Wednesday, February 25, 2015

BENKI YA POSTA TANZANIA (TPB) YABORESHA ZAIDI HUDUMA KWA WATEJA BAADA YA KUJIUNGA KATIKA MTANDAO WA TTCL KATIKA MKONGO WA TAIFA WA MAWASILIANO

PO1
Benki ya Posta Tanzania (TPB) na Kampuni ya Simu Tanzania (TTCL), wamekabidhiana rasmi mradi wa huduma kupitia Mkongo wa Taifa wa Mawasiliano.
Lengo la mradi huu ni kuhakikisha kuwa TPB inatanua wigo wa utoaji huduma zake kwa ufanisi na tija kwa kupitia huduma hii kutoka TTCL. Huduma hii inayopatikana kupitia katika Mkongo wa Taifa wa Mawasiliano una faida ambazo toka mradi huu ukamilike Benki ya Posta Tanzani (TPB) imefaidika ikiwa ni pamoja na kupungua kwa muda wa wateja kusubiria huduma kwenye matawi , kuongezeka kwa ufanisi wa utendaji kazi wa ndani ya benki,  kulinda taarifa za wateja na kampuni kwa ujumla.
 
Makao Makuu na matawi Kumi (10) ya Benki ya Posta Tanzania (TPB) yameunganishwa kwenye mtandao wa TTCL wa MPLS-VPN kupitia kwenye Mkongo wa Taifa wa Mawasiliano, ambao umeongeza wigo wa utoaji wa huduma zilizo bora kwa wananchi walio vijijini na mjini nchi nzima.
Matawi hayo ambayo yameunganishwa katika Mtandao wa TTCL, ni pamoja na  Makao makuu ya TPB, Ofisi za Dar es Salaam, Samora, Kijitonyama, Sam Nujoma na Ubungo. Matawi mengine ni YWCA,Metropolitan, Arusha, Dodoma, Mbeya na Mwanza.
 
Kwa kutambua mageuzi na uhitaji wa teknolojia katika kutoa huduma, Benki ya Posta Tanzania (TPB) iliamua kutekeleza mradi huu kwa lengo la   kuongeza ufanisi  na tija katika  kutoa huduma kwa wateja wake ambao wameenea katika mikoa na wilaya nchini kote.
 
Benki ya Posta Tanzania ni benki inayomilikiwa na Serikali kwa asilimia kubwa, itaendelea kuunganisha matawi yake nchi nzima, yale ya mikoa na wilaya ili kuwafikia watanzania waliowengi wenye mahitaji ya huduma za kibenki.
Benki ya Posta Tanzania (TPB) tunajivunia kuwa benki pekee yenye ofisi mpaka ngazi ya wilaya, yenye kutumia teknolojia ya kisasa, za haraka na nafuu katika kutoa huduma kwa wateja wake.
Tunapenda kuweka wazi kuwa kwa kutumia huduma hii ya Mult- Protocol Label Switching -Virtual Private Network (MPLS –VPN), taarifa za benki na wateja wake zitakuwa salama zaidi.
Pia, TPB inatarajia kuanza kutekeleza awamu ya pili  ya kuunganisha matawi yake 28 nchi nzima kwenye Mtandao wa TTCL, wa MPLS VPN ambao unapitia katika Mkongo wa Taifa wa Mawasiliano ikiwa ni dhumuni la dhati la kuongeza tija katika kutoa huduma. 

No comments: