Monday, May 23, 2016

ZANTEL KUWEKEZA DOLA MILIONI 10 KUIMARISHA HUDUMA ZA MAWASILIANO NCHINI PAMOJA NA KUSAMBAZA MTANDAO WA 4G

Mkurugenzi Mtendaji wa Zantel, Benoit Janin akizungumza na waandishi wa habari kuhusiana na mkakati wa uboreshaji wa mtandao unaofanywa na kampuni yake. Anayetazama kulia ni Mkuu wa Zantel upande wa Zanzibar, Mohamed Mussa.
Mkurugenzi Mtendaji wa Zantel, Benoit Janin akisisitiza jambo wakati akizungumza na waandishi wa habari kuhusiana na mkakati wa uboreshaji wa mtandao unaofanywa na kampuni yake. Anayetazama kulia ni Mkuu wa Zantel upande wa Zanzibar, Mohamed Mussa, na kushoto ni Mkurugenzi wa Masoko wa Zantel upande wa Zanzibar, Ibrahim Attas.
Mkuu wa Zantel upande wa Zanzibar, Mohamed Mussa akisisitiza jambo wakati akizungumza na waandishi wa habari kuhusiana na mkakati wa uboreshaji wa mtandao unaofanywa na kampuni yake. Anayetazama kushoto ni Mkurugenzi Mtendaji wa Zantel, Benoit Janin.

Kampuni ya simu inayoongoza visiwani Zanzibar, Zantel, imewekeza jumla ya dola milioni 10 za kimarekani ili kuimarisha huduma zake za mawasiliano nchini.Mpango huo unajumuisha kubadilisha mfumo mzima wa mawasiliano kwa kubadilisha vifaa vilivyokuwepo na kuweka mitambo mipya kwa madhumuni ya kuimarisha mawasiliano ya simu na kuongeza kasi ya mtandao.

Akizungumza na waandishi wa habari visiwani humu, Afisa Mtendaji Mkuu wa Zantel, Bwana Benoit Janin alisema kuimarisha huko katika huduma za simu na mtandao kwa upande wa Zanzibar ndio kilikuwa kipaumbele cha kwanza cha kampuni ya Zantel.‘Kampuni ya Zantel imeanza safari mpya kabisa yenye lengo la kuimarisha na kurudisha nafasi ya mtandao wa Zantel katika ubunifu na kutoa huduma bora visiwani hapa’ alisema bwana Janin.Bwana Janin pia alisema uboreshaji wa huduma za Zantel ni mpango endelevu na katika kipindi kifupi kijacho, Zantel itaendelea kufunga vifaa vipya hali ambayo itawafanya wateja waweze kuwasiliana kwa bei nafuu na bila ya bughudha.

‘Maboresho haya yamelenga kuhakikisha tunakuza na kuimarisha teknolojia ya mawasiliano ikiwa ni pamoja na kutoa huduma za kipekee na kutekeleza ahadi yetu ya kuendelea kuongoza katika kutoa huduma bora kwa wateja wetu’ alisema Bwana Benoit.Janin pia alielezea mpango wa kampuni ya Zantel kuboresha huduma ya EzyPesa kwa kurekebisha mfumo mzima ili uweze kuhimili mawakala wengi na kuongeza huduma za ndani ya mfumo huo. Katika kipindi kifupi pia kampuni ya Zantel pia imefanikiwa kuondoa mtandao wa 2G na kuweka mtandao wa 3G, sambamba na kuzindua rasmi mtandao wa kasi wa intaneti wa 4G mjini Unguja. 

‘Nina furaha kubwa jinsi utekelezaji wa mikakati yetu unavyoendelea wa kuboresha huduma zetu ambao utawapa wateja wetu nafasi ya kufurahia huduma zetu na pia kuwapunguzia gharama za mawasliano huku tukukidhi mahitaji ya wateja wetu kwa wakati huu na siku zijazo’ alisema Janin. Bwana Janin pia alisema tayari matatizo ya mawasiliano ya huduma za 3G yameshatatuliwa kwa kutumia mkonga wa fiber katika ya maeneo ya Unguja na Pemba.

‘Tumefanikiwa kuyatatua matatizo madogo madogo katika mji mkongwe kwa kuweka vifaa ambavyo vimesaidia sana kuondoa msongamano wa mawasiliano majumbani na katika sehemu za wazi’ alisema Janin. Kampuni ya Zantel ambayo ilizindua huduma ya mtandao wa 4G katika mji wa Unguja mwezi uliopita pia imefanikiwa kufikisha mawasiliano kwa asilimia 80% ya watanzania kutoka asilimia 40% waliyokua wanawafikia awali.

No comments: