Sunday, May 31, 2015

MWIGULU NCHEMBA NAYE ATANGAZA NIA YA KUWANIA URAIS


Mwigulu Nchemba akitangaza nia ya kuwania nafasi ya kugombea Urais kupitia CCM jioni hii mkoani Dodoma.
NAIBU Waziri wa Fedha, Mwigulu Nchemba, ametangaza nia ya kuwania nafasi ya kugombea Urais jioni hii kupitia Chama Cha Mapinduzi (CCM) akiwa katika Ukumbi wa Mwl. Nyerere uliopo kwenye Chuo cha Mipango mkoani Dodoma.
Kauli mbiu ya Mwigulu ni ‘Mabadiliko ni Vitendo Wakati ni Sasa.’
Katika hotuba yake Mwigulu ameanza kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu, wazee, ndugu zake, wananchi wake wa Iramba na wananchi wote waliohudhuria hafla hiyo ya kutangaza nia.
Mwigulu pia amempongeza Rais Kikwete kwa kumuamini na kumteua katika nyadhifa mbalimbali.
Amesema ameamua kutangaza nia akiwa mkoani Dodoma ili kuondoa dhana ya ‘ukwetukwetu’ iliyozoeleka miongoni kwa viongozi. Aongeza kuwa Dodoma ni makao makuu ya taifa na chama chake ndiyo maana amefanya hivyo.
Aidha Mwigulu ameeleza mambo matatu yaliyomsukuma kutangaza nia kuwa ni pamoja na:
-Kutaka Mabadiliko
-Kujua mbinu za mabadiliko
-Utayari wa kufanya mabadiliko.
Pia kiongozi huyo amekemea viongozi wanaochaguliwa kwa mazoea wakisingizia uzoefu kwa kueleza kuwa kiongozi anayechaguliwa kwa mazoea ataongoza kwa mazoea na atafanya kazi kwa mazoea maana uzoefu ni mazoea.
Kiongozi huyo ameeleza jinsi anavyozijua fika shida za Watanzania na umasikini walionao hajausoma kwenye vitabu bali ameishi maisha ya umasikini.
Mwigulu ameeleza pia alivyobeba zege baada ya kumaliza chuo kikuu na mke wake akiwa mama ntilie akiwapikia yeye na vibarua wengine wa ujenzi.

No comments: