Sunday, May 15, 2016

KIWANDA CHA BIA SERENGETI CHAPIGWA FAINI

Naibu Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa raisi Muungano na Mazingira Mh.Luhaga Mpina akipata maelezo jinsi gani kiwanda hicho kinavyochuja maji kwa njia ya kisasa kabisa kwaajiri ya matumizi na uzalishaji kiwandani hapo.
S2Naibu Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa raisi Muungano na Mazingira Mh.Luhaga Mpina wa kwanza kushoto,katikati aliyevaa kanzu ni mbunge wa Temeke(CUF)Mh.Abdallah Mtolea wakitembezwa sehemu mbalimbali za kiwandani hapo mara baada ya kufanya ziara ya kushtukiza.
S3Naibu Waziri Wa nchi Ofisi ya Makamu wa raisi Muungano na Mazingira Mh.Luhaga Mpina(katikati) akipata maelezo kutoka kwa Afisa mazingira wa kiwanda cha serengeti Bw.Simon Peter mara baada ya kufanya ziara ya kushtukiza kiwandani hapo.
………………………………………………………………………………………………….
Na Mwandishi wetu-Dar es Salaam
Kiwanda cha bia aina ya serengeti kilichopo chang’ombe wilaya ya Temeke jijini Dar es salaam kimepigwa faini ya shillingi za kitanzania millioni kumi na sita(16)na Baraza la usimamizi wa mazingira Nchini(NEMC)baada ya kutokutimiza masharti ya sheria ya mazingira ya mwaka(2004)na kanuni zake.
Uamuzi huo umefikiwa baada ya  Naibu Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa raisi Muungano na mazingira Mh.Luhaga Mpina kupata malalamiko kutoka kwa wanainchi wanaozunguka maeneo ya kiwanda hicho na kuainisha uchafuzi wa mazingira yanayowazunguka wananchi hao na kuhatarisha  usalama wa afya zao,ambapo ilimlazimu naibu waziri kufanya ziara ya kushtukiza  kiwandani hapo,huku akiambatana na Wakurugenzi kutoka Baraza la usimamizi wa mazingira nchini(NEMC)na kujionea uharibifu huo.
Mh.Mpina  ameagiza kiwanda hicho kulipa faini hiyo na kurekebisha miundo mbinu hiyo ndani ya siku arobaini na tano kusiwepo tena na utiririshaji maji machafu na yenye kemikali kali za sumu ambayo yanatoa harufu mbaya inayohatarisha afya  za wakazi wa chang’ombe wilaya ya temeke.
Pia mkurugenzi wa mazingira Bw. Boniventure Baya ametoa siku saba kwa kiwanda hicho kiwe kimelipa faini hiyo vinginevyo hatua kali za kisheria zitachukuliwa kutokana na kwamba wamekua wakikaidi maagizo yanayotolewa na Baraza hilo la mazingira nchini(NEMC)na kuwataka kufanya hivyo haraka iwezekanavyo baada ya kukiuka sheria ya utunzaji mazingira ya mwaka(2004) na kutokutimiza masharti waliyopewa takribani miaka miwili iliyopita.
Naye mbunge wa Temeke(CUF) Mh.Abdallah Mtolea alisema kiwanda hicho kimekua na mahusiano mabaya na wananchi wanaozunguka  maeneo jirani na kiwanda hicho hivyo kupelekea kuwa na mgogoro wa muda mrefu na uongozi  kiwandani hapo na  kumuomba Naibu waziri kutatua tatizo hilo ambalo limekua likifanywa kwa makusudi na na uongozi wa kiwanda hicho ilihali wanajua madhara ya wanayoyapata wananchi.
Aidha kwa upande wake afisa mazingira wa kiwanda hicho Bw.Simon Peter alipinga vikali tuhuma hizo ambazo zimeelekezwa katika kiwanda hicho na kusema uongozi wa kiwanda hicho unafanya kila jitihada ili kuweza kutatua kero hiyo na si kweli kwamba hawashughulikii tatizo hilo la mazingira jirani na wakazi hao.
Kwa upande wao wananchi kupitia kwa Bi.Emanuela Peter,walisema hiyo ni kero kubwa sana kwao ambapo imekuwa ikiwalazimu kuyahama makazi yao hasa wakati wa kipindi cha masika ambapo maji ya mvua na yale ya kiwanda huchanganyikana na kujaza uchafu wote majumbani mwao kutoka kiwandani na kuhatarisha afya zao hivyo kuhamia kwenye nyumba za kulala wageni kwa muda,hivyo wameiomba serikali kuangalia kwa makini na kuweza kulipatia ufumbuzi.
Vilevile Mh.Luhaga alifanya ziara ya kushtukiza katika kiwanda cha Cement Wazo kilichopo Tegeta wilaya ya kinondoni jijini Dar es salaam,hata hivyo hakuweza kukutana na kiongozi yeyote wa kiwanda hicho kwa madai kua walikua nje ya mkoa wa Dar es salaam,aidha Mh.Mpina alitoa tamko la serikali kuwa,serikali ya awamu ya tano haina uadui na wafanyabiashara pamoja na wawekezaji kama inavyozaniwa na watu wengine,bali inachotaka ni kufuatwa kwa Sheria,taratibu na kanuni kama inavyostahili.

No comments: