Saturday, January 16, 2016

TAARIFA YA UREJESHAJI WA FOMU ZA TAMKO LA RASILIMALI NA MADENI KWA VIONGOZI WA UMMA NA AHADI YA UADILIFU

JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA



OFISI YA RAIS, SEKRETARIETI YA MAADILI YA

VIONGOZI WA UMMA

   

        

 TAARIFA KWA UMMA

 

        Sekretarieti ya Maadili ya Viongozi wa Umma inawafahamisha Viongozi wa Umma wanaowajibika na Sheria ya Maadili ya Viongozi wa Umma Na. 13 ya Mwaka 1995 kwamba tarehe ya mwisho wa urejeshaji wa Fomu za Tamko la Rasilimali na Madeni ilikuwa ni tarehe 31 Desemba, 2015.



         Hadi kufikia   Disemba 31, 2015 jumla ya viongozi 11,428 tu wamerejesha matamko yao kwa Kamishna wa Maadili na Viongozi 3709 hawajatimiza wajibu huo wa kisheria na hivyo kukiuka Sheria ya Maadili ya Viongozi wa Umma Na. 13 ya Mwaka 1995 yanayowataka viongozi kurejesha fomu hizo katika muda uliowekwa kwa mujibu wa sheria na hivyo hatua za kisheria zitachukuliwa dhidi yao ikiwa ni pamoja na kuwafikisha mbele ya Baraza la Maadili, iwapo sababu za kuridhisha juu ya ukiukwaji huo wa sheria hazitatolewa kwa Kamishna wa Maadili.

        Serikali pia imeanzisha utaratibu wa kutia saini Fomu ya Ahadi ya Uadilifu kwa Viongozi wote na Watumishi wote wa Umma ambao wako katika mihimili mitatu (3) inayounda Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, yaani Serikali, Bunge na Mahakama.

        Viongozi wote wanaowajibika na Sheria ya Maadili ya Viongozi wa Umma Na. 13 ya Mwaka 1995 wanatakiwa kutia saini Tamko la Ahadi ya Uadilifu kwa Viongozi wa Umma na kurejesha kwa Kamishna wa Maadili kabla ya tarehe ya mwisho  ambayo ni tarehe 28 Februari, 2016. Wakuu wa Wizara, Taasisi na Idara au sehemu husika wahakikishe Viongozi waliopo sehemu zao wanatia saini katika tamko hilo.

        Kwa kuzingatia Misingi ya Maadili iliyoainishwa katika Ibara ya 132 ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ya mwaka 1977 na masharti ya Sheria ya Maadili ya Viongozi wa Umma Na. 13 ya mwaka 1995 Viongozi wa Umma wanapaswa kuzingatia viwango vya juu vya Maadili, uzingatiaji wa maadili utakuza  utu, uwazi, uadilifu, uwajibikaji, maendeleo ya nchi na kuimarisha imani ya wananchi kuhusu dhana ya Utawala Bora kwa ujumla.

Jaji (Mst.) Salome S. Kaganda

KAMISHNA WA MAADILI

No comments: