Tuesday, January 27, 2015

TRA YATOA SEMINA YA HIMAYA MOJA YA FORODHA KWA TUME YA MIPANGO

001
Naibu Katibu Mtendaji wa Ofisi ya Rais, Tume ya Mipango na Mkuu wa Kongane ya Biashara ya Kimataifa na Ushirikiano wa Kiuchumi, Bw. Paul Sangawe (Kushoto) akizungumza wakati wa ufunguzi wa Semina ya Himaya Moja ya Forodha jijini Dar es Salaam.
002
Mtaalamu wa Masuala ya Forodha kutoka TRA, Bw. Stambuli Myovela (Kulia) akizungumza wakati wa Semina ya Himaya Moja ya Forodha (Single Customs Territory) kwa watumishi wa Ofisi ya Rais, Tume ya Mipango.
003
Baadhi ya watumishi wataalamu wa Ofisi ya Rais, Tume ya Mipango wakifuatilia kwa umakini mawasilisho kuhusu Himaya Moja ya Forodha (Single Customs Territory) katika semina iliyoandaliwa na Mamlaka ya Mapato nchini (TRA).
004
Naibu Katibu Mtendaji (Huduma za Jamii na Masuala ya Idadi ya Watu), Ofisi ya Rais, Tume ya Mipango, Bibi Florence Mwanri (Kushoto) akichangia mada wakati wa Semina ya Himaya Moja ya Forodha (Single Customs Territory) kwa watumishi wa Ofisi ya Rais, Tume ya Mipango
005
Bw. Elykedo Ngonyani ambaye ni Mchumi Mwandamizi (Sekta za Uzalishaji) akichangia mada wakati wa Semina ya Himaya Moja ya Forodha (Single Customs Territory) kwa watumishi wa Ofisi ya Rais, Tume ya Mipango.
………………………………………………….
Na Saidi Mkabakuli
Mamlaka ya Mapato nchini (TRA) imetoa semina juu ya Himaya Moja ya Forodha (Single Customs Territory) kwa watumishi na viongozi waandamizi wa Ofisi ya Rais, Tume ya Mipango.
Akizungumza katika ufunguzi wa Semina hiyo, Naibu Katibu Mtendaji wa Ofisi ya Rais, Tume ya Mipango na Mkuu wa Kongane ya Biashara ya Kimataifa na Ushirikiano wa Kiuchumi, Bw. Paul Sangawe amesema kuwa semina hiyo ina lengo la kuhakikisha kuwa kuna uelewa wa pamoja kuhusu utaratibu huo kwa watumishi wa umma na watanzania wote.
“Lengo la semina hii ni kupata ufahamu wa kutosha kuhusu mambo mbalimbali yanayoendelea, ili kuweza kushauri Serikali ipasavyo katika masuala mbalimbali ya kisera katika Mtangamano wa Jumuiya ya Afrika ya Mashariki,” alisema Bw. Sangawe.
Akiwasilisha mada juu ya Mfumo wa Himaya Moja ya Forodha kwa watumishi, Mtaalamu wa Masuala ya Forodha, Bw. Stambuli Myovela alisema kwamba mfumo huo unaainisha utaratibu wa Mzunguko Huru wa Biashara, Usimamizi wa Mapato, na Mfumo wa Kisheria.
Bw. Myovela aliongeza kuwa kwa mujibu ya mfumo uliokubalika ni kwa kila Nchi Wanachama zitakushanya mapato yake ya kodi. Aidha, kwa bidhaa zinazopitia Nchi moja kuelekea katika Nchi nyingine wanachama (Transit Goods), Nchi Wanachama zimekubaliana kuwa nchi husika bidhaa zinapokwenda itakusanya mapato yake na kuifahamisha mamlaka ya forodha mizigo ilipoingilia katika Jumuiya kwa ajili ya kuruhusu bidhaa kuondoshwa.
Akieleza namna ya utendaji kazi wa mfumo huo, Bw. Myovela aliongeza: “Baada ya kuthibitisha kuwa kodi imelipwa, mizigo itasafirishwa kutoka kituo cha kwanza cha forodha chini ya usimamizi wa Mamlaka ya Forodha kwenda nchi ambayo mizigo hiyo imekusudiwa kutumika ndani ya Jumuiya. Mfumo maalum wa ufuatiliaji kielektroniki (Electronic Cargo Tracking System) utatumika kuhakikisha mizigo inafika salama katika nchi iliyokusudiwa katika Jumuiya.”
Mfumo wa Himaya Moja ya forodha uliridhiwa na Baraza la Mawaziri la Jumuiya ya Afrika Mashariki katika Mkutano wake wa 28 ambapo kwa pamoja Mawaziri hao waliridhia kuwa na Mpangokazi unaoainisha masuala ya kutekeleza katika kipindi cha miezi sita ili kuwezesha kuanzishwa kwa Himaya Moja ya Forodha ifikapo mweizi Juni, 2014.

No comments: