mingine inayolenga wananchi wa kada ya chini.
Mheshimiwa Rais, jengo hili limebuniwa likiwa na mahitaji muhimu yakiwa sehemu moja, na ili kuwarahisishia wananchi wengi kufika katika majengo haya, Shirika litazungumza na Mamlaka ya Usafiri wa haraka Jijini Dar es Salaam(DRAT) kufikisha miundombinu ya usafiri wa haraka katika majengo haya.
Mheshimiwa Rais, mradi huu ni utekelezaji wa maagizo yako uliyoyatoa mwaka 2006 ulipotembelea Wizara ya Ardhi kwa mara ya kwanza mara ulipochaguliwa kuwa Rais wa Taifa letu. Katika ziara hiyo uliagiza NHC kutumia fursa ya kuwa wamiliki wa majengo mengi katikati ya miji yetu, kubadili sura za miji hiyo hadi kufikia miji kama Manhattan. Ujenzi wa majengo haya kwa hakika unatarajiwa kuboresha mazingira ya biashara katika Jiji la Dar Es Salaam. Jengo la Morocco Square lipo karibu kabisa na kitovu cha Jiji likiwa limezungukwa na maofisi na makazi muhimu kabisa. Eneo la Morocco Square linatoa fursa kwa mkazi kuweza kufika kwa karibu kabisa sehemu mbalimbali muhimu za Jiji la Dar Es Salaam kama vile Mikocheni, Oystebay, Masaki, katikati ya Jiji la Dar Es Salaam, Kinondoni, Kawe na Mlimani City.
Mheshimiwa Rais, Jengo hili litawekewa miundombinu imara ya zimamoto, mfumo wa vipoza joto, kebo za mtandao wa mawasiliano, lifti, ulinzi wa saa 24 wa kamera za CCTV na kisima kirefu cha maji chenye mfumo wa kusukuma maji ya kutosha kwa wakazi, Hoteli  na maofisi yatakayokuwa hapa.
Mheshimiwa Rais, kabla sijamaliza maelezo yangu, nichukue fursa hii kuwahamasisha wananchi wanaohitaji sehemu kwa ajili ya ofisi, biashara na nyumba za kuishi wafanye wajitokeze kwa wingi kununua na hivyo kuwa wamiliki wa nyumba hizi ili kukuza uchumi na ustawi wa maisha yao.
Mheshimiwa Rais, nisingependa kuchukua muda mwingi kwa hotuba ndefu. Nirudie kukushukuru kwa dhati kuja kutuwekea jiwe la msingi katika mradi huu.

Mheshimiwa Rais, baada ya kusema hayo, sasa nimkaribishe Mheshimiwa Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, ili akukaribishe uwasalimie wananchi na kutuwekea jiwe la msingi. Ahsanteni sana kwa kunisikiliza.

No comments: