Wednesday, January 13, 2016

MAHAKAMA KUU YA TANZANIA YAKABIDHI MSAADA WA VYAKULA NA VITU MBALIMBALI KWA MAHABUSU YA WATOTO DAR

Mkuu wa Kitengo cha Habari na Mawasiliano Mahakama Kuu ya Tanzania Bw. Nurdin Ndimbe (kushoto) akimkabidhi Afisa Mfawidhi wa Mahabusu ya Watoto jijini Dar es salaam Bw. Ramadhan Yahaya (kulia) msaada wa vyakula na vitu mbalimbali vilivyotolewa na Mahakama Kuu ya Tanzania leo.
Mkuu wa Kitengo cha Habari na Mawasiliano Mahakama Kuu ya Tanzania Bw. Nurdin Ndimbe (kushoto) akishirikiana na Afisa Mfawidhi wa Mahabusu ya Watoto jijini Dar es salaam Bw. Ramadhan Yahaya (kulia) kupakua msaada wa vyakula na vitu mbalimbali vilivyotolewa na Mahakama Kuu ya Tanzania leo.
Afisa Mfawidhi wa Mahabusu ya Watoto ya jijini Dar es salaam Bw. Ramadhan Yahaya (kulia) akipakua msaada wa vyakula na vitu mbalimbali vilivyotolewa na Mahakama Kuu ya Tanzania leo jijini Dar es salaam. Anayeshuhudia kushoto ni Mkuu wa Kitengo cha Habari na Mawasiliano Mahakama Kuu ya Tanzania Bw. Nurdin Ndimbe
Mkuu wa Kitengo cha Habari na Mawasiliano Mahakama Kuu ya Tanzania Bw. Nurdin Ndimbe (kushoto) akiagana na Afisa Mfawidhi wa Mahabusu ya Watoto ya jijini Dar es salaam Bw. Ramadhan Yahaya (kulia) mara baada ya kutoa msaada wa vyakula na vitu mbalimbali. 

                           (Na. Aron Msigwa- Dar es salaam)

Jamii imeaswa kujenga utamaduni wa kuwasaidia watu na makundi yenye mahitaji maalumu hususan wafungwa walio magerezani na wasiojiweza  ili kudumisha upendo na kuyafanya makundi hayo kujiona yanathaminiwa katika jamii.

Wito huo umetolewa leo jijini Dar es salaam na Mkuu wa Kitengo cha Habari na Mawasiliano Mahakama Kuu ya Tanzania Bw. Nurdin Ndimbe wakati akikabidhi msaada wa vyakula na vitu mbalimbali kwa Mahabusu ya Watoto ya jijini Dar es salaam vilivyotolewa na Mahakama Kuu ya Tanzania kama zawadi yao ya mpya 2016.

Bw. Ndimbe amesema Mahakama Kuu ya Tanzania imetoa msaada wa vitu mbalimbali vikiwemo Mchele, Sabuni, Vinywaji, Chumvi, Unga wa Ngano, Unga wa Sembe, Mchele ,Sukari na Mafuta ya kupikia  kwa Mahabusu hao kuonyesha Upendo na namna Mahakama hiyo inavyowathamini watoto hao.

Ameongeza kuwa Mahakama Kuu ya Tanzania imetoa msaada huo kwa lengo la kujenga mahusiano mema baina yake na watoto hao ili waendelee kuipenda na kuwa na mtazamo chanya juu ya utendaji wake.

‘ Nimekuja kukabidhi msaada huu kwa niaba ya Mahakama Kuu ya Tanzania kwa Mahabusu hii ya Watoto ikiwa ni zawadi yao ya mwaka mpya, lengo letu ni kujenga mahusiano mema kati yetu Mahakama na watoto hawa wajue kuwa tunasaidia jamii katika masuala mbalimbali’’ Amesema Bw. Ndimbe.

Kwa upande wake Afisa Mfawidhi wa Mahabusu hiyo Bw. Ramadhan Yahaya akizungumza mara baada ya kupokea msaada huo ameishukuru Mahakama Kuu ya Tanzania kwa uamuzi wake wa kuwakumbuka Mahabusu hao.

Amesema kitendo cha Mahakama Kuu ya Tanzania kuwapatia msaada huo kimewapa faraja watoto hao na kuwafanya wajione wanathaminiwa na kupendwa na Mahakama hiyo.

Ametoa wito kwa Taasisi na Mashirika mengine kuiga mfano huo ulioonyeshwa na  Mahakama  Kuu ya Tanzania ili kudumisha upendo miongoni mwa makundi ya watu wenye mahitaji maalum.

No comments: