Friday, March 01, 2013

HOTUBA YA RAIS WA JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA, MHESHIMIWA JAKAYA MRISHO KIKWETE, KWA WANANCHI, 28 FEBRUARI, 2013

Utangulizi
Ndugu wananchi;
Namshukuru Mwenyezi Mungu, mwingi wa rehma, kwa kutujalia uzima na kutuwezesha  kuwasiliana kupitia utaratibu wetu mzuri tuliojiwekea wa kufanya hivyo kila mwisho  wa mwezi. Leo nimepanga kuzungumza nanyi mambo matatu; yaani Mpango wa Amani, Usalama na Ushirikiano wa Jamhuri ya Kidemokrasi ya Kongo, Uhusiano wa Waislamu na Wakristo na Matokeo ya Mtihani wa Kidato cha Nne.
Mpango wa Amani, Usalama na Ushirikiano wa
Jamhuri ya Kidemokrasi ya Kongo

Ndugu Wananchi;
Tarehe 8 Februari, 2013 kule Addis Ababa, Ethiopia niliungana na Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa, Mhe. Ban Ki-Moon, Mwenyekiti wa Kamisheni ya Umoja wa Afrika, Mhe. Nkosozana Dlamini Zuma na viongozi wa nchi 12 za Afrika Mashariki, Kati na Kusini kutia saini Mpango wa Amani, Usalama na Ushirikiano wa Jamhuri ya Kidemokrasi ya Kongo na jirani zake.  Pamoja na Jamhuri ya Kidemokrasi ya Kongo zilikuwepo nchi za Burundi, Rwanda, Uganda, Sudani Kusini, Jamhuri ya Afrika ya Kati, Jamhuri ya Kongo, Angola, Zambia na Tanzania ambazo ni jirani ya Kongo.  Nchi za Ethiopia, Msumbiji na Afrika ya Kusini pamoja na Umoja wa Mataifa na Umoja wa Afrika zilitia saini kama wadhamini.  Ethiopia kwa nafasi yake ya kuwa Mwenyekiti wa sasa wa Umoja wa Afrika na Msumbiji kwa kuwa Mwenyekiti wa Jumuiya ya Maendeleo ya Kusini mwa Afrika (SADC).  Nchi wanachama wa Mkutano wa Ukanda wa Maziwa Makuu ziliwakilishwa na Uganda ambayo ni Mwenyekiti wake wa sasa.  Afrika ya Kusini ilishirikishwa kwa kuwa taifa kubwa na linalotegemewa katika ukanda wetu.
Mpango huu ni jitihada nyingine ya kusaidia Jamhuri ya Kidemokrasi ya Kongo ipate amani ya kudumu.  Kama tujuavyo, tangu mwaka 1997 wakati wa vita vilivyosababisha kuondolewa kwa Rais Mobutu Seseseko mpaka sasa nchi hiyo rafiki na jirani haijapata amani na utulivu wa kudumu.  Kumekuwepo jitihada na mipango kadhaa ya kuleta amani ambayo hata hivyo baada ya muda fulani machafuko hutokea tena na mipango hiyo kuvurugika.  Inakadiriwa kuwa takriban watu milioni 5.4 wamepoteza maisha na watu wengi kuwa wakimbizi ndani na nje ya nchi yao.  Pia kumekuwepo na vitendo vya ukatili dhidi ya wanawake na watoto pamoja na mali nyingi kuharibiwa au kuporwa.
Ndugu Wananchi;

No comments: