Saturday, January 02, 2016

BALOZI SEIF ALI IDI: SHEREHE ZA MIAKA 52 YA MAPINDUZI YA ZANZIBAR ZIPO KAMA KAWAIDA

id01
Balozi Seif Ali Iddi akinukuu kifungu cha Katiba ya Zanzibar kinachomruhusu Dkt. Ali Muhamed Shein kuendelea kuiongoza Zanzibar mpaka atakapoapishwa Rais mwengine.
id1
Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Ali Iddi akizungumza na Waandishi wa Habari kuhusu  maadhimisho ya Sherehe za Mapinduzi ya Zanzibar ya mwaka 1964 kufikia miaka 52 Ofisini kwake Vuga Mjini Zanzibar.
id2
Baadhi ya Waandishi  wa habari waliohudhuria mkutano wa  Makamu wa Pili wa Rais w Zanzibar Balozi Seif Ali Iddi wakifuatiliia mkutano huo uliofanyika  Ofisini kwake Vuga Mjini Zanzibar.
……………………………………………………………………………………………….
Na Khadija Khamis – Maelezo  
Serikali ya Mapinduzi Zanzibar imesema kuwa Maadhimisho ya Shereha za Miaka 52 ya Mapinduzi ya Zanzibar yapo kama kawaida na yanatarajiwa kuanza  rasmi tarehe 3.12.2016  kwa kazi za usafi  wa mazingira katika maeneo mbali mbali  ya makaazi pamoja na sehemu za kutolea huduma za kijamii kama vile Hospitali Sokoni  na maeneo mengine.
Kauli hiyo imetolewa  na Makamo wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Ali Iddi  alipokuwa akizungumza na waandishi wa habari  Ofisini kwake Vuga Mjini Zanzibar.
Alisema ingawa zoezi  la usafi hufanyika kila tunapoanza maadhimisho ya  Sherehe za Mapinduzi  lakini kwa muda huu wananchi  wanapaswa kuchukuwa  juhudi maalum ili kuhakikisha kuwa maeneo yote yanakuwa safi   muda wote kwa vile  hivi sasa  nchi inakabiliwa  na tatizo kubwa la kuenea kwa maradhi ya kipindupindu.
“Zoezi la usafi  wa mazingira litakuwa la lazima na kutaandaliwa utaratibu maalum kwa kila Mamlaka za Mikoa ,Wilaya Baraza la Manispaa Mabaraza ya Miji na Halmashauri za wilaya kuratibu zoezi  la usafi na viongozi Wakuu  wa Kitaifa wataungana nasi katika katika maeneo watakayopangiwa, “Alisisistiza.
Amesema  mbali na usafi wa mazingira, katika maadhimisho ya mwaka huu kutakuwa na shughuli mbali mbali zikiwemo ujenzi wa Taifa ,uwekaji wa  mawe ya msingi  na ufunguzi wa miradi mbali mbali ya maendeleo pamoja na burudani na michezo na kilele cha maadhimisho hayo itakuwa siku ya Jumanne katika Kiwanja cha Amaani.
“Kama  kawaida kila ifikapo tarehe 12 Januari ya kila mwaka nchi yetu huadhimisha sherehe za Mapinduzi matukufu ya Zanzibar ya mwaka 1964,  kwa mwaka 2016 tutakuwa tunatimiza miaka 52 tangu viongozi na wazee wetu walivyokomboa nchi yetu,”  alisema Balozi  Seif Ali Iddi.
 Alikumbusha kuwa mafanikio na maendeleo  yaliyopatikana  Zanzibar  yanatokana   na imani na jitihada kubwa za viongozi ambao ni wanamapinduzi chini ya uongozi wa Marehemu Sheikh Abeid Amani Karume aliyeweka msingi imara wa mashirikiano .
Alisema siku ya kilele cha maadhimisho hayo  katika Uwanja wa Amaani  kutakuwa na Gwaride la  Vikosi  vya Ulinzina Usalama , Burudani ya Ngoma za Utamaduni  pamoja na Maandamano ya Wananchi wa Mikoa Mitano ya Zanzibar.
Makamo wa Pili  Balozi Seif Ali Iddi alisema kuwa sherehe hizo zitahudhuriwa na Viongozi mbali mbali  wa Serikali na vyama vya siasa kutoka Zanzibar na  Jamhuri ya Muungano wa Tanzania .
Amewataka  wananchi kujitokeza kwa wingi katika maadhimisho ya miaka 52 ya Mpinduzi ya Zanzibar na amewahakikishia  Serikali imejipanga kikamilifu kuona kunakuwa na hali ya utulivu na usalama mkubwa katika maeneo yote ya Zanzibar wakati  wa maadhimisho hayo.

No comments: