Saturday, January 24, 2015

HATIMAYE WAZIRI WA NISHATI NA MADINI, PROFESA SOSETER MUHONGO AJIUZULU

Waziri wa Nishati na Madini, Profesa Sospeter Muhongo akiongea na wanahabari ofisini kwake leo.
Hatimaye Waziri wa Nishati na Madini, Profesa Sospiter Muhongo amejiuzulu leo jijini Dar es Salaam.
Waziri Muhongo amechukua uamuzi huo leo ofisini kwake mbele ya waandishi wa habari.
Jinsi sakata la Escrow lilivyozungumzwa Bungeni
Kujiuzulu kwa Muhongo kumetokana na maazimio ya Kamati ya Bunge  ya Hesabu za Serikali chini ya Mhe. Zitto Kabwe ilitokana na sakata la ufisadi wa Akaunti ya Escrow ambapo zaidi ya shilingi bilioni 306 zilichukuliwa kiholea Benki Kuu ya Tanzania na kusababisha mjadala mzito ndani na nje ya Bunge.
Ukaguzi maalum uliofanywa na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG)  na uchuguzi wa Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (Takukuru) kwenye akaunti hiyo, ulifanywa na ripoti zikatolewa na bunge, likajadili na kufikia tamati kwamba kuna kodi ya umma iliibwa.
Kwa vile suala hili liligusa utendaji wa viongozi wa ngazi za juu serikalini pamoja na wanasiasa wengine,  bunge lilitaka kuyumba kutokana na kupendeleana licha ya ukweli kwamba fedha zilizochukuliwa ni nyingi sana .
Mhe. Muhongo alipokuwa Bungeni wakati wa sakata hilo
Ripoti ya Kamati ya Bunge ya Hesabu za Serikali (PAC), chini ya Uenyekiti wa Zitto Kabwe ilipitia kwa ufasaha ukaguzi wa Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali,(CAG)  na uchunguzi wa Takukuru wakatoa ripoti yao na uthibitisho wa kutosha kuwa kuna (aliyekuwa) Mwanasheria Mkuu wa Serikali, Jaji Frederick Werema, Waziri wa Madini na Nishati, Profesa Sospiter Muhongo pamoja na watendaji wengine serikalini wamehusika kwa njia moja au nyingine na upotevu wa fedha hizo za Escrow ama kwa kukusudia ama kwa kutojua, kitu ambacho kilielezwa kuwa ni uzembe.
Rais Jakaya Kikwete alichukua uamuzi wa kumfuta kazi Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Profesa Anna Tibaijuka  kutokana na madai kuwa alichotewa shilingi Bilioni 1.6  zilizotoka katika akaunti hiyo ya Escrow.
Mhe. Anna Tibaijuka
Rais Kikwete alisema Profesa Muhongo alikuwa amemuweka kiporo. Hata hivyo, Watanzania wengi wakati wa kikao cha bunge liliopita walishangazwa kuona baadhi ya wabunge kukaza misuli ya shingo zao na kutetea wizi ili wahusika wasiwajibishwe. Wengine walipingana na ripoti ya CAG.
Wakati wa kikao hicho cha Bunge aliyekuwa Mwanasheria Mkuu wa Serikali, Jaji Fredrick Werema alidaiwa kutaka kumpiga Mbunge wa Kigoma Kusini, David Kafulila ambaye ndiye aliyeanzisha mjadala wa sakata hilo bungeni.
Aliyekuwa Mwanasheria wa Serikali, Jaji Werema
Vyombo vya habari vikatangaza kuwa kama siyo kuzuiwa na mawaziri, Jaji Werema angezua tafrani bungeni kutokana na kitendo chake cha kutaka kumpiga mbunge huyo  kutoka NCCR-Mageuzi, David Kafulila.
Ilidaiwa kuwa tafrani hiyo ilitokea baada ya Mwenyekiti wa Bunge, Mussa Azzan Zungu kuahirisha kikao cha Bunge hadi jioni ya siku hiyo, ikiwa ni muda mfupi baada ya Werema na Kafulila kurushiana maneno bungeni baada ya jaji kuchukizwa na kitendo cha mbunge huyo kijana kumwita mwizi, akijibu mapigo baada ya mbunge huyo kuitwa tumbili (na mwanasheria mkuu huyo wa nchi).
Waliomzuia Jaji Werema asizipike baada ya kumzunguka inadaiwa ni baadhi ya mawaziri ambao walimsindikiza hadi nje ya Ukumbi wa Bunge.

Jaji Werema pia alituhumiwa kumtishia kifo Kafulila ambaye alilalamika bungeni. Ikadaiwa kuwa jaji huyo alimtolea maneno hayo ya vitisho mbunge huyo kwenye viunga vya bungeni mjini Dodoma baada ya bunge kuahirishwa.
Mhe. David Kafulila
Jaji Werema alinukuliwa na vyombo vya habari akidaiwa kumwambia Kafulila: "I will take your head, unless you apologize," ikimaanisha atamkata kichwa iwapo hatamwomba msamaha!

Kufuatia tishio hilo Kafulila akajihami kwa kuiandikia barua ya madai ya kutishiwa maisha ofisi ya spika wa bunge, huku nakala ya barua hiyo akiipeleka kwa Mkuu wa Jeshi la Polisi Tanzania, IGP Ernest Mangu na nakala nyingine ameipeleka kwa kamanda wa polisi mkoa wa Dodoma.
Hili ni tukio baya sana ambalo limeingia katika rekodi. Werema pia alijiuzulu kutokana na kashfa hiyo.

No comments: