Sunday, April 10, 2016

KIWANDA CHA KARATASI MUFINDI KUTOZWA FAINI YA SHILINGI MILIONI ISHIRINI KWA UCHAFUZI WA MAZINGIRA

8
Mkuu wa Wilaya ya Mufindi Bw. Jowika Kasunga akitoa ufafanuzi kwa Naibu Waziri Ofisi ya Makamu wa Rais Mazingira na Muungano Mh. Luhaga Mpina (kushoto) wa namna ambavyo wilaya imeelekeza Kiwanda cha Mbao cha Sao Hill na Green Resources Limited cha Mufindi kutunza Mazingira, (katikati) ni Mkurugenzi Mtendaji wa Kiwanda hicho Bi Roselyne Mariki.
9
Naibu Waziri Ofisi ya Makamu wa Rais Muungano na Mazingira Mh. Luhaga Mpina akiangalia kipande cha gogo ambacho ni moja ya waste product  (taka) inayotoka katika kiwanda cha Sao Hill and Green Resources Limited  baada ya uzalishaji wa mbao na nguzo ambayo taka hiyo ya gogo pia hutumika kutengenezea gundi.
10
Naibu Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Rais Muungano na Mazingira akitoa maelekezo kwa uongozi wa kiwanda cha Sao Hill and Green Resources Limited, wa namna ya kuondosha taka za nguzo (hazipo pichani) zilizozagaaa katika eneo la kiwanda hicho..alipofanya ziara ya viwanda, ukaguzi wa usafi wa mazingira na kupanda miti Mkoani Iringa leo.(Picha zote na Evelyn Mkokoi wa Ofisi ya Makamu wa Rais)
………………………………………………………………………………..
Kiwanda cha kuzalisha karatasi cha Mufindi Paper Mills kilichopo wilayani Mufindi Mkoani Iringa, kimetozwa faini ya shilingi milioni ishirini kwa kukiuka sheria ya usimamizi wa mazingira ya mwaka 2004 na kanuni zake.
Faini hiyo inayotakiwa kulipwa katika kipindi kisichozidi wala kupungua wiki mbili imetokana na ukiukwaji wa sheria ya mazingira kwa utiririshaji wa kemikali hatarishi kwa viumbe hai na mazingira katika mto kigogo, na maeneo ya jirani na vijiji vinavyo uzunguka mto huo.
Akimfafanulia Naibu Waziri Ofisi ya Makamu wa Rais Muungano na Mazingira Mh. Luhaga Mpina alipofanya ziara kiwandani hapo, Mratibu wa Baraza la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira (NEMC) kanda ya Nyanda za Juu kusini. Bw. Godlove Mwaisojo, ameeleza kuwa moshi, vumbi na majitaka yanayotoka katika mitambo ya kiwanda hicho baada ya uzalishaji wa karatasi, yamezidi viwango vya sheria kwa kuwa na kemikali hatarishi kwa baiyonuwahi na mazingira na hivyo Baraza limekuwa likielekza mara kadhaa uongozi wa kiwnda hicho kurebisha mfumo wa utoaji taka bila utekelezaji wa aina yoyote.
Bw. Mwamsojo alimueleza Mh Naibu Waziri Mpina Kuwa, kiwanda hicho kimeshauriwa na baraza kuhakiki ubora wa hali wa hewa, na mitambo yao ya uzalishaji lakini kilikaidi.
Kwa Upande wake Mkuu wa Wilaya ya Mufindi Bw. Jowika Kasunga, amemueleza Mh. Naibu Waziri Mpina kuwa, pamoja na ukiukwaji wa utekelezaji wa sheria ya mazingira unaofanywa na kiwanda hicho, pia menejimenti ya kiwanda hicho imekuwa na mgogoro mkubwa  wa ardhi na mahusiano mabaya  na wanakijiji wanaozunguka kiwanda hicho, na kuwa karibia hekta elfu kumi na nne za misitu  zilizopo katika eneo hilo, zipo katika mgogoro wa muda mrefu baina ya wanakijiji na muwekezaji huyo, ambapo mgogoro huo umepelekea eneo hilo kutotumika  na wanakijiji wala muwekezaji huyo.
Mh. Naibu Waziri Mpina, ameutaka uongozi wa mkoa wa Iringa kwa kushirikiana na wizara husika kutatua mgogoro huo wa ardhi, ili uzalishaji wa rasilimali ya misitu uendelee kwa manufaa ya taifa.
Kwa upande wake Mkuregenzi Mtendaji wa kiwanda hicho Bw. CHOUDARY kutoka barani Asia, alikubaliana na adhabu hiyo na kuhaidi kurekebisha mitambo ya uzalishaji katika kiwanda hicho kwa kipindi kisichozidi wiki mbili.
Ziara ya Naibu Waziri Mpina, pia ilihusisha ukaguzi wa mazingira katika kiwanda cha uzalishaji mbao,nguzo na nishati cha Sao Hill and Green Resources Limited, cha Mjini Mufindi na kujionea namna ambavyo kiwanda hicho kinavyokabiliana na athari zitokanazo na mabadiliko ya tabia nchi kwa kumiliki mashamba makubwa ya misitu katika vijiji vya Mapanda na Achimbile, na kufanya biashara ya hewa ukaa.

No comments: