Thursday, November 21, 2013

BABU SEYA, PAPII KOCHA WASHINDWA TENA, WAREJESHWA JELA MAISHA

MSOTO WA BABU SEYA, PAPII KOCHA!
Ile hukumu ya rufaa ya mwanamuziki Nguza Viking na mwanaye Johnson Nguza 'Papii Kocha' imewarejesha tena jela maisha baada ya hoja za serikali za kukazia hukumu kuzidi zile za upande wa utetezi.
Babu Seya na Papii Kocha walihukumiwa kifungo cha maisha jela mwaka 2004 baada ya kupatikana na hatia ya ubakaji na kuwanajisi watoto wa Shule ya Msingi, Mashujaa, Sinza jijini Dar ambapo wamekuwa wakikata rufaa mara kwa mara lakini wakagonga mwamba.
Hukumu hii ya rufaa ndiyo ya mwisho kusikilizwa huku wakiwa wamepitia msoto karibia miaka kumi sasa wakitaka kujinasua.
Babu Seya na wanawe walidaiwa kutenda makosa 10 ya kubaka watoto hao wa shule ya msingi waliokuwa na umri kati ya miaka sita na minane.
Pia mahakama iliwatia hatiani kwa makosa mengine 11 ya kulawiti watoto wa kike wenye umri huohuo kati ya Aprili na Oktoba 2003.
Juni 25, 2004, Hakimu Mkuu Mkazi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu, Dar, aliwatia hatiani Babu Seya na wanaye kwa kupatikana na hatia ya kubaka na kulawiti.
Januari 27, mwaka 2005, Jaji wa Mahakama Kuu Kanda ya Dar es Salaam, Thomas Mihayo alitupilia mbali rufaa yao iliyokuwa ikipinga hukumu iliyotolewa na aliyekuwa Hakimu Mkuu Mkazi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu, Addy Lyamuya ambaye aliwatia hatiani kwa makosa yote waliyokuwa wameshitakiwa nayo Juni 25, mwaka 2004.
Awali mwaka 2004, baada ya kukutwa na hatia katika kesi hiyo, Babu Seya, Papii Kocha na wakili wao Mabere Marando walikata rufaa ya pili ambayo ilitupiliwa mbali.
Mwaka 2010 waliomba tena rufaa ambayo marejeo yake yalisikilizwa na kutolewa hukumu Februari 2010 baada ya  mahakama hiyo kuridhia hukumu ya kifungo cha maisha kwa Babu Seya na Papii Kocha huku ikiwaachia huru watoto wawili wa Babu Seya, Nguza Mbangu na Francis Nguza.
Mwaka huu, Babu Seya, Papii Kocha na wakili wao Marando waliwasilisha maombi ya kupitiwa upya kwa rufaa ya hukumu yao ya kifungo cha maisha jela ili waachiwe huru lakini wakagonga mwamba baada ya hoja za serikali za kukazia hukumu ya kifungo kuzidi zile za upande wa utetezi.

( PICHA NA HABARI: RICHARD BUKOS/GPL )

No comments: