Monday, March 23, 2015

DKT. BILAL AFUNGA MAADHIMISHO YA WIKI YA MAJI KITAIFA MJINI MUSOMA.

1
Makamu wa Rais wa Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Mohamed Gharib Bilal akishuka kwenye ndege baada ya kuwasili kwenye uwanja wa ndege wa Musoma
2
 Makamu wa Rais wa Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Mohamed Gharib Bilal, akiambatana na wenyeji wake baada ya kuwasili mjini Musoma.
3
 Makamu wa Rais, Dkt. Bilal, akisalimiana na Katibu Mkuu wa CCM mkoa wa Mara Adam Ngalawa baada ya kuwasili mjini Musoma.
4
 Makamu wa Rais, Dkt. Bilal, akisikiliza wimbo wa Tanzania uliokuwa unaimbwa na wanafunzi wa Shule ya Sekondari Kisangula.
5
 Mkurugenzi Mtendaji ya Mamlaka ya Majisafi na Usafi wa Mazingira Musoma, (MUWASA) Mhandisi Said Gantala, akimuonesha Makamu wa Rais, Dkt. Bilal (katikati), ramani ya Mradi wa Ujenzi wa Uboreshaji wa Hudumu ya Majisafi na Usafi wa Mazingira Mjini Musoma. Kushoto ni Waziri wa Maji, Prof. Jumanne Maghembe.
6
Waziri wa Maji, Prof. Jumanne Maghembe, akimkaribisha Makamu wa Rais, Dkt. Bilal kuzungumza na wananchi kwenye eneo la mradi.
7
 Makamu wa Rais, Dkt. Bilal, akizungumza na wananchi.Kulia ni Mkuu wa Mkoa wa Mara Kapteni Mstaafu Aseri Msangi na kushoto ni Waziri wa Maji, Prof. Maghembe.
8
 Makamu wa Rais, Dkt. Bilal (katikati) akikata utepe wa Mradi wa Ujenzi wa Uboreshaji wa Hudumu ya Majisafi na Usafi wa Mazingira Mjini Musoma.Kushoto kwake ni Balozi wa Ufaransa nchini, Melika Berak na viongozi wengine wa chama.
9
 Makamu wa Rais, Dkt. Bilal akiweka jiwe la Msingi la Mradi wa Ujenzi wa Uboreshaji wa Hudumu ya Majisafi na Usafi wa Mazingira Mjini Musoma.Kushoto ni Waziri wa Maji, Prof. Jumanne Maghembe na katikati ni Balozi wa Ufaransa nchini Melika Berak.
10
 Mkurugenzi wa Idara ya Ubora wa Maji, Nadhifa Kemikimba akimuonesha Makamu wa Rais, Dkt. Bilal teknolojia ya kusafisha maji kwa kutumia mifupa.
11
 Baadhi ya washiriki wa maonesho ya Wiki ya Maji Kitaifa
12
 Katibu Mkuu wa Wizara ya Maji, Mhandisi Mbogo Futakamba akizungumza na wananchi juu ya maadhimisho.
13
 Makamu wa Rais, Dkt. Bilal akimpa kikombe Mkuu wa Idara ya Rasilimali za Maji na Uhandisi wa Umwagiliaji wa Chuo cha Maji, Eng. Pantaleo Tumbo ikiwa ni moja ya zawadi zilizotolewa kwa washiriki wa maonesho ya maadhimisho ya wiki ya Maji.
……………………………………………………………………..
Hussein Makame-MAELEZO, Musoma
MAKAMU wa Rais wa Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Mohgamed Ghalib Bilal amesema kuwa kila ahadi ya Serikali iliyotolewa itatimizwa ili kuhakikisha kuwa inaacha kazi nyepesi kwa viongozi watakaokuja katika kuendeleza maendeleo ya Tanzania.
Dkt. Bilal aliyasema hayo kwenye kilele cha Maadhimisho ya Wiki ya Maji Duniani ambayo kitaifa yamefanyika mkoani Mara yakiwa na Kaulimbiu isemayo “Maji kwa Mandeleo Endelevu.
Katika kilele cha Maadhimisho hayo, Dkt. Bilal aliweka jiwe la Msingi kwenye Mradi wa Ujenzi wa Uboreshaji wa Hudumu ya Majisafi na Usafi wa Mazingira Mjini Musoma ambao utagharimu Shilingi Bilioni 44 hadi kukamilika kwake.
“Tumewaahidi kupata maji na hilo tutatekeleza.Kila ahadi ya Serikali itatimizwa swali ni muda na wakati lakini kwa kweli hatukusudii kuwaacha njiani, mambo tuliyosema tutayafanya ili tuwaachie watakaokuja kazi nyepesi ya kuendeleza maendeleo ya nchi yetu” alisema Dkt. Bilal.
Mradi huo mkubwa wa maji unatarajiwa kukamilika mwezi Aprili, 2015 ambapo Dkt. Bilal alisema mradi huo utakapokamilika itaipatia Manispaa ya Musoma maji ya uhakika kwa asilimia 100.
Aliongeza kuwa mafanikio ya mradi huo pia ni kuongezeka kwa uzalishaji wa maji kutoka mita za ujazo 10,000 za sasa kwa siku, hadi mita za ujazo 36,000 kwa siku.
Dkt. Bilal alitoa rai kwa wananchi wa Manispaa ya Musoma na mkoa wa Mara kutunza mradi huo na miradi yote inayoendelea kutekelezwa ili iendelee kuwasaidia wananchi na vizazi vijavyo.
“Na juu ya haya yote, ni msisitizo katika utunzaji endelevu wa mazingira yetu ili yaendelee kutuhifadhi. Aidha, teknolojia za uvunaji wa maji ya mvua na ujenzi wa mabwawa ni maeneo ambayo yatatuhakikishia kwamba tunakuwa na huduma endelevu ya rasilimali ya maji” alisema.
Alisema Tanzania haina budi kuwa na mikakati ya makusudi kukabiliana na changamoto hizo, jambo ambalo Serikali imeanza kulifanyia kazi.
Alifafanua kuwa uhaba wa maji na kutopatikana kwake kwa uhakika kunaleta athari mbaya katika shughuli zote za kiuchumi.
“Majanga yanayohusiana na maji kama vile, mafuriko na ukame kwa kiwango kikubwa ni maafa yanayojitokeza mara nyingi katika sehemu mbalimbali duniani hivi sasa” alisema Dkt. Bilal na kupngeza kuwa:
“Vifo, uharibifu wa mali, makazi na miundombinu vina athari kubwa kwa maendeleo ya mtu mmoja mmoja, kikundi, jamii na hata Taifa”
Hivyo, alitoa wito kwa wadau wote kuunganisha nguvu pamoja katika kukabiliana na athari mbaya za mabadiliko ya hali ya hewa kwani, mabadiliko hayo yana athari kuanzia kwenye kupungua kwa misitu na vyanzo vya maji.
Alitaja athari nyingine kuwa ni kupungua kwa rasilimali za maji juu na chini ya ardhi; kuathirika kwa ubora wa maji ya kunywa; hadi kukua kwa utoaji wa gesi ya ukaa.
Hata hivyo alisema, Serikali ya Tanzania itaendeleza juhudi za kuhakikisha inawafikishia wananchi maji safi na salama katika maeneo ya nchi ambayo yamekosa huduma hiyo.
Aliwakumbusha wananchi kuwa wana jukumu kubwa la kutunza vyanzo vya maji popote pale vinapopatikana na kwamba wana kubwa kwenu wananchi ni kutoa mchango unaostahili katika usimamizi na uendelezaji wa rasilimali za maji.
Akimkaribisha Dkt. Bilal, Waziri wa Maji, Prof. Jumanne Maghembe alisema wizara yake itajitahidi na kufanya kila linalowezekana ili katika kipindi kisichozidi miezi mitatu maji yatoke mjini Musoma na wananchi wafurahie huduma hiyo.
Alisema katika kipindi cha Maadhimisho ya Wiki ya Maji, viongozi mbalimbali walishiriki katika kukagua miradi ya maji na kutembelea wilaya zote za Mara na kuweka mawe ya msingi na kuzindua miradi ya maji ambayo imekamilika.
Kwa upande wake, Mkurugenzi Mtendaji ya Mamlaka ya Majisafi na Usafi wa Mazingira Musoma, (MUWASA) Mhandisi Said Gantala alisema mradi huo unajengwa na Serikali ya Tanzania kwa kushirikiana na Serikali ya Ufaransa kupitia Shirika la Maendeleo la Ufaransa (AFD).
Alisema mradi huo unajumuisha ujenzi wa chanzo kipya cha maji, chujio, mtambo wa kisasa wa kutibu maji na ujenzi wa matenki mapya mawili yenye mita za ujazo 5,500.
Aliongeza pia kuwa, ujenzi huo utajumuisha ujenzi wa mfumo mpya wa mabomba ya usambazaji maji na ujezni wa miundombinu mingine.
“Mheshimiwa mgeni Rasmi Serikali ya Ufaransa kupitia Shirika lake la AFD kwa kushirikiana na Benki ya Uwekezaji ya Jumuiya ya Ulaya (EAD) wamekubali kufadhili mradi wa kuondoa majitaka katika manispaa ya Musoma” alisema Mhandisi Gantala.
Naye Balozi wa Ufaransa nchini Melika Berak alisema kuwa amefurahishwa na ushirikiano anaoupata kutoka Serikali ya Tanzania katika kuhakikisha wanapunguza tatizo la maji nchini.
Katika kilele cha maadhimisho hayo ya 27 ya Wiki ya Maji Duniani, washiriki wa maonesho katika maadhimisho hayo walipewa vyeti vya kushiriki na zawadi za vikombe kutokana na makundi washiriki.

No comments: