Friday, March 27, 2015

KATIBU MKUU- UTUMISHI BW. GEORGE D. YAMBESI ASTAAFU UTUMISHI WA UMMA

1
Katibu Mkuu Utumishi Bw.George D. Yambesi (kushoto) akikabidhi ofisi kwa Naibu Katibu Mkuu Utumishi Bw.HAB Mkwizu baada ya kustaafu Utumishi wa Umma.Makabidhiano hayo yamefanyika ofisini kwake.
2
Katibu Mkuu -Utumishi Bw. George D. Yambesi (katikati) akipongezwa na Mkurugenzi wa Idara ya Utawala na Rasilimali Watu Bw. Aloyce Msigwa, (kushoto) ni Naibu Katibu Mkuu-Utumishi Bw. HAb Mkwizu. Bw. Yambesi amestaafu Utumishi wa Umma.
………………………………………………………………………………..
Katibu Mkuu, Ofisi ya Rais- Menejimenti ya Utumishi wa Umma Bw. George D. Yambesi amestaafu Utumishi wa Umma. 
Akiongea katika hafla fupi ya makabidhiano ya Ofisi Bw. Yambesi amewashukuru Wakurugenzi na Watumishi wa Ofisi ya Rais-Menejimenti ya Utumishi wa Umma kwa ushirikiano katika kutekeleza majukumu na kufikia mafanikio na malengo yaliyopangwa.
“Nimefurahi kufanya kazi na kila mmoja wenu katika kipindi chote hata pale rasilimali zilipokua chache kila mmoja wenu alijitahidi kufikia lengo la kuwahudumia wadau wetu” Bw. Yambesi alisema na kuongeza jambo la msingi ni kuhakikisha Watumishi wanaendelea kujengewa uwezo ili ubora wa kazi na huduma uendelee kuwa wa kiwango stahili.
Katibu Mkuu Bw. Yambesi aliainisha kuwa amekua Mtumishi wa Umma kwa muda wa miaka 38 na kwa hilo anamshukuru Mungu kwa kumwezesha kutekeleza majukumu mbalimbali kwa muda wote aliotumikia Umma.
Wakati huohuo, Naibu Katibu Mkuu-Utumishi Bw. HAB Mkwizu alimpongeza Bw. Yambesi kwa utendaji wake mzuri. “Unastaafu lakini umejenga uwezo kwa wanaobaki ofisini hivyo kiwango cha huduma zinazotolewa na ofisi na ushirikiano tutaendeleza” Bw. Mkwizu alisema.
MWISHO.

No comments: