Wednesday, August 12, 2015

Dk Slaa aikana akaunti ya twitter inayomzushia mazito


Wakati kukiwa na taarifa zinazosambaa mtandaoni zikimuhusisha Dk Willibrod Slaa na akaunti ambayo imekuwa ikitoa msimamo wake wa kujitenga na shughuli za siasa pamoja na Ukawa, katibu huyo mkuu wa Chadema amekanusha taarifa hizo akisema hajawahi kuwa na akaunti ya twitter.
Hii ni mara ya pili kwa Dk Slaa kuzungumza na gazeti hili, lakini akikatakaa kufafanua mambo mbalimbali yanayohusu sakata lake na Chadema, akiahidi kuwa kufanya hivyo baadaye, huku akiweka bayana kuwa hajawahi kuwa na akaunti ya twitter.
Dk Slaa, aliyekuwa anatajwa kuwa mgombea urais wa Chadema, hajaonekana hadharani katika matukio makubwa ya kichama tangu Chadema na Ukawa walipomkaribisha waziri mkuu wa zamani, Edward Lowassa na kumteua kuwa mgombea urais anayeungwa mkono na vyama vinne vinavyounda umoja huo.
Mara ya mwisho kuonekana kwenye shughuli za chama hicho ni katika kikao cha Kamati Kuu wakati Lowassa alikaribishwa kufanya majadiliano na kujibu hoja za wajumbe.
Lakini baada ya hapo Dk Slaa hakuonekana wakati wa kutambulishwa kwa Lowassa kwa waandishi wa habari, tukio la kuchukua na kurudisha fomu za urais ndani ya chama na tukio la juzi la kuchukua fomu za urais kutoka Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC).
Wakati hayo yakiendelea, kuna akaunti ya twitter yenye jina la “Dr Willibrord Slaa” ambayo imekuwa ikitoa kauli mfululizo zikiwa na ujumbe mbalimbali unaoendana na mazingira aliyomo sasa mwanasiasa huyo.
 Agosti 10, kulitumwa ujumbe zaidi mara 10, mmojawapo ukijaribu kuwaaminisha watu kuwa hiyo ni akaunti halisi ya Dk Slaa.
“Ndugu zangu Watanzania, hii ni akaunti yangu rasmi, bila shaka yoyote na naomba ninachoandika hapa kifikishwe kwa Watanzania popote walipo,” unasema ujumbe huo.
Taarifa nyingine zilizotumwa kwenye akaunti hiyo ya twitter ni pamoja na ile iliyoeleza kuwa   Dk Slaa ameomba ulinzi kutoka nchi na mashirika ya kimataifa na atazungumza kupitia runinga na redio pindi atakapopata ulinzi.
Akizungumza na gazeti hili jana, Dk Slaa alisema hajawahi kutuma taarifa yoyote kwenye mitandao ya kijamii.
“Sijawahi ku-operate (kuendesha) kitu chochote kwenye akaunti ya twitter, sina akaunti kama hiyo,” alisema Dk Slaa.
Mbali na kukanusha kumiliki na kuendesha akaunti hiyo, Dk Slaa alirudia kauli yake ya wiki iliyopita kuwa atatoa msimamo wake muda muafaka utakapofika, baada ya kuulizwa swali kuhusu hatma yake ndani ya Chadema na kisiasa kwa ujumla.
“Subira yavuta heri, sasa ili uipate hiyo heri unatakiwa kuvumilia. Kwa hiyo wakati ukifika nitazungumza tu na Watanzania,” alisema.
Alipoulizwa ni wapi alipo kwa sasa, alisema yupo Dar es Salaam anapumzika, lakini akasisitiza kuwa ipo siku ataweka wazi mustakabali wake kisiasa.
Dk Slaa alisema yeye na mke wake Josephine Mushumbusi wanatarajia kusafiri kwenda nje ya nchi katika siku chache zijazo, ingawa hakuweka wazi nchi anayotarajia kuitembelea, lakini akasema atarejea baada ya wiki moja.
chanzo:gazeti la mwananchi
- See more at: http://edwinmoshi.blogspot.com/2015/08/dk-slaa-aikana-akaunti-ya-twitter.html#sthash.asRKVf8G.dpuf

No comments: