Wednesday, June 22, 2016

WAKALA YA SERIKALI MTANDAO KUFANYA ZIARA YA KUTEMBELEA TAASISI ZA SERIKALI

Meneja wa Habari, Elimu na Mawasiliano toka Wakala wa Serikali Mtandao Bi Suzan Mshakangoto akifafanua jambo kwa waandishi wa habari (hawapo pichani) kuhusu mpango wa taasisi yake kutembelea wateja wake ambao ni taasisi za Umma ikiwa ni sehemu ya maadhimishi ya wiki ya Utumishi wa Umma. 
Na Eliphace Marwa - Maelezo

Wakala wa Serikali Mtandao (eGA) imeandaa utaratibu wa kutembelea wateja wake ambao ni taasisi za umma ili kusikiliza na kutatua changamoto zinazo tokana na huduma wanazotoa,huduma hizo ni pamoja na mfumo wa barua pepe unaorahisisha mawasiliano serikalini.

Hayo yamesemwa na Meneja wa Habari, Elimu na Mawasiliano wataasisi hiyo Bi Suzan Mshakangoto, alipokuwa akiongea na waandishi wa habari ofisini kwake mapema hii leo jijini Dar es Salam na kutaja baadhi ya taasisi 34 zitakazoanza kutembelewa kuanzia tarehe 22 Juni hadi Juni 23.

Alizitaja baadhi ya taasisi hizo kuwa ni pamoja na Ofisi ya Raisi Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Ofisi ya Waziri Mkuu Sera, Bunge,Kazi, vijana, Ajira na Walemavu, Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo na Makazi, Wizara ya Elimu,Sayansi Teknolojia na Ufundi, Wizara ya Habari,utamaduni Sanaa na Michezo, Wizara ya kilimo, Mifugo na Uvuvi, Wizara ya Mambo ya Nje Ushirikiano wa Afrika Mashariki Kikanda na Kimataifa.

Aidha aliongeza kuwa huduma nyingine zinazotolewa na wakala wa serikali ni pamoja na uhifadhi wa mifumo ya tovuti za serikalini, utoaji huduma za simu za mikononi, Uratibu wa mitandao serikalini, Ugawaji wa masafa ya internet, huduma za ujumbe mfupi wa maandishi (sms) pamoja na utengenezaji wa mifumo ya tovuti na usajili anuani za tovuti.

Hiyo ni kutimiza Agizo la Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais Menejimenti ya Utumishi wa Umma Mh.Angela Kairuki la kutaka kila Wizara, wakala na Taasisi za Serikali katika kipindi cha Wiki ya Utumishi wa Umma kukutana na wateja wao na kusikiliza kero walizonazo ili kuweza kuzipatia ufumbuzi, aidha kauli mbiu ya mwaka huu ni, “Uongozi wa Umma kwa Ukuaji jumuishi kuelekea katika Afrika tunayoitaka”.

Kila taasisi itatembelewa na wataalam wawili wa wakala wa serikali watakao sikiliza maoni na kutoa msaada wa kiufundi na ushauri wa kitaalamu katika kutatua changamoto mbali mbali zinazojitokeza juu ya huduma mbali mbali zinazotolewa na wakala.

No comments: