Monday, August 18, 2014

SERIKALI YASHAURIWA KUTUNGA SERA YA KUDHIBITI POMBE

DSC_0279
Banda la Mtandao wa mashirika yapatayo 30 ya kupambana na matumizi ya kupita kiasi ya pombe nchini (Tanzania Network Against Alcohol Abuse) kwenye maadhimisho ya siku ya kimataifa ya vijana duniani.(Picha na Zainul Mzige wa MOblog).
Na Mwandishi Wetu
SERIKALI imeshauriwa kutunga sera madhubuti ya udhibiti wa pombe katika jamii ili pamoja na mambo mengine kuhakikisha vijana wanalindwa dhidi ya bidhaa hiyo kwenye soko.
Akizungumza na Moblog Tanzania jijini Dar es Salaam katika viwanja vya chuo kikuu wakati wa maadhimisho ya siku ya kimataifa ya vijana, Msemaji wa Mtandao wa kupambana matumizi ya pombe kupita kiasi (Tanzania Network Against Alcohol Abuse) Bw, Mathias Kimiro amesema kwamba kuna umuhimu wa serikali kutunga sera mpya ya pombe ili kuzuia madhara kwa vijana na taifa kwa ujumla.
“Kwa kawaida matumizi ya pombe kupita kiasi ina madhara makubwa katika afya ya mtumiaji lakini vile vile ina madhara kwenye familia kupitia kaya moja moja na kusababisha mateso kwa familia hasa watoto,” amesema Bw Kimiro
Amesema kwamba umuhimu wa kuwa na sera madhubuti ya kudhibiti pombe katika jamii ni kuangalia upya ni kwa kiwango ngani matangazo ya pombe yanavyohamasisha unywaji kupita kiasi kwenye jamii.
Bw Kimiro aliongeza kwamba mashirika yasiyo ya kiserikali yataendelea kuwakumbusha mamlaka zinazohusika umuhimu wa kuwa na sera ya kudhibiti pombe katika jamii pamoja na kuangalia madhara ya matangazo kwa wasomaji wa mabango.
DSC_0300
Mkurugenzi Mtendaji wa Makangarale Youth Theatre, ambao ni taasisi chini ya Tanzania Network Against Alcohol Abuse (TAAnet), Bw. Ismael Mnikite akifafanua jambo kwa Mgeni Rasmi kutoka Wizara ya Habari, Utamaduni, Vijana na Michezo, Bibi Venerose Mtenga wakati wa maadhimisho hayo.
Aliongeza kwamba sera ya pombe ni muhimu katika kuwabana makampuni ya vileo kupunguza uhamasishaji wa unywaji wa pombe kwa sababu ina madhara makubwa kwa vijana ambao ndio nguvu kazi ya taifa.
Bw Kimiro amesema kwamba sera ya udhibiti wa pombe ikifanikiwa nchini itapata fursa kupitia bunge kutunga sheria dhidi ya uuzaji na usambazaji holela wa pombe kwenye jamii ya kitanzania.
Amesema kwamba lengo la shirika lao ni kuhamasisha uwepo wa sera ya pombe nchini Tanzania kwa sababu hakuna sera mbali kuna sheria ndogo ndogo zilizowekwa katika jamii.
Bw Kimiro alifafanua kwamba hata sheria hizo ndogo ndogo siku hizi hazitekelezwi kama vile muda wa kuuza na kutokuuza pombe hauzingatiwi nah ii kupelekea upatikanaji wa pombe kiholela kwenye jamii.
Amesema kwamba ina madhara mengi kwa mfano kijamii unyanyasaji wa kijinsia hasa kwa wanawake na watoto na ndoa nyingi huvunjia na baadhi ya wanawake kubakwa na watoto kukosa mahitaji muhimu.
Bw Kimiro aliongeza kwamba madhara ya pombe kiuchumi ni makubwa kama vile kupunguza nguvu kazi ya taifa, matumizi mabaya ya fedha na kusababisha njaa kwenye jamii baada ya nafaka nyingi kutumiak kutengeneza pombe.
Shirika la Tanzania Network Against Alcohol Abuse ni mtandao wa mashirika yapatayo 30 ni ilianza kazi rasmi mwaka 2011 na ina matawi Dar es Salaam, Arusha, Kilimanjaro na Tanga.
DSC_0293
Mgeni rasmi akipata maelezo kutoka kwenye banda la Tanzania Network Against Alcohol Abuse kwenye moja la shirika lake la Tanzania Girl Guides Association, anayetoa maelezo ni Fadhia Khamis Ally na kushoto kwake ni Shadya Soud Milanzi wasichana hao wanatoka Girl Guides ambacho ni chama kisicho cha kiserikali na ni chama cha kujitolea, madhumuni yake ni kuwaendeleza wanawake pamoja na mtoto wa kike katika maswala ya kijamii na kiuchumi kwa kuwapa elimu na mafunzo.
DSC_0476
Msemaji wa Mtandao wa Kupambana na matumizi ya kupita kiasi ya pombe, Tanzania Network Against Alcohol Abuse, Mathias Kimiro akizungumza na Moblog Tanzania umuhimu wa serikali kuja na sera na baadaye sheria ya kudhibiti pombe nchini wakati wa maadhimisho ya siku ya kimataifa ya vijana duniani.
DSC_0477
Baadhi ya wafanyakazi kutoka mashirika mbalimbali chini ya Mtandao wa kupambana na matumizi ya pombe, Tanzania Network Against Alcohol Abuse wakiwa katika picha ya pamoja kwenye maadhimisho ya siku ya kimataifa ya vijana duniani yaliyofanyika katika viwanja vya Chuo Kikuu cha Dar es Salaam.

No comments: