Monday, May 25, 2015

SERIKALI YA TANZANIA NA UNESCO KUADHIMISHA WIKI YA UKOMBOZI WA BARA LA AFRIKA

JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA

WIZARA YA HABARI, VIJANA, UTAMADUNI NA MICHEZO





IDARA YA HABARI (MAELEZO)

S.L.P.  8031, Dar es Salaam, Simu: 2110585, 2122771/3, Fax: 2113814, e-mail: maelezopress@yahoo.com

TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI



SERIKALI YA TANZANIA NA UNESCO KUADHIMISHA WIKI YA

UKOMBOZI WA BARA LA AFRIKA NA KUZINDUA MRADI WA NYARAKA ZA URITHI WA TANZANIA



Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kushirikiana na Shirika la Umoja wa Mataifa linalo shughulikia Elimu, Sayansi na Utamaduni (UNESCO) itaadhimisha Wiki ya Ukombozi wa Bara la Afrika kuanzia tarehe 25 hadi 29 Mei, 2015 kwa kufanya maonesho ya picha na kumbukumbu mbalimbali zinazoonesha na kuelezea harakati za ukombozi wa bara la Afrika pamoja na midahalo mbalimbali itakayowahusisha wasomi na baadhi wa watu mashuhuri walioshiriki katika harakati za ukombozi.



Maadhimisho hayo yatatanguliwa na uzinduzi wa Mradi wa Nyaraka za Urithi wa Tanzania (TAHAP) utakaofanyika tarehe 25 Mei, 2015 katika Ukumbi wa Makumbusho ya Taifa jijini Dar es salaam. Mgeni Rasmi katika ufunguzi wa Maadhimisho hayo anatarajiwa kuwa Mhe. Bernard Membe (Mb.), Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa.



Mradi wa Nyaraka za Urithi wa Tanzania unaofadhiliwa na Umoja wa Ulaya kwa kushirikiana na UNESCO ukikamilika unaatarajia kuweka na kutunza  kumbukumbu na nyaraka mbalimbali zinazohusu harakati za ukombozi wa bara la Afrika na ushiriki wa Tanzania kama mwenyekiti wa iliyokuwa Kamati ya nchi za mstari wa Mbele katika kuzikomboa nchi na kuvijengea uwezo vyama vya wapigania uhuru kusini mwa bara la Afrika.



Miongoni mwa matukio muhimu katika maadhimisho hayo ni mdahalo utakaohusu Mchango wa vyama vya Siasa katika harakati za Ukombozi utakaoongozwa na Mhe. Salim Ahmed Salim na Wazungumzaji Wakuu watakuwa ni Prof. Issa Shivji na Mhe. Ibrahimu Kaduma, aliyewahi kuwa Waziri wa Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa.



Mdahalo mwingine Utajikita katika kuangalia "Mchango wa Wapiganaji/Wanajeshi katika harakati za Ukombozi" tarehe 26 Mei, 2015 utakaofanyika Chuo Kikuu Cha Dar es salaam utakaoongozwa na Prof. Penina Mlama na Wazungumzaji Wakuu watakuwa Balozi Dkt. Augustine Mahiga na Brigedia Jenerali Ananias Mwanga.



Tarehe 27 Mei, 2015 kutakuwa na mdahalo mwingine kuhusu "Mchango wa Wanawake katika harakati za ukombozi" utakaoongozwa na Prof. Ruth Meena na wazungmzaji wakuu watakuwa ni Dkt. Alexander Mkulilo na Mhe. Balozi Getrude Mongela (MB). Mdahalo huu utafanyika katika ukumbi wa Nkrumah, Chuo Kikuu Cha Dar es salaam.



Mdahalo kuhusu "Mchango wa vyombo vya habari Wakati wa Harakati za ukombozi" utafanyika Chuo Kikuu  Huria Cha Tanzania tarehe 28 Mei, 2015 na kufuatiwa na  mdahalo kuhusu "Mchango wa Wasanii na Watunzi katika Harakati za Ukombozi" tarehe 29 Mei, 2015 utakaofanyika katika ukumbi wa Makumbusho ya Taifa. Mdahalo huo utaongozwa na Mzee Walter Bgoya. Wazungumzaji wakuu katika mdahalo huo watakuwa Prof. Penina Mlama na Bw. Zahiri Zahoro.



Maadhimisho hayo yatafungwa Rasmi na Mhe. Dkt. Fenella Mukangara, Waziri wa Habari, Vijana, Utamaduni na Michezo tarehe 29 Mei, 2015.



Vyombo vya habari vinaombwa kushiriki kwa kuandika na kutangaza Matukio hayo muhimu katika kutunza kumbukumbu za ukombozi wa bara la Afrika katika mikono ya wakoloni na utawala dhalimu wa Afrika Kusini.


MKURUGENZI IDARA YA HABARI (MAELEZO)

No comments: