Saturday, May 23, 2015

WAWANIA URAIS CCM WAMALIZA ADHABU


Chama Cha Mapinduzi (CCM) kimetangaza kuwaachia huru wanachama wake waliokuwa
wakitumikia adhabu waliyopewa wanachama sita waliokiuka kanuni za
maadili na kupewa Onyo Kali, adhabu iliyodumu kwa kipindi kisichopungua
miezi 12. 
Makada hao wamekuwa huru baada ya Kamati Kuu ya CCM, kupokea na kukubali pendekezo la Kamati ya Usalama na Maadili la kumalizika kwa kipindi cha adhabu kwa wanachama hao
“Kwahiyo adhabu hiyo kwa sasa imemalizika, na wanachama hao wameruhusiwa kuendelea na shughuli zao katika Chama”, amesema Katibu wa NEC, Itikadi na Uenezi, Nape Nnauye, akizungumza na waandishi wa habari  kuhusu yaliyojiri katika kikao cha Kamati Kuu ya CCM kinachoendelea leo mjini Dodoma, chini ya Mwenyekiti wa CCM, Rais Jakaya Kikwete.

SOMA TAARIFA KAMILI KAMA ILIVYOTOLEWA NA NAPE JIONI HII MJINI DODOMA

TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI

Kamati Kuu imepokea na kutafakari taarifa ya Kamati ya Usalama na Maadili ambayo ilipitia adhabu waliyopewa wanachama sita waliokiuka kanuni za Maadili na kupewa Onyo Kali, adhabu iliyodumu kwa kipindi kisichopungua miezi 12.
Wanachama hao sita ni;-
i. January Makamba
ii. Willium Ngeleja
iii. Steven Wasira
iv. Bernard Membe
v. Edward Lowassa
vi. Fredrick Sumaye
Kamati Kuu imepokea na kukubali pendekezo la Kamati ya Usalama na Maadili ya kumalizaka kwa kipindi cha adhabu kwa wanachama hawa. Kwahiyo adhabu hiyo kwa sasa imemalizika, na wanachama hao wameruhusiwa kuendelea na shughuli zao katika Chama.
Hata hivyo Kamati Kuu inawataka wanachama hawa na wale wengine wenye nia ya kugombea Urais kupitia CCM Kuzisoma , Kuziheshimu na Kuzizingatia Kanuni za Maadili za CCM na kanuni zingine zinazoongoza mchakato ndani ya Chama, ili wasikumbwe na adhabu itokanayo na kuzivunja kanuni hizo.
Wale wote wanaotaka kugombea, yaani waliokuwa kwenye adhabu na wengine watakaojiingiza kwenye kampeni mapema na hivyo kukiuka maadili na miiko ya Chama, taarifa za kukiuka kwao zitatumiwa wakati wa kuchuja majina ya wagombea utakapofika.
Taarifa hizo zitatumika katika kuwapima na kuamua iwapo wana sifa za kutosha na wanafaa au hawafai katika kupata uteuzi wa nafasi wanayoiomba.
Imetolewa na;-
Nape Moses Nnauye
Katibu wa Itikadi na Uenezi
22/05/2015

No comments: