Wednesday, June 22, 2016

CCM YAWASILISHA GHARAMA ZA UCHAGUZI KWA MSAJILI WA VYAMA LEO

Mkaguzi Mkuu wa Ndani wa CCM, Stanslaus Mamilo akimkabidhi vielelezo vya CCM vya matumizi ya Uchaguzi mkuu uliopita, kwa Mwangalizi wa Ofisi ya Msajili wa Vyama, Mkuu wa Masijala Galasia Simbachawene, leo jijini Dar es Salaam. (Picha na Bashir Nkoromo).

Na Bashir Nkoromo

CHAMA Cha Mapinduzi (CCM) leo kimewasilisha kwa Msajili wa Vyama, hati zake za gharama ya Uchaguzi Mkuu uliofanyika mwaka jana, na kuwa chama cha pili kufanya hivyo kwa mujibu wa sheria za uchaguzi nchini.

Ujumbe wa CCM uliongozwa na Mkaguzi Mkuu wa Ndani wa CCM, Stanslaus Mamilo na Mwanasheria wa CCM Adamson Sinka na kuwasilisha hati na vielelezo vya matumizi hayo kwa Mwangalizi wa Ofisi ya Msajili wa Vyama, Mkuu wa Masijala Galasia Simbachawene.

Akikabidhi hati na vielelezo hivyo Mamililo alisema, CCM imelichukua swala hilo umuhimu mkubwa ndiyo sababu imefanya hivyo ndani ya wakati kwa kuwa mda wa kuwasilisha matumizi ya gharama za uchaguzi kwa wagombea na vyama vyote vilivyoshiriki uchaguzi huo uliofanyika Oktoba 2015, ni Juni 25, 2016.

"Sisi hatuwezi kuwa kama vyama vingine kwa kuwa ni Tasisi kubwa ambayo  haina budi kufuata kanuni, taratibu na sheria za nchi hasa ikizingatiwa kwamba CCM ndiyo chama tawala hivyo lazima kionyeshe mfanomzuri ili kiendelee kuwa chama cha kuigwa ", alisema Mamilo.Mamililo aliwasilisha hati na vielelezo vya matumizi ya Chama na wagombea wa nafasi mbalimbali  kupitia CCM ikiwemo Urais, Wabunge na Madiwani.

Akizungumza baada ya kukabidhiwa hati na vielelezo hivyo, Galasia alisema, katika vyama vyote vilivyoshiriki katika uchaguzi mkuu uliopita ni CCM na ACT-Wazalendo ndivyo ambavyo tayari vimekamilisha bila shuruti sheria ya  kuwasilisha gharama zake za uchaguzi.

Alisema, uwasilishaji wa gharama hizo ni muhimu sana kwa kuwa ni suala la kisheria, kwa kuwa vyama au wagombea wanaoshindwa kutimiza sheria hiyo watachukuliwa hatua ikiwemo kupelekwa makahamani ambako wakipatikana kwa upande wa Chama kitafungiwa kushiriki uchaguzi wowote utakaofuatia na kwa upande wa wagombea mhusika atatozwa faini ya sh. milioni 2, au kifungo cha mwaka mmoja jela au vyote pamoja.

Kulingana na Sheria ya Uchaguzi, chama kinatakiwa kisitumie ghara inayozidi sh. bilioni 17, na kikilazimika kuzidi kiwango hicho kisididi zaidi ya asilimia 15 ya kiwango kinachotakiwa, huku kwa upande wa wagombea kiasi kinachotakiwa ni sh. bilioni saba na kwa wabunge sh. milioni 33 hadi 88 kulingana na mazingira ya jimbo.

No comments: