Wednesday, June 29, 2016

MAKAMU WA RAIS AWATAKA WAKUU WA WILAYA NA MIKOA KUKAMILISHA ZOEZI LA MADAWATI KABLA YA JUNE 30.
















Na Daudi Manongi,MAELEZO

Makamu wa Rais Mhe Samia Suluhu amewataka wakuu wa wilaya na mikoa kuhakikisha wanamaliza zoezi la upatikanaji wa madawati kwa shule za msingi na sekondari.

Mhe. Suluhu ameyasema hayo leo Ikulu Jijini Dar es Salaam wakati wakuu wa wilaya na mikoa walipokuwa Ikulu wakila kiapo cha maadili ya viongozi kabla ya kwenda kuapishwa na wakuu wa mikoa yao.

Aidha amewaagiza viongozi hao kusoma alama za nyakati kwa kuangalia makosa ya waliokuwepo kabla yao ili kuhakikisha hawarudii makosa yaleyale.

Mhe.Suluhu pia amesema kuwa Serikali haitaki kusikia wananchi wanalia njaa na hivyo wakuu wa wilaya wahakikishe chakula kinapatikana katika maeneo yao kwani hilo ni jukumu lao.

Aliongeza kuwa wakuu wa wilaya wana majukumu makubwa ya kuhakikisha wananchi wanapata huduma zote za muhimu katika maeneo yao kwani wananchi wana mategemeo makubwa juu yao.

Aidha ameagiza wakuu wa Wilaya hao kufanya kazi karibu na Maafisa Tarafa ili kujua kero za wananchi na kuzifanyia kazi kwa kasi ili wananchi wafaidike na maendeleo yawafikie kwa haraka.

Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (Tamisemi), George Simbachawene ivi karibuni aliwaagiza wakua wa wilaya na mikoa kuhakikisha wanatimiza agizo la Rais John Pombe Magufuli kuhakikisha hakuna mwanafunzi atakayekaa chini kwa uhaba wa madawati kufikia June 30,2016.

No comments: