Wednesday, November 20, 2013

MAUAJI DAR; MTU MMOJA AUA, AJERUHI NA KUJIUA KWA RISASI

mauajiPolisi wakikagua gari walilokuwa wakisafiria watu wanne kabla ya kushambuliwa kwa risasi na mtu alitajwa kuwa jina la Gabriel Munisi aliyedaiwa kuua watu wawili na yeye kujiua baada ya kujeruhi wengine jana asubuhi jirani na Club ya Wazee, Ilala, jijini Dar es Salaam. Picha ndogo polisi wakikagua silaha iliyotumika.Picha na Silvan Kiwale 
Dar es Salaam. Mfanyabiashara wa magari, Gabriel Munisi (35), jana alijiua baada ya kumuua mtu mmoja na kujeruhi wengine watatu jijini Dar es Salaam katika tukio linalohusishwa na wivu wa mapenzi.
Munisi, ambaye alikuwa mkazi wa Mwanza, aliwapiga risasi watu watatu akiwamo mchumba wake, Christina Alfred katika Mtaa wa Bungoni Wilaya ya Ilala, Dar es Salaam.
Baada ya kumpiga risasi mchumba wake huyo na kudhania kwamba amemuua, inadaiwa kwamba Munisi aliendelea kuwamiminia risasi watu wengine na kumuua mdogo wake Christina, Alpha (22).
Katika tukio hilo, Christina na mtu anayedaiwa kuwa mchumba wake mpya, Francis Shumila wamelazwa katika Hospitali ya Taifa ya Muhimbili baada ya kujeruhiwa. Mama yake Christina, Helen Alfred amelazwa katika Hospitali ya Amana baada ya kujeruhiwa pia.
Kamanda wa Polisi Mkoa wa Ilala, Marieta Minangi alisema Munisi alikutwa na bastola moja, magazini mbili na yalikutwa maganda 14 ya risasi zilizotumika na risasi mbili ambazo zilikuwa hazijatumika.
Tukio hili limetokea mwezi mmoja baada ya mwandishi wa habari wa ITV, Ufoo Saro kujeruhiwa kwa risasi na mzazi mwenzake, Anthery Mushi.
Katika tukio hilo, Mushi alijiua baada ya kumuua mama mzazi wa Ufoo na inaaminika pia tukio hilo lilisababishwa na masuala ya mapenzi.
Lilivyotokea
Mashuhuda waliokuwapo katika tukio hilo walisema mauaji hayo yalitokea saa 1.15 asubuhi baada ya Munisi kufika Ilala Bungoni na kwenda katika Klabu ya Wazee iliyo jirani na eneo yalipotokea mauaji na kunywa supu kabla ya kusogea karibu na lango la nyumba anakoishi mchumba wake.
Mmoja wa majirani, Noel Gerald alisema alimuona Munisi akiwa amesimama karibu na lango la nyumbani kwa kina Christina.
Alisema baadaye waliona gari aina ya Toyota Hilux, Surf, likitoka katika lango la nyumba hiyo na mara walimuona Munisi akimwamuru dereva ashushe kioo lakini alikataa na kudai kwamba ndipo alipoamua kuwapiga risasi waliokuwamo kwenye gari hilo.
Alidai kuwa Munisi alipiga risasi nane mfululizo huku akiwa analizunguka gari hilo na kwamba alimpiga dereva ambaye baadaye alifahamika kuwa ni Shimula. Imeelezwa kuwa majeruhi huyo ni raia wa Kenya na ni rubani wa ndege.
“Katika gari lile walikuwemo watu watatu ambao ni Christina, Helen na Shimula, ambaye alikuwa ndio dereva huku marehemu Alpha akiwa getini na Munisi alimpiga risasi ya kifua,” alidai Gerald.
Shuhuda huyo alidai kwamba Munisi aliendelea na mashambulizi yake kwani magazini ya kwanza ilipomaliza risasi katika bastola yake, aliongeza nyingine na kumfuata mama yake Christina ambaye pia alikuwa ndani ya gari hilo, na kumpiga risasi mkononi. Alidai kwamba alipona baada kutoka na kukimbilia uvunguni mwa gari.
Alisema baada ya kufanya mauaji hayo, Munisi aliamua kujipiga risasi ya kifuani na kufariki papo hapo akiwa amekaa karibu na lango hilo.
Ilidaiwa kwamba Shimula na Christina walikuwa wanaelekea Uwanja wa Ndege wa Mwalimu Julius Nyerere kuelekea Visiwa vya Cyprus.
Uhusiano wa Christina na Munisi
Rafiki wa Munisi aliyejitambulisha kwa jina la Samwel Alex alisema Christian alikuwa mchumba wa Munisi na walikuwa wamepanga kuoana.
Alisema Munisi baada ya kuwa na wasiwasi na mchumba wake ndipo alipoamua kumpigia simu mama mzazi wa Christina na kumwambia kuwa amesikia mwanaye yupo hapo Dar es Salaam lakini alikataa na kumweleza kuwa amesafiri kwenda Moshi.
“Ninawafahamu kwa muda mrefu, Christina alikuwa anafanya kazi Barclays Bank na Munisi ni mchumba wake wa muda mrefu kwani alikuwa anajulikana hata kwa ndugu zake wote,” alisema Alex.
Hospitali ya Amana
Mkuu wa Kitengo cha Dharura Hospitali ya Amana, Dk Christopher Mzava alisema wamepokea majeruhi watatu wanawake wawili na mwanamume mmoja pamoja na maiti mbili ya mwanamke na mwanamume.
Dk Mzava alisema kati ya majeruhi hao mmoja amelazwa Hospitali ya Amana na wawili walipelekwa Hospitali ya Taifa ya Muhimbili. Msemaji wa Aminiel Eligaesha alisema hospitali hiyo ilipokea maiti mbili moja ya mwanaume ambaye jina lake halikufahamika na nyingine ya mwanamke, aliyefahamika kwa jina la Alpha.
Pia alisema walipokea majeruhi wawili, Helen na Shimula, ambaye amelazwa katika Taasisi ya Tiba ya Mifupa Muhimbili (Moi), wote wakiwa na majeraha makubwa ya risasi.
CHANZO: MWANANCHI

No comments: