Tuesday, January 27, 2015

WATANZANIA WASHIRIKI MAONESHO YA SANAA-MASCUT OMAN

1
Sehemu ya Juu ya Msikiti wa Pili kwa ukubwa duniani “Masjid Sultan” ambayo Taa yake inayoonekana kwa juu  ina uzito wa Tani nane ikiwa imebeba Balbu 2220. Watanzania Wanaoshiriki Maonesho ya Kimataifa ya Sanaa na Utamaduni walienda kutembelea Msikiti huo kujifunza zaidi.
Picha zote-Faki Mjaka-Mascut Oman
2
3
Wafanyakazi wa Msikiti wa Pili kwa ukubwa duniani “Masjid Sultan” wakijibu maswali na kutoa ufafanuzi kutoka kwa Watalii mara baada ya kumaliza kutembelea msikiti huo. Watanzania Wanaoshiriki Maonesho ya Kimataifa ya Sanaa na Utamaduni nchini Oman nao walienda kutembelea Msikiti huo kujifunza zaidi.
5
Wageni na Baadhi ya Watanzania Wanaoshiriki Maonesho ya Kimataifa ya Sanaa na Utamaduni nchini Oman wakiwa Sehemu ya mbele (Qibla) ya Msikiti wa Pili kwa ukubwa duniani “Masjid Sultan”. Msikiti huo umefanywa kama  Kivutio cha Watalii na kujifunza. Watanzania hao walienda kutembelea Msikiti huo kujifunza zaidi.
7
Sehemu ya nje ya Msikiti wa Pili kwa ukubwa duniani “Masjid Sultan”. Msikiti huo umefanywa kama  Kivutio cha Watalii na kujifunza ambapo Watanzania Wanaoshiriki Maonesho ya Kimataifa ya Sanaa na Utamaduni nchini Oman waliutembelea Msikiti huo kujifunza zaidi.
…………………………………………………………………….
Faki Mjaka-Mascut Oman
Taasisi za Kidini nchini Tanzania zimeshauriwa kujenga Nyumba za Ibada zitakazokuwa huru kwa Mtu yeyote kuzitembelea na kujifunza ili kuzidisha upendo na mshikamano miongoni mwa jamii.
Kufanya hivyo kutasaidia kupunguza chuki na misimamo mikali ya kidini inayoweza kutokea miongoni mwa Jamii husika.
Ushauri huo umetolewa na Watanzania wanaoshiriki Maonesho ya Kimataifa ya Sanaa na Utamaduni baada ya kutembelea Msikiti Mkubwa wa Sultan Qabus uliopo Mascut nchini Omani.
Msikiti huo wa pili kwa Ukubwa Duniani umefanywa kama kivutio cha Utalii na Uwekezaji ambapo Wenyeji na Wageni kutoka Mataifa mbalimbali hupata nafasi ya kuutembelea na kuuliza chochote kwa Wafanyakazi wake.
Watanzania hao wamesema kuna mengi ya kujifunza baada ya kutembelea Msikiti huo ambayo yanaweza yakasaidia sana iwapo yataigwa nchini Tanzania.
Mmoja ya Watanzania hao Fred Halla amesema nchini Tanzania Nyumba za Ibada hugeuzwa kuwa sehemu ya kwenda kufanya Maombi na kuondoka kwa Waumini wa dini husika jambo ambalo haliwaunganishi vyema Watanzania.
Amesema umefika wakati kwa Taasisi za Dini kuzifanya Nyumba za Ibada kama kimbilio la watu wa dini Tofauti kwenda kujifunza utamaduni na dini kwa usahihi wake jambo ambalo linaweza kuzidisha upendo zaidi.
“Kule kwetu ni Ajabu Muislamu kwenda Kanisani au Mkristo kwenda Msikitini lakini Katika Msikiti huu unaingia unapotaka na kuuliza chochote na unapata majibu..kwa hili unakuta unapata ukweli wa dini husika kinyume na unavyosikia Mtaani” Alisema Fred.
Amesema alikuwa anaamini kuwa Waislam ndio ambao wanaruhusiwa kuingia Msikitini tu lakini amebaini kuwa Msikitini anaweza kuingia Mtu yeyote na kuuliza chochote ilimradi kafuata sheria.
 Kwa upande wake Mkuu wa Utawala Ubalozi wa Tanzania nchini Oman Abdallah Kilima amesema mfano wa Miskiti kama huo wa Sultan Qabus unaweza ukatumika pia kama njia ya kupunguza Misimamo Mikali na uelewa mbaya wa dini.
Amesema ni vyema pia Tanzania kuwe na utamaduni unaoruhusu Nyumba za Ibada kuwa sehemu ambayo Muumini wa Dini yeyote anaweza kwenda na kuuliza kwa uhuru kama ilivyokuwa kwa Masjid Sultan.
“Kuna mambo mengi watu wanaaminishwa kuwa Misikitini Kuna hili na lile au Kanisani kuna hivi na vile lakini mtu anapopata fursa ya kwenda na kujionea na kuuliza maswali anaondoka akiwa amepata majibu sahihi na kuridhika kama Sisi tulivyopata nafasi hiyo” Alisema Kilima. 
Msikiti huo wa pili kwa ukubwa duniani ulijengwa kwa muda wa Miaka sita kutoka mwaka 1995 hadi 2001 ambapo miongoni mwa maajabu yake ni kuwa na Taa kubwa yenye uzito wa Tani 8 na balbu 1220.
Aidha Msikiti huo wenye huduma Tofauti ikiwemo kumbi za kufanyia mikutano,Kituo cha Taarifa, pia unauwezo wa kuchukua Waumini 10,000 kwa wakati mmoja na Maegesho ya Magari 4,000 kwa pamoja.

No comments: