Tuesday, November 12, 2013

AIRTEL KUKABILIANA NA CHANGAMOTO ZA ELIMU NCHINI

Meneja masoko wa Kampuni ya simu za mkononi ya Airtel kanda ya kusini na mkoa wa Morogoro Aminata Keita akimkabidhi Mwalimu Mkuu Msaidizi wa shule ya sekondari ya Chalinze iliyopo mkoani Pwani baadhi ya vitabu vilivyotolewa na Kampuni ya simu za mkononi ya Airtel kwa shule hiyo. Wanaoshuhudia katikati ni Mwalimu Mkuu wa shule hiyo Bw. Emmanuel Kahabi pamoja na msimamizi wa bodi ya shule hiyo Bw. Mzee Madeni.
 **********
Kampuni ya simu za mkononi ya Airtel Tanzania imeamua kupambana na changamoto zinazoikabili sekta ya elimu nchini kwa kuzisaidia shule mbalimbali za sekondari kupata miundombinu ya kufundishia na vifaa vya kujifunzia.

Airtel  kupitia mradi wake wa shule yetu imewanufaisha wanafunzi wa shule ya sekondari Chalinze iliyopo mkoani Pwani baada ya kukabidhi vitabu vya masomo ya sayansi vyenye thamani ya shilingi milioni tano kwa shule hiyo.

Akizungumza wakati wa kukabidhi vitabu hivyo, Meneja masoko wa Airtel kanda ya kusini na mkoa wa Morogoro Aminata Keita alisema vitabu hivyo vitatumika katika kuongeza kiwango cha uelewa na kukuza ufaulu kwa wanafunzi wa shule hiyo ambao walikuwa na tatizo la uhaba wa vitabu.

“Vitabu hivi vitatumika kukuza ufaulu kwa wanafunzi maana wanafunzi wataweza kujisomea kwa urahisi na kufuatilia masomo kwa ukaribu zaidi” alisema Aminata.

Aliendelea kwa kusema msaada huo wa vitabu ni sehemu ya mpango mkakati wa kuzisaidia shule za kata zinazolalamikiwa kufanya vibaya katika mitihani yao ya kitaifa.

“Tumetoa vitabu vya masomo ya sayansi tukijua kabisa wanafunzi wengi hushindwa masomo hayo kwa sababu mbambali ikiwemo upungufu wa zana za kujifunzia ila nina imani mradi huu wa shule yetu utaziwezesha shule za kata kufanya vizuri kwenye mitihani ya kitaifa” alisema Aminata.

Kwa upande wake mkuu wa shule ya sekondari Chalinze, Bw. Emmanuel Kahabi alisema upatikanaji wa vitabu utarahisisha kazi ya ufundishaji kwa wanafunzi na pia wanafunzi wataweza kuelewa kiurahisi maana zana za kufundishia zinapatikana.

“Tofauti na awali wanafunzi wengi walikuwa wanatumia kitabu kimoja kujisomea ila kwa sasa tuna vitabu vingi hii itatusaidia kufundisha kwa urahisi na wanafunzi kuelewa kwa urahisi vilevile. Pia itapunguza utoro shuleni kwani wanafunzi wataweza kujisomea kwa nafasi. Tofauti na ilivyokuwa awali ambapo wanafunzi wengi walikuwa wakitumia kitabu kimoja,” alisema Kahabi.
Kwa upande wao wanafunzi wa shule ya sekondari Chalinze waliishukuru Airtel kwa msaada huo wa vitabu na kusema kupatikana kwa vitabu hivyo kutawawezesha kumudu kujisomea hata kwa muda wa ziada.

No comments: