Tuesday, June 21, 2016

WANANCHI WA CHASIMBA KUWENI WAVUMILIVU MTAKULA MBIVU

Na Jacquiline Mrisho-MAELEZO

Baada ya mtafaruku mkubwa kutokea katika Kijiji cha Chasimba kilichopo katika Wilaya ya Kinondoni Jijini Dar es Salaam na kuwaacha wakazi wa eneo hilo katika hali ya sintofahamu juu ya maisha yao ya siku zijazo, wakazi wa eneo hilo wamepata ahueni baada ya Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi Mhe.Willium Lukuvi kuingilia kati na kutoa suluhu ya mtafaruku huo.

Mgogoro huu baina ya wananchi wa Kijiji cha Chasimba na mwekezaji wa Kiwanda cha Saruji cha Twiga, Bw. Alfonso Rodriguez kilichopo Wazo Hill ambao ulianza takribani miaka 15 iliyopita baada ya Mkurugenzi huyo kugundua kuwa wananchi wamevamia eneo lake na kujenga makazi yao.

Hayo yalitokea baada ya kiwanda hicho kushindwa kuilinda mipaka yake kwa muda mrefu na kusababisha wananchi kujenga maeneo hayo na kukaa kwa muda mrefu sana hali iliyowapelekea kujiona kama wana haki na eneo hilo na kukataa kuhama.

Mkurugenzi Msaidizi Usanifu wa Miji na Uendelezaji Upya Maeneo wa Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Bi. Immaculata Senje alisema kuwa eneo hilo ni mali ya mwekezaji wa Kiwanda hicho."Ni ukweli usiofichika kuwa eneo hili la Chasimba ni mali ya mwekezaji na ana hati ya mwaka 1957 aliyopewa na Wizara yetu inayoonyesha ukubwa na mipaka ya eneo lake kwahiyo wananchi ndio wavamizi wa eneo hilo".anakiri Bi. Senje.

Mgogoro huo ulileta tafrani kubwa baada ya Waziri wa Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi William Lukuvi kutoa agizo kuwa wananchi waliojenga katika eneo hilo wahame mara moja na kwenda eneo ambalo wamepangiwa na Wizara ambapo takribani wakazi 30 waligoma kuondoka katika eneo hilo na kuamua kwenda mahakamani kudai haki yao, hatua ambayo haiukupata suluhu ya mgogoro.

Ili kuwasaidia wakazi wa Chasimba, Waziri Lukuvi aliamua kuingilia kati kwa kufanya mazungumzo ya amani na muwekezaji wa kiwanda hicho ambapo alimuomba Mkurugenzi huyo kuwaachia wakazi wa Chasimba sehemu hiyo kwa makubaliano maalumu watakayoafikiana.

No comments: