Tuesday, June 07, 2016

SERIKALI KUUNDA CHOMBO CHA KUDHIBITI UPANDAJI WA KODI ZA NYUMBA ZA KUPANGA






Na Daudi Manongi-MAELEZO

Katibu Mkuu Wizara ya Ardhi,Nyumba na Maendeleo ya Makazi Dkt Yamungu kayandabila amesema kuwa serikali iko mbioni kuunda chombo cha kudhibiti upandaji wa kodi za nyumba za kupanga.Dkt Kayandabila ameyasema hayo leo hii jijini Dare s Salaam alipokuwa akizungumza katika kipindi cha asubuhi cha Power Breakfast kinachorushwa na Clouds Fm.

“Sisi kama serikali tumesikia kilio cha wapangaji na tuko mbioni kumaliza tatizo hili kwa kuunda chombo kitakachodhibiti upandaji wa kodi hizi za nyumba kiholela,tumeshapokea kesi nyingi sana kutoka kwa wananchi na hivyo tumejipanga kulitatua kabisa tatizo hili”Alisema Dkt Yamungu.

Aidha katibu mkuu huyo amewaasa wapangaji wa nyumba za kupanga kuhakikisha wanakuwa na mikataba ya kisheria yenye makubaliano ya pande zote mbili kupunguza migongano isiyokuwa ya kilazima na kushauri kama watashindwa kumudu gharama za mwanasheria wanaweza kuwatumia wenyeviti wa serikali za mitaa kama mashaidi katika kusaini mikataba yao.

Awali ya yote Dkt Yamungu alizungumzia kukamilika kwa Sera ya nyumba ambayo iko mbioni kukamilika ikizungumzia masuala haya yote na kwa kiasi kikubwa sera hii itapunguza migogoro mingi ya masuala ya nyumba kwa ujumla.

Mwaka huu mwezi wa nne Waziri wa Ardhi,Nyumba na Maendeleo ya Makazi Mhe.William Lukuvi aliweka wazi Bungeni nia ya serikali kutungwa kwa sheria itakayounda chombo cha kudhibiti upandaji wa kodi za nyumba za kupanga. 

No comments: